Friday 20 March 2015

Obama atoa pongezi kwa Benjamin Netanyahu

Rais Obama amemtumia salaam za pongezi waziri mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu kutokana na ushindi uliokipata chama chake katika uchaguzi uliofanyika Jumanne.
Lakini Bwana Obama ameelezea dhamira yake ya kuupatia ufumbuzi mgogoro kati ya Israel na Wapalestina kuwa ni kuunda taifa la Palestina.
Awali Ikulu ya Marekani ilielezea wasiwasi kuhusu ahadi ya Bwana Netanyahu wakati wa kampeni za uchaguzi kwamba asingeruhusu kuundwa kwa taifa la Palestina.
Waziri mkuu wa Israel tangu wakati huo amelegeza msimamo wake, akisema atakubali suluhisho la kuwepo mataifa mawili jirani endapo usalama katika eneo la Mashariki ya Kati utaimarishwa.

Ajali zaendelea kuitesa Tanzania, yaua watu 7

Mchana wa  jana  basi ya RUWINZO DAR kwenda  SONGEA na Basi la IFAKARA EXPRESS yamegongana maeneo ya mikumi. Inasemekana Abiria 7 wamefarik hapo hapo. Tuendelee kuombea Taifa letu .
Image result for ajali ya basi jana  Mwandishi wetu alifanikiwa kuongea na mmoja wa mhanga wa ajali hiyo alisema "Hali halisi ya ajali ni kuwa na mwendo wa kasi dereva wetu tulipofika mikumi majira ya saa 5:30 asubuhi tukitokea dar es salaam kuelekea malininyi-mahenge Gari nililolipanda mimi linaitwa MSANGA line express ambalo linafanya safari zake Dar,ifakara-malinyi tulipofika mikumi mbele yetu kulikuwa na lori lenye namba za usajili  T 299 nalo lilikuwa linatoka dar-iringa dereva wetu alikuwa ana-over take hilo lori kabla hajamaliza kupita hilo lori alikutana  uso kwa uso na basi la ruwenzo ambalo lilikuwa linatoka njombe kuelekea dar sasa dereva wetu akaona amkwepe huyu mwenye basi la ruwenzo anafanya hivyo na ruwenzoakawa ameshaingia kwahiyo  amelipiga kwa nyuma Gari letu na hapo hapo Gari letu kwa sababu lilikuwa na mwendo kasi lilivyopigwa likabilingika Mara moja juu chini alafu likakaa sawa na kuziba njia marehemu nilioshuhudia kwa macho yangu ni 7 majeruhi usiseme wengine wamekatika miguu wangine mikono wangine kichwa vinavuja damu kama maji sasa nilivyokuwa nahojiwa na Mkuu wa polic wa wilaya akapigiwa simu tena kusema waliobebwa Hosp.wamefaliki 3 so ukijumlisha utapata 10 ili kuna uwezekano wa waliofariki wakaongezeka maana  hali zao ni mbaya sana

Zitto kuwaaga wabunge leo na kuhamia ACT

Pamoja na mpango wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kuliaga Bunge kukwama jana, Chama cha ACT- Tanzania kimetangaza kukamilisha maandalizi ya kumpokea mwanasiasa huyo kuanzia leo.
Mbunge huyo alipanga kuliaga bunge na alisema amekwishapata ruksa ya Spika kuwa angesimama bungeni kuwaaga wabunge na wanachama wa Chadema baada ya chama hicho kumtimua uanachama wake hivi karibuni, lakini ghafla mpango huo uliyeyuka kwa kile kilichoelezwa kuwa Spika amemkatalia.
Tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka mmoja uliopita, Zitto amekuwa akihusishwa kukianzisha, hivyo kitendo chake cha kujiunga nacho kitahitimisha mjadala wa muda mrefu wa mashabiki wake waliokuwa wakihoji wapi ataelekea baada ya kung’olewa Chadema.
Akizungumza na gazeti hili jana, Katibu Mkuu wa ACT, Samsom Mgamba aliangua kicheko na bila kuuma maneno alisema: “Hahahaa... tutampokea kuanzia kesho (leo) na maandalizi yamekamilika.”
Alipotakiwa kueleza wapi mapokezi hayo yatafanyika alisema: “Hilo mbona liko wazi, yatafanyikia makoa makuu yetu (yapo Makumbusho, Dar es Salaam) lakini kwa taarifa zaidi tutawajuza.”
Zitto anaingia ACT ikiwa ni siku tisa kabla ya chama hicho kufanya uchaguzi wake mkuu, huku akitajwa kuwa ameandaliwa kushika wadhifa wa mwenyekiti kuendeleza harakati zake za siasa.
Hivi karibuni, chama hicho kilimvua uongozi aliyekuwa mwenyekiti mwanzilishi, Lucas Limbu kutokana na mgogoro uliokuwapo baina ya viongozi na kufanya nafasi hiyo kubaki wazi.
Tayari washirika wa Zitto waliohusishwa naye kuandika waraka wa mapinduzi ndani ya Chadema na baadaye kufukuzwa uanachama, Mwigamba na Profesa Kitila Mkumbo wametua ndani ya chama hicho kipya.
Chama hicho ambacho kinaendelea na uchaguzi katika ngazi ya mikoa kikibakiza Mkoa wa Geita unaofanya uchaguzi wake kesho. Kitaanza vikao vyake vya kitaifa Machi 27 na kuhitimisha kwa mkutano mkuu Machi 29.
Akizungumzia uchaguzi huo, Mwigamba alisema: “Maandalizi yanakwenda vizuri na hakuna shaka utafanikiwa kwa kiasi kikubwa na tunawaomba Watanzania watuunge mkono.”
Tangu juzi, Zitto alitarajiwa kuliaga Bunge lakini hakufanya hivyo kwa kilichoelezwa kuwa aliitwa na Spika wa Bunge, Anne Makinda na kupewa ushauri kuwa afanye hivyo jana jioni.
Jana asubuhi mbunge huyo hakuingika katika kikao cha Bunge lakini alionekana katika viwanja vya Bunge akiwa amevaa shati la drafti na suruali ya kaki akizungumza na rafiki yake wa karibu, Deo Filikunjombe ambaye ni mbunge wa Ludewa kupitia CCM.

Katika kipindi cha jioni, mbunge huyo aliingia katika viwanja vya Bunge saa 11:10 jioni akiwa amebeba mafaili huku akizungumza na simu na baadaye kutaniana na waandishi wa habari waliokuwa nje ya ukumbi wa Bunge.
Mbunge huyo aliyekuwa amevalia shati nyeupe na suruali nyeupe kabla ya kuingia ndani ya ukumbi wa Bunge alizungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya.
Akwama kuliaga Bunge
Habari zilizopatikana bungeni jana jioni zilieleza kuwa Spika Bunge, Makinda alimpiga ‘stop’ mbunge huyo kuaga bungeni bila kuweka wazi sababu za kufanya hivyo.
Mbunge huyo juzi alitinga bungeni kwa mara ya kwanza tangu Chadema kitangaze kumvua uanachama na kufanya kikao cha siri na Makinda kwa zaidi ya saa moja na baadaye kulieleza gazeti hili kuwa angezungumzia hatima ya ubunge wake jana.
Habari zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na watu wake wa karibu naye zilieleza kuwa licha ya Makinda kumshauri mbunge huyo kuaga bungeni, jana aligoma kumpa ruhusa hiyo.
“Kazuiwa kuaga sijui kwa nini, ila kwa jinsi tunavyoona Makinda ni kama anahitaji Zitto aendelee kubaki bungeni. Ngoja tusubiri kwanza tuone nini kitatokea,” zilieleza habari hizo.
Alipoulizwa juu ya taarifa hizo Zitto, alisema: “Hata mimi nasikia hivyo ila sina hakika sana. Ngoja niende ndani nitajua zaidi, mimi nataka kuaga, can’t stay any more (siwezi kuendelea kubaki).
Alipoingia katika ukumbi wa Bunge, Zitto alionekana akizungumza na baadhi ya wabunge wa upinzani na baadaye wakati mjadala wa muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Uhamiaji ukiendelea, alitoka nje na watu wa karibu wa mbunge huyo walisema alikuwa akishinikiza kuaga kama alivyopanga.
Spika Makinda hakupatikana kuzungumzia sababu za kukataa kumruhusu mbunge huyo na Mkurugenzi wa Shughuli za Bunge, John Joel alipoulizwa juu ya suala hilo alisema hajui chochote.
Mbunge wa Tabora Mjini (CCM), Ismail Aden Rage alisema mbunge huyo kisheria hana mamlaka ya kushinikiza kuaga bungeni na kumtaka asubiri mamlaka husika zifanye kazi hiyo, akimaanisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kulijulisha Bunge kuwa Zitto si mbunge tena baada ya kupata barua ya Chadema.
Chadema ilitangaza kumvua Zitto uanachama siku 10 zilizopita, saa chache baada ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kutupa shauri lake alilofungua akitaka chombo hicho cha sheria kimlazimishe katibu mkuu wa chama hicho kumpa nyaraka za vikao vya Kamati Kuu vilivyomvua nyadhifa zote.Awali, Mahakama hiyo ilitoa amri ya muda ya kuzuia Chadema kumjadili na amedumu kwenye nafasi ya ubunge chini ya zuio hilo kwa takribani mwaka mmoja.

Monday 16 March 2015

Silaha bandia za Watoto kupigwa marufuku Tanzania

IFIKAPO Julai Mosi mwaka huu endapo mwanao atabainika kuwa na silaha bandia (mwanasesere) atakuwa amefanya kosa la jinai, kwa vile Muswada wa Sheria ya Usimamizi na Udhibiti wa Silaha na Risasi umepiga marufuku uingizwaji na matumizi yake nchini.
Muswada huo uliopitishwa na Bunge jana utaanza kutumika Julai mwaka huu, pamoja na mambo mengine, unalenga kuziba mianya ya kuingiza silaha bandia nchini.
Mbali na hilo, Muswada huo unasema mtu akibainika kuwa ni mlevi hatakuwa na sifa ya kumiliki silaha.
Pia muswada huo unataja moja ya sifa za kumiliki silaha kuwa ni mtu na umri wa miaka 25 na kuendelea. Sheria ya sasa ilikuwa haijaainisha ni umri gani ambao mtu anatakiwa kumiliki silaha.
Akisoma kwa mara ya pili muswada huo jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Silima, alisema moja ya sababu ya kutungwa kwa sheria hiyo ni kutoainishwa vema silaha zinazoweza kumilikiwa na raia.
Alisema sababu nyingine ni kutobainishwa kwa utaratibu wa kuweka alama kwenye silaha kisheria.
Silima alisema pia kuwa tangu mwaka 2003 hadi 2013 serikali imeteketeza silaha mbalimbali 28,380.
Akisoma maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama, Kapteni John Chiligati, alisema kutokana na ongezeko la uhalifu wa kutumia silaha, adhabu iliyopendekezwa na serikali irekebishwe.
“Kifungu cha 20 (2) kinatoa adhabu ya kulipa faini ya Sh milioni 10 au kutumikia kifungo cha miaka mitano au vyote kwa pamoja kwa mtu anayetiwa hatiani kwa kosa la kumiliki silaha kinyume cha sheria,”alisema.
Naye msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Godbless Lema, alisema mbali ya kutungwa sheria kali, serikali inapaswa kuzingatia misingi ya utawala bora, haki, usawa, ukweli na ustawi wa jamii kulinda amani na utulivu nchini.

Chelsea yabanwa Koo na Southampton

Chelsea
Chelsea imeendeleza uongozi wake katika ligi kuu ya Uingereza baada ya kupata sare ya 1-1 dhidi ya Southampton katika mechi ya msisimuko mkubwa iliochezwa katika uwanja wa darajani.
Diego Costa aliipatia Chelsea uongozi kupitia kichwa kizuri kabla ya Dusan Tasic kusawazisha kupitia mkwaju wa penalti baada ya Nemanja Matic kumchezea visivyo Sadio Mane katika lango la Chelsea.
Kocha wa Chelsea Mourinho
Kipa wa Southampton Frazer Forster alifanya kazi ya ziada kuokoa mashambulizi ya Oscar,Eden Hazard na Loic Remy.
The blues sasa inaogoza ligi ikiwa na pointi sita zaidi ya mabingwa watetezi wa ligi ya EPL Mancity waliocharazwa bao moja kwa nunge dhidi ya Burnley.

Saudi Arabia yapinga mkataba wa nyuklia Iran

Mitambo ya kinyuklia ya Iran
Kiongozi mkuu wa familia ya kifalme nchini Saudia ameonya kwamba makubaliano ya mpango wa nyuklia wa Iran huenda yakasababisha nchi zingine katika eneo hilo la ghuba kuanza kurutubisha madini ya atomiki.
Mwanamfalme Turki al-Faisal ameiambia BBC kwamba Saudi Arabia pia itatafuta haki sawa kama yatakavyofanya mataifa mengine.
Mataifa sita yenye nguvu duniani yanayojadiliana na Iran yanadai kwamba inatosha kudhibiti shughuli za nyuklia za Iran ili isiweze kuunda silaha za nyuklia.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani akizungumza na Waziri wa Iran Mohhamad Zarif
Lakini wakosoaji wanasema mpango mzima wa Iran ni lazima usitishwe kuepuka hatari ya ushindani wa umiliki silaha za kinyuklia unaotokana na ushindani mkali kati ya Iran na Saudi Arabia.
''Kwa hakika nimekuwa nikiwaeleza mataifa haya ya magharibi kuwa iwe itakavyokuwa Iran itadai haki sawa na yale makubaliano ya Iran na mataifa 6 yenye nguvu za kitonoradi'' alisema Faisal ambaye amekuwa akihudumu kama
mkuu wa kitengo cha ujasusi.
"Ikiwa Iran Itaruhusiwa kurutubisha madini ya kinyuklia kwa kiwango chochote kile, bila shaka Saudi Arabia itadai haki sawa.
Viongozi wanaojadili mkataba wa kinyuklia wa Iran
Saudi Arabia tayari imetia sahihi mkataba wa ushirikiano na Korea Kusini ambayo inapaswa kutathmini uwezekano wa kujenga vinu viwili vya kinyuklia nchini humo.
Aidha Riyadh inamakubaliano na China, Ufaransa na Argentina, kujenga vinu 16 vya kinyuklia katika kipindi cha miaka 20 ijayo.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Marekani , John Kerry,alizuru Riyadh mapema mwezi huu kujaribu kuzima tetesi kuwa Iran itaruhusiwa kumiliki silaha za kinyuklia.



 Iran inasema mitambo yake ya Nyuklia ni ya kuzalisha umeme
Inaaminika kuwa Ufalme wa Riyadh ulimfahamisha kuhusu ushirikiano baina ya serikali ya Iran na wanamgambo wa kishia ambao wamezua vurugu katika mataifa ya Ghuba na mashariki ya kati.
''Bwana Kerry alifahamishwa mchango wa Iran katika vita vinayoendelea Yemen, Syria, Iraq, Palestina, na Bahrain," alisema mwanamfalme Turki.
Kwa sasa Saudi Arabia inashuku mchango na niya mahsusi ya Iran kuchangia kuwafurusha wapiganaji wa kundi la Iraqi Islamic State (IS).

Kipengele kilichotumika kunifukuza Chadema kilitungwa kwa ajili yangu

Zitto-KabweMBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, amevunja ukimya baada ya kuzungumzia tuhuma mbalimbali ambazo zimekuwa zikielezwa juu yake, ikiwamo usaliti ndani ya chama chake na hatima yake ya siasa baada ya kutimuliwa.
Katika mahojiano haya, zitto anatoa maelezo yote juu ya tuhuma dhidi yake.
Swali: Mwaka 2009, ulitaka kugombea uenyekiti wa Chadema, uamuzi huo ulikuwa ni wako mwenyewe ama kuna watu nyuma yako walikushawishi kufanya hivyo?
Jibu: Chadema nilivyoingia kwenye uongozi Makao Makuu, kulikuwa na wabunge watano, wanne wa kuchaguliwa na mmoja wa viti maalumu.
Nilivyoingia pale nilipewa nafasi ya kuwa Mkurugenzi wa Uchaguzi na wa Mambo ya Nje kwa ajili ya kujenga mahusiano ya chama chetu na vyama vingine vya kimataifa, hiyo kazi niliifanya kwa ubora na mpaka sasa uhusiano wote ya Chadema na vyama vya nje, niliyajenga mimi.
Mwaka 2005 niliandika mkakati wa uchaguzi tukapata majimbo mengi zaidi, tulipata asilimia nane ya kura hivyo tukapata wabunge sita wa viti maalumu.
Kabla ya hapo Chadema ilikuwa ikizidiwa hata ya UDP, pamoja na kwamba kilikuwa na wabunge tangu 1995.
Wabunge wake hawakujitanabaisha kama wapambanaji wa misingi ya kitaifa, tulivyoingia (Bungeni) sisi na kina Ndesamburo (Mbunge wa Moshi mjini, Philemon Ndesamburo), DK Slaa (Katibu Mkuu wa Chadema Dk. Willibrod Slaa), tukaanza kubadilisha hali hiyo.
Tukaanza kupambana na ufisadi, kabla ya hapo Dk. Slaa alikuwa bungeni kwa miaka 10 lakini hakuwa machachari kama ilivyokuwa kuanzia 2005.
Alivyoingia mwaka 2005 ndipo tukaanza na hoja kama zile za EPA na Buzwagi.
Baada ya hapo mimi na kina Profesa Kitila Mkumbo tukaona kuna haja ya kubadilisha chama, mwaka 2009 nilivyotaka kugombea uenyekiti nilikuwa na nia ya dhati kabisa.
Ndani ya Chadema kuna watu wanaamini katika uliberari, kama biashara na taji, hawa ni watu kama kina Mbowe (Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe), sisi tunaamini katika demokrasia ya jamii. Hapa kwenye kundi hili unatukuta mimi kina Profesa Mkumbo, Profesa Mwesiga Baregu, na wenginr, tulitaka kukitoa chama kwenyel mrego wa kihafidhina kwenda kwenye ujamaa.
Hata hivyo wazee walinitaka niache kugombea nikaacha, ni kweli ukiangalia chanzo cha ugonzi ni mwaka 2009, ila mimi sikudahani kama kitu kile kingeleta chuki, nilidhani mambo yangeishia pale.
Swali: Nini kilifanya iwe vigumu kumaliza tofauti zako na Chadema?
Jibu: Mara zote nimekuwa nikiwaambia Chadema kwanza waniambie kosa langu ni nini, Ndesamburo aliwahi kunifuata ili tuyamalize, Wenje naye alinifuata na siku kutaka tuyamalize, lakini upande mwingine viongozi nao wanasema yao kwa hiyo ni undumilakuwili tu kila mahali.
Swali: Kuna baadhi ya watu wanaamini kuwa wewe na Mbowe mna ugomvi binafsi, tofauti na vile ambavyo watu wanadhani kuwa mnagombea uongozi. Wengine wanasema uliwahi kutoa siri zake, juu ya kuwa na nyumba Dubai, madai haya yana ukweli?
Jibu: Kama Mbowe ana mali nje mimi kwa kweli sijui, mimi nilitoa hoja ikaundwa kamati ya uchunguzi, kama ilimkuta ana mali nje sijui.
Hata hivyo kama ana nyumba, ama mali nyingine ni kwa nini auogope? Kama una nyumba Marekani, Afrika Kusini, Dubai ama wapi hiyo siyo tabu, ilimradi kwenye tamko la maadili (Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma) uwe umesema kuwa unazo na TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) wajue umepata wapi hizo fedha.
Swali: Lakini inadaiwa kuwa ulikaa na Mbowe wewe akakueleza kama mtu wake wa karibu kuwa ana nyumba Dubai na wewe ukatoa hizo habari kwa umma na ndicho kilichomuudhi.
Jibu: Mimi sijawahi kukaa na Mbowe kuzungumza hayo mambo. Sina ugomvi binafsi Mwenyekiti wa Chadema, siku zote nimekuwa nikimchukulia kama kaka, ndiyo maana hata akinishambulia nimekuwa nikijitahidi kukaa kimya.
Mwanzoni kabisa yeye alikuja chuo kikuu kunifuata, mwanzoni mwa mwaka 2001, nikiwa mwanachama wa Chadema lakini siyo kiongozi, yeye akiwa Mbunge wa Hai, alikuja akaniambia naomba tuzungumze utusaidie kwenye chama.
Alikuwa anataka kufanya mabadiliko ya katiba ya chama, nikatumia nafasi yangu ya uanaharakati wa wanafunzi na uwezo wangu wa uchambuzi tukafanya hivyo tulivyofanya.
Tukabadilisha chama mimi na yeye, mabadiliko makubwa ambayo yanaonekana hivi sasa Chadema ni kazi ambayo tulifanya mimi na yeye, hata gumboe mwaka 2009 niliona ni jambo la kawaida. Kilichopo ni mitizamo tofauti ya namna ya kuendesha siasa, na tofauti hizo zimesababisha yatokee yaliyotokea.
Wakati mwingine nikikaa peke yangu huwa yangu na kujiuliza, huwa sioni msingi wa ugomvi wangu na chadeama, naona ni ugomvi tu wa madaraka na juhudi za watu kutaka kuondoa wengine katika ulingo.
Katika mazingira kama hayo ni rahisi kutoa tafsiri kwamba kuna ugomvi binafsi.
Yeye (Mbowe) alikuja hapa Kigoma akafanya mkutano wa hadhara akanitukana, akasema alinisaidia sijui gari, sijui nini, yaani alikuja nyumbani kwetu kunisimanga.
Nikasema huyu mtu ananisimanga, kwanza ni mambo ya kishamba, kwamba unamsaidia mtu halafu unakuja kumsema, kwanza kuna vitu ambavyo mimi mwenyewe nimemsaidia labda kifedha ama siyo fedha, na tunajua kati ya mimi na yeye.
Siyo vitu naweza kuibuka nikasema nilimdharau sana kwa kweli, na juzi nimemsikia huko Shinyanga akisema kuwa hawezi kukaa na kuongea na mimi kwamba ni msaliti na mambo kama hayo. Huu ni undumilakuwili kwa kweli kwa sababu huku anatuma watu kwamba kina Ndesamburo (Philemon Ndesamburo), kwamba tuongee tuone namna ya kuyamaliza haya mambo alafu yeye huku nyuma akikaa anaongea yake.
Kwa hiyo binafsi naamini sina ugomvi naye sanasana ni tofauti za kiitikadi. Mimi na yeye tumekaa Bungeni miaka 10, naomba tu watu watupime.
Katika miaka yangu 10 ni hoja gani nimezisimamia na yeye ni zipi amezisimamia.
Mimi siku zote siasa zangu ni hoja na issue za kusaidia wananchi na nafurahi ninavyosimamia vitu na kuona vikienda.
Swali: Mara kadhaa viongozi wa chama chako wamekuwa wakikutuhumu kwa kusaliti chama, na kwamba kwa upande mmoja unatumiwa na CCM na upande mwingime usalama wa taifa, ni kwa nini ushutumiwe kwa tuhuma kama hizo?
Jibu: Kwenye siasa ukitaka mwanasiasa amalizike ni kumpa hizo tuhuma. Lakini waulize (Chadema), ni taarifa zipi zinapelekwa kwenye usalama wa taifa, watu haohao walisema siendi kwenye vikao vya chama, wala ofisini, sasa hizo taarifa ninazozipeleka ni zipi wakati kwenye vikao wala ofisini siendi? Mtu anayepeleka taarifa ni yule asiyekosa kwenye vikao. Anahudhuria kila kikao ili apate taarifa za kupeleka.
Lakini pia angalia, mwaka 2010 nilitoa taarifa ya kumuomboa Waziri Mkuu, hoja ile ikaungwa mkono kwa kusainiwa na wabunge wa pande zote, hivyo ikasaidia kuondoa baadhi ya mawaziri waliokuwa na shutuma.
Mwaka 2013 kulikuwa na Operesheni Tokomeza. Ripoti ya Kamati ya Bunge iliyokuwa imewasilishwa ilikuwa inamtaja waziri mmoja tu, lakini nilisimama na kujenga hoja mawaziri wengi tu wakaondolewa.
Mwaka 2014 nimepeleka hoja ya Escrow na nikaisimamia, mawaziri wameondoka, serikali imetikisika, sasa mtu anayetumika na Chama Cha Mapinduzi kwa nini aiangushe serikali ya chama hicho mara tatu ndani miaka mitano? Mtu ambaye anatumika inawezekanaje alete mjadala utakaoingusha serikali?
Ndiyo maana sipotezi muda kujibizana na propaganda za aina hiyo, watuambie ni taarifa gani zilipelekwa huko zikawaathiri?
Swali: Baada ya Mahakama kutoa uamuzi wake na Mwansheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lisu kutangaza kuwa umefukuzwa uanachama kwa kuwa kukishitaki chama ni kujifukuza katika chama moja kwa moja, tangu ukiwa kiongozi wa chama uliwahi kukitilia shaka kifungu hicho kwa kuwa hivi sasa umeonekana kukilalamikia.
Jibu: Hiki kifungu kipo kwenye kanuni na wala siyo Katiba, kilitungwa mwaka 2013. Mwaka huo kuna mabadiliko fulani fulani yalifanywa. Mabadiliko yale yalikuwa na malengo fulanifulani ikiwamo kulenga watu fulanifulani.
Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri, mamlaka ya kutoa haki iko kwenye chombo kimoja tu nacho ni Mahakama, kila raia ana haki ya kwenda mahakamani kudai haki, unaposema mwananchama wa Chadema akienda mahakamni amejivua uanachama ina maana wewe huitambui Katiba ya Jamuhuri.
Hii ina maana kama mwanachama amekipangisha chama, na chama kikashindwa kulipa kodi, yule mwanachama akienda mahakamani amejivua mwenyewe uanachama kwa kuwa haruhusiwi kwenda mahakamani.
Hicho ni kipengele ambacho hakikupaswa kuwap, Wanachama wa Chadema waende mahakamani kushtaki kipengele hicho ili kitangazwe kuwa siyo halali.
Chama kinachopambana kushika dola hakipaswi kuwa na vipengele kama hivi. Ila yote kwa yote hiki kipengele kimewekwa mwaka 2013 na mwaka 2015 kikatumika kwangu, ni wazi kilitungwa kwa ajili yangu.
Swali: Baada ya kufukuzwa Chadema, ni nini hatma yako kisiasa?
Jibu: Nina ziara ya kuzunguka na wananchi wa jimbo langu kuangalia jinsi ya kuwatumikia, leo (jana) nawaaga rasmi kwamba sintakuwa nao baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu, lakini ni nini kinachokuja baadaye ya hapo tutakijua vizuri wiki ijayo (wiki hii).
Hatujajua kama Chadema wameandika barua kwa Spika ili kunitangaza kuwa jimbo liko wazi, kama ndivyo tutakaa kujua ni nini cha kufanya.
Ilipaswa baada ya kesi kwisha taratibu zifuatwe, mpaka sasa sijapata taarifa zozote za kufukuzwa ndiyo maana nasema mpaka wiki kesho iishe tutajua, nitakuwa na nia ya kuendelea kutumikia kwenye jimbo lolote Oktoba.
Swali: Una mpango wa kujiunga na ACT?
Jibu: Tusijaribu kuvuka mto kabla hatujafika pa kuvukia.
Swali: Vipi hukumu ya Mahakama Kuu juu ya kesi yako na Chadema?
Jibu: Kwenye kazi yangu kuna miguu ya watu wengi naikanyaga, taarifa yangu ya Escrow nimewakanyaga mpaka mahakama. Kwa hiyo yawezekana kabisa mahakama iliona hapa ndipo kwa kunikanyaga, ama yawezekana kabisa ni taratibu.
Inaonekana kuna uhusiano wa karibu wa mahakama na wanasheria wa Chadema, sisi tulisikia kwenye vyombo vya habari kwamba hukumu ya kesi yetu imetolewa.
Hata baada ya hukumu hiyo, tulijaribu kufuatilia ili kupata hukumu, kwa siku mbili tulizungushwa, siku ya tatu tukaambiwa kuwa jalada lipo kwa jaji kiongozi.
Lakini mimi bado nina imani kwamba wakuu wa mahakama watachunguza jambo hili na kuona kama kuna cha kufanya.
Sisi tulipaswa kuitwa mahakamani, lakini hatukuitwa, kuna taratibu za mahakama hazikufuatwa, tuna imani kuwa viongozi wa mahakama watachunguza kama kuna suala la rushwa katikati hapa ama kuna nini.
Lakini pia hali hii imenifanya niwe na kiu zaidi ya kuhakikisha nikipata tena nafasi nitafanya operesheni kwenye mfumo wa mahakama kwa kuwa umekuwa na malalamiko sana ya kuwaumiza wananchi.

Makundi yapigana vikumbo kwa Lowassa huko CCM

(FILES) An undated file photo shows TanzMAKUNDI ya watu wa kada mbalimbali yamezidi kutua nyumbani kwa Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa (CCM), yakimtaka achukue fomu ya kuwania urais kupitia CCM muda utakapofika.
Lowassa ambaye pia ni Waziri Mkuu wa zamani, kwa wiki kadhaa sasa amekuwa akipokea wageni wa makundi mbalimbali nyumbani kwake wakimtaka awanie nafasi hiyo ya uongozi wa juu wa nchi.
Kutokana na joto hilo la urais ndani CCM, jana makundi mawili ya wana CCM yalibisha hodi nyumbani kwa kada huyo na kumshawishi kufanya hivyo pamoja na kumkabidhi fedha za kuchukulia fomu.
Kundi la kwanza lilikuwa ni wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Arumeru ambao waliwasilisha ombi lao kwa mbunge huyo pamoja na kumkabidhi Sh milioni moja za fomu.
Akizungumza katika kikao hicho, Mwenyekiti Mstaafu wa Halmashauri ya Meru, John ole Saitabau, alisema wamefikia hatua hiyo baada ya kuona Lowassa ana sifa zote za kuwania nafasi hiyo ya uongozi wa nchi.
“Sisi tumekuja hapa kukushawishi uchukue fomu ya kuwania urais kupitia chama chetu cha CCM… uwezo huo unao na Tanzania inakuhitaji,” alisema ole Saitabau.
Naye Mathias Manga, ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (MNEC), alisema zaidi ya asilimia 75 ya wajumbe wa NEC wanamshawishi Lowassa awanie urais kwa sasa kutokana na sifa yake ya uchapakazi mbele ya jamii.
Kundi la pili ambalo lilifika nyumbani kwa Lowassa ni la marafiki wa Lowassa, Kanda ya Kaskazini, ambako zaidi ya watu 500 kutoka kada mbalimbali wakiwamo walemavu wa macho na watu wenye albino, walimkabidhi Lowassa Sh milioni 2.5.
Akisoma risala kwa niaba ya vijana waliotoka katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara, Protas Soka, alisema kwa sasa Watanzania wanamuhitaji Lowassa aweze kuliongoza Taifa.
“Kwa lugha nyingine Lowassa sasa tunakuomba utangaze nia ya kuingia kwenye kinyang’anyiro cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mwaka huu wa 2015 wewe ni tumaini la walio wengi hapa kwetu Tanzania,” alisema.
Vilevile, Jumamosi iliyopita Uongozi wa Shirika la Umoja wa Machinga Tanzania (SHIUMA), ulimtembelea Lowassa na kumkabidhi Sh milioni moja za kuchukulia fomo ya urais ndani ya CCM muda utakapofika.
Mwenyekiti wa shirika hilo, Matondo Masanja, akisoma risala yao kwa Lowassa, alisema wamefikia hatua hiyo baada ya kumuona Lowassa ndiye mtu sahihi kumrithi Rais Jakaya. Kikwete.
Lowassa na maombi kwa Mungu
Akizungumza baada ya kupokea maombi hayo, Lowassa aliwashukuru kwa imani kubwa waliyoionyesha kwake na kuwaambia wamuombe Mungu jambo hilo liende salama.
“Naendelea kumuomba Mungu ajalie atimize ndoto ya safari ya matumaini,” alisema Lowassa.
Alisema anajivunia mafanikio aliyoyapata wakati akiwa mdhamini wa Umoja wa Vijana wa CCM ambako alisimamia Umoja huo kupata kitega uchumi kikubwa. Jengo hilo liko makao makuu ya Umoja huo Dar es Salaam.
Viongozi wa Serikali, Chama na wafugaji wa kutoka Wilaya ya Mkinga walifungua njia ya kumchangia fedha za kuchukulia fomu Lowassa kwa kumpatia Sh 200,000.

Yanga yapeleka Kilio Zimbabwe, Yaichapa Fc Platinum 5-1

Timu pekee iliyobakia kwenye mashindano ya shirikisho la mpira wa miguu barani Afrika kutoka Tanzania, Yanga, imeendelea kuweka matumaini hai ya kusonga mbele baada ya kuiangushia kipigo kikali timu ya Platnum ya Zimbabwe kwa mabao 5-1.
Mchezo huo wa raundi ya kwanza ya vilabu vinavyoshiriki Kombe la Shirikisho la CAF, ulifanyika Jumapili jijini Dar es Salaam.
Kipindi cha kwanza kilimalizika kwa kufungana mabao 2-1.
Kipindi cha Pili ndicho kilichokuwa kiama chya Platnum baada ya kuruhusu mabao matatu zaidi.
Wafungaji wa timu ya Yanga ni Mrisho Ngasa aliyefunga magoli mawili, Haruna Niyonzima, Salum Telela, na Amisi Tambwe walifunga bao moja kila mmoja. Kwa matokeo hayo Yanga imejenga mazingira ya kusonga mbele.
Michezo mingine ya Shirikisho ilikuwa katika ya Orlando Pirates ya Afrika kusini dhidi ya URA ya Uganda, hadi mwisho wa mchezo Orlando mabao ilitoka na ushindi wa 2-1. Nayo Vita klabu ya DR Congo iliiadhibu Ferrroviario Beira ya Msumbiji mabao 3-0

Hostel za Mabibo chuo cha UDSM zaungua moto

Ajali ya Moto imetokea leo majira ya saa 5:30 asubuhi katika chuo Kikuu cha Dar-es Salama kwenye hostel zao ziitwazo Mabibo Hostel.
 
Chanzo cha ajali hiyo ya Moto bado hakijaweza kufahamika kwa mapema wala dhamani ya vitu vilivyo teketea kwa moto havijaweza kufahamika kwa mapema, Moto huo ulianza kuwaka katika hostel hizo Block "B"
Vikosi vya zimamoto vimeshawasili kwa zoezi la kuzima moto

Wednesday 11 March 2015

Biashara ya Kuuza watoto yashamiri China


Uchunguzi wa BBC umegundua kuwa watoto wanawekwa katika matangazo ya kuuzwa kupitia kwa mitandao nchini China licha ya kuwepo kwa jitihada za polisi za kupambana na ulanguzi wa watoto.
Mojawapo ya matangazo hayo ni lile la mtoto wa umri wa miezi minane aliyekuwa akiuzwa kwa dola 30,000.
Mchunguzi wa  wa shirika la utangazaji la Uingereza BBC aliyejifanya kuwa mnunuzi alionyesha mtoto kupitia kwa video ya mtandao na mwanamke ambaye alisema kuwa hangeweza kukidhi mahitaji ya kumlea mwana huyo.
Licha ya hatua ya kutangazwa kwa watoto mitandaoni kuwa halali nchini China, matangazo ya watoto ili kuwauza ni haramu .

Watoto waliookolewa wasahau majina yao

Jeshi la Cameroon likiwasaka wapiganaji wa Boko Haram,

Takriban watoto 80 waliookolewa katika kambi ya kundi la Boko Haram nchini Cameroon hawawezi kukumbuka majina yao kulingana na afisa mmoja aliyewatembelea.
Watoto hao wenye umri wa miaka 5 hadi 18 hawakuzungumza kiingereza,kifaransa ama lugha nyengine yeyote ile kulingana na Christopher Fomunyoh,ambaye ni mkurugenzi wa kitaifa wa taasisi ya National Democratic Institute {NDI}.
Watoto hao walipatikana katika kambi kazkazini mwa Cameroon mnamo mwezi Novemba.
Kundi la Boko Haram kutoka Nigeria limepanua mashambulizi yake hadi nchini Cameroon.
Wapiganaji hao wanajaribu kusimamisha taifa lenye uongozi wa kiislamu kazkazini mashariki mwa Nigeria.
Wanadhibiti miji kadhaa na vijiji katika jimbo hilo na hivi majuzi waliahidi kuiga mfano wa kundi la Islamic State ambalo limeteka eneo kubwa la Syria na Iraq.

Ndege inayotumia umeme jua imetua India

http://ichef.bbci.co.uk/news/ws/660/amz/worldservice/live/assets/images/2015/03/09/150309053101_solar_impulse_2_test_flight_640x360_epa.jpg
Ndege ya kwanza inayotumia umeme jua imejaribiwa leo

Jaribio la ndege inayotumia umeme jua kuzunguka dunia pasi na kutumia hata tone moja ya petroli imeingia mkondo wa pili jana baada ya ndege hiyo kufaulu kutua nchini India
Ndege hiyo imetua katika uwanja wa ndege wa Ahmedabad na kuweka rekodi ya kuwa ndege ya kwanza isiyotumia petroli kupaa juu ya bahari ya Arabian zaidi ya kilomita 1468 kuanzia Muscat Oman hadi
Ahmedabad India.
Safari hiyo ilichukua zaidi ya saa 15.
Marubani hao wawili sasa wanapumzika kabla ya kuendelea mbele na mikondo mingine 10 zilizosalia katika jitihada za kuzunguka duniani bila ya kutumia petroli.
Kiongozi wa ujumbe huo Rubani Bertrand Piccard amesema wamefurahishwa mno na jinsi mpango wao unavyoendelea.
Rubani Bertrand na mswisi mwenza Andre Borschberg wanapanga kutumia miezi 5 ijayo kukamilisha safari hiyo.
Ndege hiyo inauwezo wa kupaa hata usiku kutokana na betri zenye uwezo wa kuhifadhi umee kutoka kwa jua
Ndege hiyo iliruka majira ya saa 12 saa za Afrika Mashiriki ikianzia Abu Dhabi.
Ndege hiyo yenye kiti kimoja ina mabawa yenye ukubwa sawa na ya ndege kubwa za jumbo zinazotumika kwa uchukuzi wa abiria inamabawa yenye upama wa mita 72.
Hata hivyo inauzani wa tani 2.3 tu uzito sawa na wa gari.
Mabawa yake yamefunikwa na vifaa vya vya kunasia mionzi ya jua yaani solar panels.
Betri zake zina uwezo wa kuhifadhi nguvu ya umeme jua na hivyo kuiweza kusafiri hata nyakati za usiku.
Marubani wawili wanaorusha ndege hiyo Bertrand Piccard na Andre Borschberg watapita katika hatua kumi na mbili za safari yao.

Polisi wakamatwa na pembe zaFaru Nchini Kenya

Pembe za faru

Afisa mmoja wa polisi amekamakwa na pembe ya faru ilio na thamani ya dola 40,000.
Tayari amefikishwa mahakamani.
Afisa huyo na wenzake watatu walipatikana wakiwa katika harakati ya kuuza pembe hizo kwa wapelelezi wa shirika la wanyama pori nchini Kenya KWS.
Mshukiwa huyo ni afisa wa cheo cha chini katika kikosi cha polisi cha Kenya .
Aliingizwa mtengoni na maafisa wa shirika la wanayama pori waliojifanya kuwa wanunuzi wa pembe hiyo ya faru.
Wakati maajenti hao walipojaribu kumkamata afisa huyo alionya kuwapiga risasi lakini akashindwa nguvu.
Alipelekwa katika kizuizi usiku wa jumatatu pamoja na washukiwa wengine.
Mshukiwa wa nne alitoroka.
Pembe za faru hudaiwa kuwa na thamani zaidi ya dhahabu barani Asia,ambapo pembe zinazoibwa barani Afrika hupelekwa.

Mlinzi wa Dk. Silaa aendelea kusota rumande

Image result for Mlinzi wa silaaKHALID Kangezi, mlinzi binafsi (PSU) wa Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilibrod Slaa, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi kwa uchunguzi kuhusu tuhuma dhidi yake.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Polisi Kinondoni, Camillus Wambura alisema uchunguzi unaendelea dhidi ya Kagenzi ambaye alifikishwa katika Kituo cha Polisi Osterbay juzi.
“Suala hili nilitakiwa kulitolea taarifa kwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleimani Kova, lakini sikumpelekea kwa sababu uchunguzi haujakamilika.
“Bado tunaendelea kumchunguza mtuhumiwa, zipo taarifa mbalimbali ambazo hazijakamilika zitakapokamilika tutampelekea Kamishna Kova aweze kulizungumzia suala hilo.
“Tunaomba muwe na subira tuone itakuwaje na nitawasisitiza wapelelezi waongeze kasi ya uchunguzi tuweze kupeleka taarifa kwa Kamishna aweze kulitolea ufafanuzi katika jamii,” alisema Wambura.
Kangezi ambaye amekuwa mlinzi wa Dk. Slaa kwa miaka miwili, inadaiwa alikuwa akitumiwa na vyombo vya Usalama wa Taifa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuvujisha siri za chama hicho ikiwamo kupewa kazi ya kumuua Katibu Mkuu huyo wa Chadema.
Hata hivyo, jana wanasheria wa Chadema waliitwa Kituo cha Polisi Osterbay kwa ajili ya kutoa maelezo kuhusu tukio hilo.

Zitto Kabwe avuliwa uanachama wa chadema rasmi

Image result for zitto kabwe
HATIMAYE Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), jana kimetangaza rasmi kumvua uanachama Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Bw. Zitto Kabwe kwa tiketi ya chama hicho.

Chama hicho kimechukua uamuzi huo baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kutupilia mbali pingamizi la Mbunge huyo dhidi ya Kamati Kuu ya CHADEMA, kutojadili uanachama wake.

Bw. Kabwe alikuwa akikabiliwa na mashtaka ya ukiukwaji wa Katiba ya chama chake, kanuni na mwongozo wa chama ambapo kikao cha Kamati Kuu, kilichokaa Novemba 20-22, mwaka 2013, kiliazimia aachishwe nafasi zote za uongozi alizokuwa akishikilia.

