Monday 16 March 2015

Silaha bandia za Watoto kupigwa marufuku Tanzania

IFIKAPO Julai Mosi mwaka huu endapo mwanao atabainika kuwa na silaha bandia (mwanasesere) atakuwa amefanya kosa la jinai, kwa vile Muswada wa Sheria ya Usimamizi na Udhibiti wa Silaha na Risasi umepiga marufuku uingizwaji na matumizi yake nchini.
Muswada huo uliopitishwa na Bunge jana utaanza kutumika Julai mwaka huu, pamoja na mambo mengine, unalenga kuziba mianya ya kuingiza silaha bandia nchini.
Mbali na hilo, Muswada huo unasema mtu akibainika kuwa ni mlevi hatakuwa na sifa ya kumiliki silaha.
Pia muswada huo unataja moja ya sifa za kumiliki silaha kuwa ni mtu na umri wa miaka 25 na kuendelea. Sheria ya sasa ilikuwa haijaainisha ni umri gani ambao mtu anatakiwa kumiliki silaha.
Akisoma kwa mara ya pili muswada huo jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Silima, alisema moja ya sababu ya kutungwa kwa sheria hiyo ni kutoainishwa vema silaha zinazoweza kumilikiwa na raia.
Alisema sababu nyingine ni kutobainishwa kwa utaratibu wa kuweka alama kwenye silaha kisheria.
Silima alisema pia kuwa tangu mwaka 2003 hadi 2013 serikali imeteketeza silaha mbalimbali 28,380.
Akisoma maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama, Kapteni John Chiligati, alisema kutokana na ongezeko la uhalifu wa kutumia silaha, adhabu iliyopendekezwa na serikali irekebishwe.
“Kifungu cha 20 (2) kinatoa adhabu ya kulipa faini ya Sh milioni 10 au kutumikia kifungo cha miaka mitano au vyote kwa pamoja kwa mtu anayetiwa hatiani kwa kosa la kumiliki silaha kinyume cha sheria,”alisema.
Naye msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Godbless Lema, alisema mbali ya kutungwa sheria kali, serikali inapaswa kuzingatia misingi ya utawala bora, haki, usawa, ukweli na ustawi wa jamii kulinda amani na utulivu nchini.

No comments: