Monday 25 August 2014

Mchezaji afa uwanjan baada ya kutupiwa kitu na washabik

Mchezaji kutoka Cameroon Albert Ebosse amefariki dunia baada ya kurushiwa kitu na mashabiki katika mchezo wa ligi nchini Algeria. Ebosse, 24, alithibitishwa kuwa amefariki baada ya kufikishwa hospitali katika eneo la Tizi Ouzou, mashariki mwa mji mkuu, Algiers. Mshambuliaji huyo wa klabu ya JS Kabylie, ambaye alikuwa amefunga goli moja katika mchezo huo waliopoteza kwa 2-1, dhidi ya USM Alger aligongwa na kitu hicho baada ya mpira kumalizika, wakati wachezaji wakiwa wanatoka uwanjani. Wizara ya mambo ya ndani ya nchi imetaka uchunguzi kufanyika mara moja. Haijathibitishwa ni kitu gani hasa alichogongwa nacho, lakini gazeti moja la Algeria limesema mashabiki walikuwa wamekasirishwa na kufungwa na walikuwa wakirusha mawe. Taarifa iliyotolewa na klabu yake imesema :”alikufa kutokana na jeraha la kichwani” baada ya kurushiwa kitu mwisho wa mchezo. Rais wa shirikisho la kandanda barani Afrika, Issa Hayatou ametoa taarifa inayolaani tukio hilo

Wednesday 6 August 2014

Mbeya City kujenga kiwanja cha Kisasa

UJENZI wa Uwanja wa kisasa wa Mbeya City utaanza mwishoni mwa Agosti hii ambapo wataanza kujenga viwanja viwili, kimoja cha mazoezi na kingine cha mechi.
Eneo la uwanja huo utakaoitwa Mbeya City Arena upo lipo Iwambi jijini Mbeya ambapo ni nje kidogo ya jiji hilo na una ukubwa wa hekta mita 5.7.
Katibu Mkuu wa Mbeya City, Emmanuel Kimbe, ameliambia Mwanaspoti akisema: “Mwisho mwa mwezi huu ni lazima tuanze kujenga kwani tayari wananchi wamevuna mazao yao, pia tunasubiri ramani ya uwanja ambayo tumeipa kazi kampuni moja hapa jijini, tanaanza na uwanja wa mazoezi mambo mengine yatafuata hapo baadaye.”
Kuhusu maandalizi ya timu, Kimbe alisema kuwa wamewasilisha majina ya wachezaji wao Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ambapo wataingia kambini Agosti 15 akiwamo Saady Kipanga ambaye inasemekana tayari yupo jijini Mbeya.
Kipanga alikuwa ni miongoni mwa wachezaji ambao walidaiwa kusajiliwa na Simba msimu ujao, lakini dili hilo liliingia mchanga baada ya wajumbe wa Kamati ya Usajili kutokubaliana na usajili wake na hivyo kumsajili Elius Maguli wa Ruvu Shooting.

Evance Aveva amrudisha Mbabe wa Yanga Kundini


Rais wa klabu ya Simba, Evans Aveva  
Jumapili Simba walifanya Mkutano Mkuu wa wanachama ambapo walifanya mabadiliko ya Katiba katika baadhi ya vipengele huku Ibara ya 25 kipengele cha 8(iii) kimeonekana kumrudisha kundini kihalali Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Zacharia Hans Poppe.
Kigogo huyo amekuwa tishio kwa Yanga haswa kutokana na ushawishi wake.
Kabla ya mabadiliko hayo, kipengele hicho ambacho kinahusu viongozi watakaochaguliwa na Mkutano Mkuu wa uchaguzi ni wajumbe watano wa Kamati ya Utendaji, pia Rais atateua wajumbe wengine watano wa Kamati ya Utendaji ambao anaweza kuwabadilisha kwa kadiri anavyoona inafaa.
Kipengele hicho kimeendelea kuelezea kuwa wajumbe hao wa kuteuliwa wanatakiwa kuwa na sifa zile zile wanazotakiwa kuwa nazo wajumbe wa kuchaguliwa na wanachama.
Hivyo katika marekebisho ya kipengele hicho ni kwamba wajumbe watano wa Kamati ya Utendaji watachaguliwa na wanachama, lakini Rais atateua wengine watano wa kamati hiyo ambao anaweza kuwabadilisha kwa kadiri anavyoona inafaa na hawatakiwi kuwa na sifa kama zile za wajumbe wa kuchaguliwa.
Hiyo inamaana kwamba wajumbe hao wa kuteuliwa wanatakiwa kuwa na sifa ya uanachama wa klabu hiyo tu. Tayari Rais wa klabu hiyo, Evans Aveva ameteuwa wajumbe watatu ambao ni Mohamed Nassoro, Salim Abdallah na Musley Saleh hivyo amebakiwa na nafasi mbili za kujaza.
Kwa mamlaka aliyona sasa, Aveva anaweza kutumia nafasi hiyo kumpachika Hans Poppe ambaye hawezi kugombea nafasi yoyote ndani ya Simba kutokana na kubanwa na Ibara ya 26 (4) kinachosema mgombea asiwe aliyewahi kutiwa hatiani kwa kosa la jinai kwa kuhukumiwa kifungo.
Tayari Hans Poppe ambaye ni mmoja wa wanachama wa Simba wenye ushawishi mkubwa alishatamka wazi kuwa hawezi kugombea tena Simba kutokana na kubanwa na kipengele hicho

Zambia yateua Kocha mpya

Timu ya taifa ya Zambia imepata Kocha mpya, Honour Janza aliyechukua nafasi ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo Patrice Beaumelle aliyeondoka mwanzoni mwa juma hili.
Rais wa Shirikisho la soka la Zambia Kalusha Bwalya amesema ni changamoto kubwa waliyonayo lakini wana imani na Janza.
Janza anakutana na kibarua cha kwanza katika michuano ya kufuzu kombe la mataifa ya Afrika ya mwaka 2015.
Zambia iko kundi F na itaikaribisha Msumbiji tarehe 6 mwezi Septemba, kisha itaelekea Cape Verde siku nne baada ya mechi hio.
Chipolopolo imefikia hatua ya kumtafuta mrithi wa Beaumelle baada ya mfaransa huyo kuamua kuungana na aliyekua kocha wa zambia Herve Renard ambaye kajiunga na Ivory Coast.
Bwalya amesema hana hofu kuwa Janza ambaye alikua Mkurugenzi wa ufundi ndani ya shirikisho la soka la zambia atamudu kuipeleka Zambia mbele.

Picha za mwanamitindo wa India zazua balaa Nchini Humo

Picha za wanamitindo zilizopigwa kwenye basi zikionyesha mwanamke akionekana kama anayebakwa na wanaume, zimezua hisia kali kwenye mitandao ya kijamii nchini India.
Watu wengi wamesema kuwa picha hizo zinaonekena kusifu kitendo cha ubakaji kilichomkuta mwanafunzi mmoja mjini Delhi kwenye basi mwaka 2012.
Mwanafunzi huyo ambaye aliga baadaye, alibakwa na genge la wanaume.
Picha za mpiga picha Raj Shetye ambaye alipiga picha hizo, zinaonyesha mwanamke akioenekana kupigania maisha yake akiwa amezuiliwa na wanaume wawili kwenye kiti cha basi.
Ni kitendo ambacho kinaleta hisia kali kwa watu wengi na kumbukumbu za unyama uliotendewa msichana wa shule kwenye basi hadi akafa.
Watu wengi kwenye mitandao ya kijamii wanasema picha hizo ni za kukera na zinatisha .
Bwana Shetye hata hivyo amejitetea akisema picha hizo ni za kuonyesha tu hali inayowakumba wanawawake wengi nchini huo wala sio kuonyesha ubakaji.
Hata hivyo picha hizo ziliondolewa kwenye mtandao huo wa Behance baada ya hisia kali kutoka kwa watumiaji waTwitter na Facebook.
Ubakaji wa msichana huyo aliyekuwa na umri wa miaka 23 ulisababisha maandamano makubwa nchini humo na hata kulazimisha maafisa wakuu kuweka mikakati mipya ya kukabiliana na ubakaji
shirika la utangazaji la Uingereza BBC lilijaribu kumtafuta Bwana Shetye aweze kujieleza kuhusu picha hizo ingawa hatukufanikiwa badli vyombo vya habari vilimnukuu akisema hakua na nia ya kuleta kumbukumbu mbaya kuhusu kitendo cha ubakaji kilichozua hasira kote nchini India.

Reina kutua Bayern Munich

Pepe Reina
Klabu ya Bayern Munich wameukubali mpango wa kumsajili mlinda mlango wa Liverpool, Pepe Reina.
Klabu hiyo ya ujerumani kupitia mtandao wao wa Twitter wameandika, "Mlinda mlango Pepe Reina yuko tayari kuhama kutoka Liverpool kuja FC Bayern kisha vipimo vya afya vitafuata.
Mwispainia huyo amepoteza nafasi yake kama mlinda mlango nambo moja wa Liverpool kutoka kwa Meneja Brendan Rodgers baada ya kumsajili Simon Mignolet ambapo msimu uliopita alikuwa Napoli.

Sunday 3 August 2014

Saady Kipanga asajiliwa kwa mabavu simba

Said Kipanga
SAKATA la usajili wa mshambuliaji wa Mbeya City, Saady Kipanga, kwenda Simba, limechukua sura mpya baada ya viongozi wa klabu hiyo kushindwa kuelewana kwa maelezo kwamba kigogo mmoja amemsajili kibabe bila wenzake  kuridhia.
Awali viongozi wa Kamati ya Usajili kwa ushirikiano na viongozi wengine wa Simba, walikubaliana kufuta usajili wa mchezaji huyo. Lakini baadaye mmoja wa vigogo hao (jina tunalo) aliliibua suala hilo upya juzi Jumatano kwa madai kuwa tayari amemsainisha Kipanga mkataba wa miaka miwili.
Siku hiyo kamati hiyo  ilikutana kujadili mustakabali mzima wa usajili na kufunga kazi hiyo ili kocha apate muda wa kukaa na wachezaji husika, lakini ishu ya Kipanga ikatibua uelekeo wa kikao.  Kikao hicho kiliongozwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Zacharia Hans Poppe.
Suala hilo lilionekana kuwagawa baadhi ya wajumbe wa kamati ambapo walio wengi walionekana kupinga juu ya usajili huo huku wajumbe watatu pekee wenye ushawishi wa kifedha wakiunga mkono. Wajumbe wengi walikuwa wakimtaka Elius Maguli ambaye yupo kwenye orodha ya matakwa ya kocha.
Mbeya City watoa tamko
Uongozi wa Mbeya City umesema kuwa ulipokea barua ya kiongozi mmoja wa juu wa Simba juu ya maombi ya usajili wa Kipanga, Deus Kaseke na Anthony Matogolo na kuwapa masharti ya kutimiza.
Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Emmanuel Kimbe, alisema baada ya kuijibu barua hiyo ya Simba, hawakupokea mwendelezo wowote wa mawasiliano juu ya usajili hivyo wanashangaa kusikia Kipanga kasajiliwa Simba wakati bado ana mkataba wa mwaka mmoja na nusu na klabu hiyo na kama ni kweli watashtaki.
“Kuna barua ilitumwa kutoka Simba na tuliwajibu, lakini hakuna majibu yaliyorudi kutoka kwao, hivyo tunasubiri itakuwaje maana tunasikia tu kuwa wamemsajili, huo utakuwa usajili wa kinyemela na uvunjaji wa kanuni za usajili, sisi tumewasiliana na TFF juu ya hilo.
“Kanuni zipo wazi huwezi kufanya mazungumzo na mchezaji ambaye ana mkataba kuanzia mwaka mmoja na klabu nyingine labda angebakiza miezi sita, wachezaji wetu wanatakiwa kufika kambini, Kipanga ni mmoja wao,” alisema Kimbe.
Kuhusiana na usajili wa Maguli ndani ya Simba, ukombozi inajua kwamba Wekundu wa Msimbazi hao wameshatuma ofa JKT Ruvu. Jana Alhamisi walitarajia kumalizana naye huku uongozi wake ukikiri kupokea barua kutoka Simba.
“Tunakutana viongozi kujadili, lakini hatuwezi kumzuia mchezaji ambaye ameonyesha nia ya kwenda kucheza timu yoyote kwani tukimzuia hatafanya vizuri kwetu, Simba wametuma barua lakini haina ofa yoyote ila tutamruhusu akachezea Simba kwani ndio timu aliyoipenda, naamini tutakubaliana na hatuwezi kuwakomoa kwa kutaka fedha nyingi,”  alisema Msemaji wa JKT Ruvu, Masau Bwire.

Pirre Kwizera amaliza ubishi Msimbazi

UBISHI mkubwa uliokuwa umetawala kwenye usajili wa Simba ni kuhusiana na usajili wa vichwa vitatu, straika Elius Maguli wa Ruvu Shooting, Mrundi Pierre Kwizera wa Afad ya Ivory Coast na kiungo wa zamani wa Msimbazi, Shaaban Kisiga. Ubishi huo umekwisha jana Ijumaa kiulainii na vijana hao tayari wako Msimbazi.
Mrundi Pierre Kwizera wa Afad ya Ivory Coast.
Maguli alikuwa na mkataba wa mwaka mmoja na klabu yake ambayo kwa zaidi ya miezi miwili ilikuwa ikikomaa kwamba hauzwi lakini wamelegea baada ya kuonyeshwa fungu la maana na mabosi wa Simba, Kwizera alitua Dar es Salaam jana jioni na barua mkononi ikithibitisha kwamba yeye ni mchezaji huru na leo Jumamosi asubuhi atasaini mkataba wa miaka miwili na Simba. Lakini Kisiga ambaye ni fundi kwenye kiungo akitokea Mtibwa kama mchezaji huru amerejea Simba kwa rekodi ya kuwa mchezaji mzoefu aliyesajili kwa bei chee zaidi Sh 5 milioni tu na hakuna hata chenji iliyobaki.
Kama ubishi huo hautoshi Simba jana ilifunga hesabu ya wachezaji wa kigeni watakaovaa uzi mwekundu msimu ujao na kufuta kabisa uwezekano wa Emmanuel Okwi na Hamis Kiiza kutua Msimbazi kama mmoja wao akitemwa na Yanga kwani tayari Simba ina vichwa vitano.
Mbali na Kwizera, Simba  ina wachezaji wengine wa kigeni ambao ni Amissi Tambwe (Burundi),  Donald Mosoti (Kenya ), Joseph Owino (Uganda) na Paul Kiongera ambaye amewaahidi viongozi kwamba atamalizana na KCB ya Nairobi wikiendi hii na Jumatatu atatua Msimbazi kusaini mkataba ambao tayari wameshapatana bei kwani wiki iliyopita alikuwa Bongo ambapo alifikia Kijitonyama.
KWIZERA
Kwizera ambaye ni bingwa wa kupiga mipira mirefu na kufunga magoli kwa faulo baada ya kutua jana aliiambia ukombozi kuwa: “ Nimekuja kuwapa ubingwa Simba na kazi yangu kubwa ni kuhakikisha ushindi unapatikana na timu inafunga lakini pia hairuhusu goli kwenye lango letu.
“Mimi ni kiungo na ninapenda kucheza nafasi ya kiungo mkabaji zaidi kuliko ile ya kiungo mshambuliaji na zaidi napendelea kucheza mipira mirefu. Hivyo ninachoomba ni muda kidogo wa kuzowea mazingira lakini pia nataka kucheza Simba kwa mafanikio, niko tayari kwani hata nilivyokuja nimetoka kwenye ligi na naamini sitawaangusha Wanasimba.
“Ninachoomba ni michezo miwili ya kujiweka sawa na kumuonyesha kocha kile nilichonacho, tena nitaonyesha kile nilichojifunza nikiwa Ivory Coast na hii itanifanya niwe na nguvu na kuisaidia Simba. Namjua Tambwe kwani tuliwahi kucheza wote timu ya Taifa ya Burundi, anajua kufunga lakini pia ninafuraha kuwa tayari ninajua jinsi anavyocheza na tena nimeifuatilia Simba kwa zaidi ya misimu miwili na kuiona hivyo sina wasiwasi wa kucheza.
MAGULI NA KISIGA
MAKAMU wa Rais wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ aliwatambulisha wachezaji hao jana. Maguli ambaye alishika nafasi ya pili katika ufungaji bora msimu uliopita akiwa na mabao 14 na Tambwe alikuwa mfungaji bora kwa mabao 16.
Kaburu alisema Maguli amesaini mkataba wa miaka miwili na Kisiga mwaka mmoja.
“Tumekamilisha usajili wa Maguli ambaye kwa muda mrefu tulikuwa tunamhitaji, kamati pia imefanikiwa kumalizana na klabu yake ya Ruvu ambao walikuwa na mkataba naye, watu wanaweza kuona mambo yanaenda taratibu, hayo yote yanatokana na ukweli kwamba tunataka kufanya usajili kwa umakini mkubwa,” alisema Kaburu ambaye ni mzoefu wa mambo ndani ya Simba.
MKUTANO NA SIMBA DAY
Akizungumzia kuhusu Mkutano  Mkuu wa Simba, Kaburu alisema utafanyika kesho Jumapili kama ulivyotangazwa na Rais wake Evans Aveva ambao utafanyika katika Bwalo la Maofisa wa Polisi lililopo Oysterbay jijini Dar es Salaam.
Kaburu alisema Zesco United ya Zambia itacheza nao katika siku ya Simba Jumamosi ijayo kwenye Uwanja wa Taifa.
LOGA ANENA
KOCHA wa Simba, Zdravko Logarusic akishakabidhiwa Paul Kiongera, Saady Kipanga na Elius Maguli atalazimika kubadili mfumo na kuchezesha washambuaji wengi zaidi. Logarusic alisema Kiongera, Maguli na Kipanga si washambuliaji kamili hivyo anaweza kuwachezesha nyuma ya mshambuliaji wake mahiri Mrundi Amissi Tambwe kwa kutumia mfumo wa 4-2-3-1.

Liverpool yasajili kinda toka Bayer Leverkusen

Emre Can Leverkusen Klabu ya Ligi Kuu ya soka ya England – Premier League Liverpool, imemsaini kiungo chipukizi wa Bayer Leverkusen Mjerumani Emre Can mwenye umri wa miaka 20. Uhamisho huo umethibishwa na vilabu viwili
Can ameichezea Leverkusen mechi 39 katika vinyang'anyiro vyote tangu alipojiunga nao msimu uliopita. Can mzaliwa wa Frankfurt, mwenye asili ya kituruki, na anayeweza pia kucheza kama beki, alijiunga na Leverkusen kutokea Bayern Munich msimu uliopita, na kuwasaidia kumaliza katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa Bundesliga na kufuzu pia katika Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Kwingineko, mshambuliaji wa Japan Yuya Osako amejiunga na klabu ya FC Cologne iliyopandishwa daraja katika Bundesliga msimu ujao. Osako mwenye umri wa miaka 24, ametokea klabu ya 1860 Munich. Mshambuliaji huyo, ambaye yuko katika kikosi cha Japan kinachojiandaa kwa dimba la Kombe la Dunia, atasaini mkataba utakaomfikisha Juni mwaka wa 2017.
Mkataba huo umefanyika baada ya nahodha wa Japan Makoto Hasebe kusaini mkataba wa miaka miwili na klabu nyingine ya Bundesliga Eintracht Frankfurt kutoka Nuremberg iliyoshushwa daraja. Klabu nyingine ya Bundesliga iliyofanya biashara ni Hertha Berlin iliyomsajili Mjapan Genki Haraguchi. Haraguchi mwenye umri wa miaka 23, anajiunga na Mjapan mwenzake katika klabu hiyo ya Berlin iliyomaliza katika nafasi ya 11 msimu uliopita.

Usain Bolt aibeba jamaica

Usain Bolt
Bingwa wa mbio za mita 100 duniani Usain Bolt amelisadia taifa lake la Jamaica kufuzu katika fainali za 400 m x 100m hii leo licha ya tishio na kusisitiza kuwa amefurahi kuwa Glasgow.
Bolt amelazimika kukana madai kwamba alitoa matamshi mabaya dhidi ya mashindano hayo,ambapo nusra jamaica ishindwe baada ya mmoja ya wakimbiaji wake katika mbio za 400m X100m kupata jeraha.
Hatahivyo Bolt aliweza kuwasaidia wenzake na kushinda mbio hizo.
Bolt baadaye alikiri kwamba alifikiri kuna tatizo mahala .
Anasema kuwa alikuwa na wasiwasi lakini mwanariadha kimmari wa jamaica aliyeanza mbio hizo na kupata jeraha alimpokeza mwenzake kijiti cha kukimbia.
''Kocha wangu kwa mara nyingi hutuambia tukimbie na uchungu'',alisema Bolt.

Serenget boys wapigwa 4-0

dogo-serengeti 

TIMU ya Taifa ya Tanzania ya vijana chini ya miaka 17, Serengeti Boys imebugizwa mabao 4-0 dhidi ya timu ya Taifa ya vijana wa umri huo ya Afrika kusini maarufu kama Amajimbos katika mchezo wa kuwania kufuzu fainali za vijana za mataifa ya Afrika.
Mechi hiyo rahisi kwa Afrika kusini imepigwa jioni ya leo katika uwanja wa Dobsonville uliopo Soweto na kushuhudia wenyeji wakitoka na furaha.

Saturday 2 August 2014

Maximo ampa majukumu mazito Shadrack Nsajigwa


Kocha mpya wa timu ya vijana ya Yanga, Shadrack Nsajigwa (katikati) akiwaelekeza wachezaji wake pamoja na wachezaji wa timu ya wakubwa, walipokuwa wakifanya mazoezi ya pamoja kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola, Dar es Salaam jana.

Katika hali inayoonekana kuwa na hofu ya  kuchafua rekodi yake mapema Kocha mkuu wa Yanga, Marcio Maximo ameikacha  michuano ya Kagame kwa kumpa jukumu kocha wa timu ya vijana, Shadrack Nsajigwa ‘Fuso’  kuhakikisha anarudi na ubingwa wa Kombe la Kagame.
Maximo ambaye ameinoa Yanga tangu mwezi uliopita aliliambia gazeti hili kuwa ameshagawa timu mbili kwa malengo tofauti, moja iliyo na vijana wengi na baadhi wazoefu itakwenda Kagame na nyingine atabaki nayo yeye kambini Pemba kujiandaa na ligi.
“Nimeshateua timu itakayokwenda Rwanda na itakuwa chini ya kocha Nsajigwa na Leonardo Neiva  wakati nyingine nitabaki nayo mimi na Salvatory ambayo tutakwenda Pemba,  lengo ni kuhakikisha naiandaa timu kikamilifu kwa ajili ya Ligi Kuu.”
Maximo ameamua kuipeleka timu ya vijana kwenye michuano hiyo mikubwa Afrika Mashariki na Kati  itakayoanza Agosti 8,  huku akiongeza wachezaji  sita kutoka timu ya wakubwa.
“Nitaongeza mchezaji mmoja au wawili kati ya  wale walioko Taifa Stars ambaye naye atakwenda kwenye michuano ya Kagame kuongeza nguvu  ingawa siwezi kumtaja ni mchezaji gani kwa sasa,” alisema Maximo.
Katika mazoezi ya wiki hii Maximo alionekana kuiandaa kikamilifu timu itakayoshiriki michuano ya Kagame huku akiamini kuwa itafanya vizuri na kurudi na ubingwa.
Kwa mujibu wa mazoezi hayo wachezaji wa timu kubwa watakaoongozana na timu ya vijana ni Nizar Khalfan, Omega  Seme, Hussein Javu, Rajab Zahir, Said  Bahanuzi na kipa Ali  Mustapha ‘Barthez.’
Yanga imepangwa kundi moja na  Rayon Sports ya Rwanda, Atlabara na KMKM ya Zanzibar.

Mashambulio ya Israel yaua watu zaidi ya 100

Gaza

Maafisa wa matibabu katika eneo la Gaza wanasema kuwa zaidi ya wapalestina 100 wameuawa na makombora ya Israel tangu kukiukwa kwa makubaliano ya kusitisha vita siku ya ijumaa.
Vifo vingi vimetokea katika eneo la Rafah kusini mwa Gaza ambapo wanajeshi wawili wa Israel waliuawa na mwengine wa tatu kudaiwa kutekwanyara baada ya kuvamiwa na wapiganaji wa Hamas.
Kundi la wapiganaji wa kipalestina Hamas limesema kuwa halina habari zozote kuhusu mwanajeshi aliyetoweka Hadar Goldin na kwamba huenda aliuawa katika mapigano.