Kamati hiyo pia iliazimia Bw, Kabwe achukuliwe hatua zaidi za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kuachishwa, kufukuzwa uanachama kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za Uendeshaji za 6.5.2(d).

Lissu atoa tamko

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwanasheria Mkuu wa chama hicho ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, Bw. Tundu Lissu, alisema kutokana na uamuzi huo wa mahakama, CHADEMA kinakusudia kuiandikia barua Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Lengo la barua hiyo ni kuitaarifu NEC kuwa Bw. Kabwe si mwanachama tena wa chama hicho, hivyo amepoteza sifa ya kuwa mbunge kwa tiketi ya CHADEMA ili aweze
kumjulisha Spika wa Bunge.

Bw. Lissu alisema licha ya mahakama hiyo kutupilia mbali kesi ya Mbunge huyo, imemtaka alipe gharama zote za kesi tangu ilipofunguliwa hadi uamuzi ulipotolewa.

\"Mahakama imeamua kulifuta pingamizi lililowekwa na Bw. Kabwe mwaka 2014 akizuia kikao cha Kamati Kuu kisimjadili kabla ya shauri lake halijasikilizwa na Baraza Kuu.

\"Pingamizi hilo limetupiliwa mbali baada ya Mahakama kupitia hoja zake na kubaini kuwa, hakufuata taratibu za kisheria, hivyo
kutokana na uamuzi huo, chama kinatamka rasmi kumvua uanachama Bw. Kabwe ambaye pia alikuwa Naibu Katibu Mkuu,\" alisema Bw. Lissu.

Aliongeza kuwa, kwa mujibu wa katiba ya chama hicho, mwanachama yeyote anapofungua kesi mahakamani dhidi ya chama chake, kama atashindwa katika kesi hiyo atakuwa amejiondoa uanachama wake.

Maelezo ya Kabwe

Kwa upande wake, Bw. Kabwe alisema hakuwa na wito wa kwenda mahakamani jana na Jaji wa kesi hiyo amehamishiwa Tabora, hivyo yeye na Mawakili wake hawana taarifa ya Jaji Mpya; lakini Mwanasheria wake atafuatilia hukumu hiyo.

\"Mimi nilikuwa kwenye kikao cha Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Nishati na Maji (EWURA), nikaona katika mitandao ya kijamii kuwa kesi yetu imetupwa lakini katika kumbukumbu zetu, ilikuwa twende mahakamani Machi 12 mwaka huu si kwa ajili ya maamuzi bali kwa ajili ya kesi kutajwa.

\"Taarifa hizi zimetushangaza baada ya kusikia uamuzi umetolewa leo na CHADEMA kutangaza kunivua uanachama, hadi sasa sina taarifa rasmi, naendelea na kazi zangu kama kawaida na ratiba yangu inaonesha kesho (leo), nitakuwa TANESCO,\" alisema.

Aliongeza kuwa, kesho atakuwa anashughulikia mabilioni ya Uswisi ambapo kwa upande wake, hana taarifa rasmi na ataweza kusema chochote baada ya kupata taarifa rasmi na Wanasheria wake wameenda mahakamani kupata hati ya maamuzi ili waone hatua za kuchukua.

Kesi ya msingi
Januari 2, 2014, Mahakama hiyo ilitoa zuio la muda kwa Kamati Kuu ya CHADEMA kutojadili uanachama wa Bw. Kabwe katika kikao cha chake cha Januari 3, 2014.

Siku hiyo ya Januari 3, 2014, Mahakama hiyo ilisikiliza hoja za mawakili wa pande zote kuhusu maombi hayo mbele ya Jaji John Utamwa ambapo Januari 7, 2014, Mahakama hiyo ilitoa amri kwamba Bw. Kabwe asijadiliwe uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.

Bw. Kabwe alikuwa anatetewa na wakili, Albert Msando ambapo CHADEMA iliwakilishwa na Bw. Lissu pamoja na Peter Kibatala.

Katika kesi ya msingi, Bw. Kabwe alifungua kesi dhidi ya Baraza la Wadhamini la chama hicho na Katibu Mkuu, Dkt.Willbrod Slaa, akiiomba Mahakama itoe zuio la muda kwa
Kamati Kuu kutojadili suala la uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.

Katika maombi yake, Bw. Kabwe aliiomba mahakama hiyo kuiamuru Kamati kuu na chombo chochote kisijadili uanachama wake hadi rufaa yake itakaposikilizwa na Baraza Kuu la chama.

Pia aliiomba Mahakama imwamuru, Dkt. Slaa kumkabidhi nakala za taarifa na mwenendo mzima wa vikao vilivyomvua uongozi ili akate rufaa katika ngazi ya juu ya chama hicho.

Ajali mbaya yatokea maeneo ya Mafinga Iringa yaua 65

https://scontent-lhr.xx.fbcdn.net/hphotos-xpf1/v/t1.0-9/11035462_1168898133124603_6217082283355116026_n.jpg?oh=e9a3d779bccbb0a2f1bc9b5615966c33&oe=558DF0B4Ajali mbaya yatokea maeneo ya Mafinga Iringa sehemu kunaitwa Changarawe ambapo gari aina lori lilokuwa likitokea Dar kwenda Mbeya ambapo lilikuwa likikwepa shimo kubwa lililopo katikati ya barabara na kugongana na gari la abiria la Kampuni ya Majinja lililokuwa likitoka Mbeya kwenda Dar. Hii ni maelezo ya trafki aliyepo hapa. Kontena la lori limelalia kabisa basi, na watu wengine wamelaliwa na wengine
wameporomokea korongoni, mpaka sasa hakuna majeruhi ni maiti tu, wala hakuna mtu ambaye inadhaniwa amepona. - Kuna watoto wawili hapa, makadirio ya miaka ni mitatu na saba, lakini hawa inasemekana
kwamba walirushwa korongoni kutokana na huo
mgongano. 

Uokoaji wa maiti na majeruhi walionasa kwenye ajali hapa eneo la tukio unazorota kutokana na ukosefu wa Gesi ya kukata basi kukosekana Mafinga. Juhudi zinafanyika ili kuweza kuokoa majeruhi pamoja na maiti.