Monday 16 March 2015

Saudi Arabia yapinga mkataba wa nyuklia Iran

Mitambo ya kinyuklia ya Iran
Kiongozi mkuu wa familia ya kifalme nchini Saudia ameonya kwamba makubaliano ya mpango wa nyuklia wa Iran huenda yakasababisha nchi zingine katika eneo hilo la ghuba kuanza kurutubisha madini ya atomiki.
Mwanamfalme Turki al-Faisal ameiambia BBC kwamba Saudi Arabia pia itatafuta haki sawa kama yatakavyofanya mataifa mengine.
Mataifa sita yenye nguvu duniani yanayojadiliana na Iran yanadai kwamba inatosha kudhibiti shughuli za nyuklia za Iran ili isiweze kuunda silaha za nyuklia.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani akizungumza na Waziri wa Iran Mohhamad Zarif
Lakini wakosoaji wanasema mpango mzima wa Iran ni lazima usitishwe kuepuka hatari ya ushindani wa umiliki silaha za kinyuklia unaotokana na ushindani mkali kati ya Iran na Saudi Arabia.
''Kwa hakika nimekuwa nikiwaeleza mataifa haya ya magharibi kuwa iwe itakavyokuwa Iran itadai haki sawa na yale makubaliano ya Iran na mataifa 6 yenye nguvu za kitonoradi'' alisema Faisal ambaye amekuwa akihudumu kama
mkuu wa kitengo cha ujasusi.
"Ikiwa Iran Itaruhusiwa kurutubisha madini ya kinyuklia kwa kiwango chochote kile, bila shaka Saudi Arabia itadai haki sawa.
Viongozi wanaojadili mkataba wa kinyuklia wa Iran
Saudi Arabia tayari imetia sahihi mkataba wa ushirikiano na Korea Kusini ambayo inapaswa kutathmini uwezekano wa kujenga vinu viwili vya kinyuklia nchini humo.
Aidha Riyadh inamakubaliano na China, Ufaransa na Argentina, kujenga vinu 16 vya kinyuklia katika kipindi cha miaka 20 ijayo.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Marekani , John Kerry,alizuru Riyadh mapema mwezi huu kujaribu kuzima tetesi kuwa Iran itaruhusiwa kumiliki silaha za kinyuklia.



 Iran inasema mitambo yake ya Nyuklia ni ya kuzalisha umeme
Inaaminika kuwa Ufalme wa Riyadh ulimfahamisha kuhusu ushirikiano baina ya serikali ya Iran na wanamgambo wa kishia ambao wamezua vurugu katika mataifa ya Ghuba na mashariki ya kati.
''Bwana Kerry alifahamishwa mchango wa Iran katika vita vinayoendelea Yemen, Syria, Iraq, Palestina, na Bahrain," alisema mwanamfalme Turki.
Kwa sasa Saudi Arabia inashuku mchango na niya mahsusi ya Iran kuchangia kuwafurusha wapiganaji wa kundi la Iraqi Islamic State (IS).

No comments: