Wednesday 17 May 2017

Malima afikishwa kortini kwa kumshambulia askari

Aliyekuwa Naibu Waziri wa fedha na mbunge wa Mkuranga, Adam Kigoma Malima amefikishwa
mahakamani kujibu tuhuma za kumshambulia askari polisi. Malima anashtakiwa pamoja na dereva wake Ramadhani Mohamed Kigwande anayekabiliwa na tuhuma za kujeruhi. Washtakiwa wamesomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicious Mwijage wa
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.  Wakili wa serikali, Mwanaamina Kombakono amedai, Mei 15 mwaka huu huko Masaki katika wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam mshtakiwa Malima alitenda kosa.

Imedaiwa, siku hiyo mshtakiwa Malima alimzuia afisa wa polisi mwenye namba H.7818 PC Abdul kufanya kazi yake ya kumkamata dereva wake Kigwande aliyekuwa amefanya kosa la kumjeruhiJoseph Mwita ambaye ni afisa operation wa
Priscane Business Enterprises.Kombakono ameongeza kuwa, siku na mahali hapo, mshtakiwa Kigwande kwa nia ya kukataa kukamatwa, alimjeruhi afisa operation hiyo (Joseph Mwita) ambaye alikuwa anakamatwa kwa kosa la kupaki gari vibaya na kumsababishia Mwita Majeraha Mwilini. Watuhumiwa wote wamekana kutenda makosa hayo na wako nje kwa dhamana.mahakama imemtaka kila mshtakiwa kuwa na mdhamini mmoja atakaye saini dhamana ya milioni 5. Aidha Mahakama imemtaka kila mdhamini awe na barua ya utambulisho kutoka ofisi yoyote inayotambulika. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Juni 15, mwaka huu ambapo kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi bado haujakamilika.Wakili Kibatala ameieleza mahakama kuwa, tarehe ya kutajwa kwa kesi hiyo atawasilisha pingamizi la awali juu ya mapungufu ya kisheria yaliyopo kwenye shtaka la shambulio linalomkabili Malima Peke yake. Amedai kuwa, katika shtaka hilo maelezo ya kosa na tuhuma hazifanani.

No comments: