Saturday 31 May 2014

Raisi mpya wa malawi aapishwa


Peter Muthirika anayeongoza chama cha DPP ndiye rais mteule nchini Malawi
Rais mpya wa Malawi Peter Mutharika ameapishwa rasmi baaada ya kucheleweshwa kwa matokeo ya uchaguzi kufuatia madai ya udanganyifu na wizi wa kura.
Mutharika aliibuka mshindi wa uchaguzi huo baada ya kujipatia zaidi ya asilimia 36 ya kura zilizopigwa
Rais anayeondoka mamlakani Joyce Banda alikuwa katika nafasi ya tatu.
Banda amewataka wafuasi wake kuheshimu matokeo hayo.
Mahakama kuu ilipinga ombi la kura kuhesabiwa upya baada ya Banda kudai kuwa kumekuwa na udanganyifu mkubwa katika shughuli hiyo.
Peter Mutharika aliwahi kuhudumu kama waziri wa maswala ya kigeni na ndugu ya aliyekuwa rais wa taifa hilo marehemu Bingu wa Mutharika aliyefariki mwaka 2012 akiwa afisini.
Mwandishi wa BBC Baruan Muhuza amesema kutoka mjini Blantyre kuwa Profesa Peter Mutharika ameshinda uchaguzi huo kwa kupata asilimia 36.4 ya kura zote akifuatiwa na Dr Lazarus Chakwera mwenye asilimia 27.8 huku Rais anayemaliza muda wake Dr Joyce Banda akishika nafasi ya tatu kwa asilimia 20.2 na Atupele Muluzi amekuwa wa nne na asilimia 13.7
Mwenyekiti wa tume ya uchaguzi Jaji Mackson Mbendera amesema uchaguzi huo ulikumbwa na changamoto nyingi lakini mwishowe nchi ikalazimika kupata kiongozi wake na akawaomba wananchi kuwa na utulivu .

Wanafunzi wa chuo kikuu cha STEMUCO waandamana

Wanafunzi Stemuco waandamanaWANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Stella Maris (STEMUCO) mkoani Mtwara, wameandamana juzi wakidai kutolipwa posho za malazi na chakula na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwa miezi mitatu mfululizo.
Maandamano hayo yalianzia chuoni hapo saa 9 alasiri na kuelekea kwa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali mstaafu Joseph Simbakalia, lakini walipofika maeneo ya Bima yalizuiliwa na polisi na kutakiwa kueleza kilio chao.
Akizungumza kwa jazba, mmoja wa wanafunzi hao, alisema kwa miezi mitatu hawajalipwa fedha ya kujikimu, na hakuna tamko lolote ambalo wameambiwa wakati wana haki kama vyuo vingine.
“Hatujalipwa fedha za malazi na chakula kwa miezi mitatu sasa, ndiyo maana tumechukua hatua hii ya kuandamana, tunakwenda kwa Mkuu wa Mkoa tumuelezee matatizo yetu, kwani yeye ndio rais wa mkoa huu.
“Hakuna mwenye silaha wala hakuna anayetaka kuhatarisha amani hapa, tunaomba msaada wenu polisi, ili tumuone Mkuu wa Mkoa,” alisema mwanafunzi huyo.
Mwanafunzi mwingine alisema mbaya zaidi uongozi wa chuo umekaa kimya, hali inayochangia  baadhi ya wanafunzi kujiuza ili waweze kujikimu.
“Uongozi wa chuo umekaa kimya hadi leo na hawajaongea chochote, na inafikia kipindi hadi watoto wa kike wanajiuza na kama unabisha fanya uchunguzi, pita jioni maeneo ya baa utakuta watoto wa kike wako wengi hadi mahudhurio ya darasani yanakuwa si mazuri,” alisema.
Akizungumza na wanafunzi hao, Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mtwara, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi,  Ralph Meela, alisema amezungumza na mkuu wa chuo na kuwashauri kukutana na uongozi  huo kukutana na viongozi  wa wanafunzi hao na kuongozana nao katika ofisi wanayotaka kwenda.
Baada ya kukubaliana na wanafunzi hao, aliongozana nao na baada ya kuwapeleka katika ofisi ya mkuu wa mkoa walipelekwa kwa Kamanda wa Polisi Mkoa.

Ray C ahitaji mpenzi mzee

Ray C sasa ahitaji mpenzi mzeeMSANII wa muziki wa kizazi kipya, Rehema Chalamila ‘Ray C’, amesema kwa sasa hana mpango wa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mtu, na kama ikitokea basi atamtaka kuwa na miaka kuanzia 60.
Akizungumza katika kipindi cha ‘The Sporah Show’, Ray C alisema anahitaji wanaume wa umri mkubwa, kwa kuwa wanajua wanachokifanya, na kukiri kwamba vijana walichangia katika kurudisha nyuma maisha yake.
Msanii huyo ambaye kwa sasa ameanzisha asasi yake ya kupambana na dawa za kulevya, kutokana na yeye kuwa mmoja wa waathirika wa dawa hizo, alisema katika moja ya mambo anayoyajutia ni kuwa na mahusiano na vijana, jambo ambalo hataki kukumbuka walichomfanyia hadi kudhalilika mbele ya jamii.
Hata hivyo, alitumia fursa hiyo kuwaasa wazazi kutowatenga watoto wao ambao wamejidumbukiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya na badala yake, wawakumbatie na kuwaonyesha njia kama mama yake alivyofanya na kurudia hali yake ya kawaida.
Kuhusu kurudi kwenye muziki, Ray C alisema yupo mbioni na tayari ameshatengeneza nyimbo kadhaa, ambapo hivi sasa atakuwa akiimba miondoko tofauti tofauti, ikiwemo taarabu.
Katika kurudi kwenye muziki, jambo la kwanza alisema anatarajia kupunguza mwili wake kwa kufanya mazoezi, kwani hata daktari wake alishamwambia anatakiwa kupungua kutokana na umri wake kutoendana na kilo alizonazo.
Alipoulizwa mwanamuziki ambaye kwa sasa anamkubali Bongo, Ray C alisema wa kwanza ni AT akifuatiwa na Recho kutoka Jumba la Kukuza Vipaji (THT).

Wabunge watuhumiana wizi

Sendeka: Muhongo, Maswi weziWABUNGE jana waligeuza Ukumbi wa Bunge sehemu ya mnyukano baada ya baadhi yao kushambuliana, huku wakituhumiana kwa wizi na wamehongwa na uongozi wa Kampuni ya kufua umeme wa dharura ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) na Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), jana waliwasha moto na kuibana serikali kutaka iunde Tume Maalumu kuchunguza kashfa ya ufisadi wa zaidi ya sh bilioni 200 zilizohifadhiwa kwenye akaunti ya Escrow ndani ya Benki Kuu (BoT).
Mbali ya kutaka Bunge liunde Kamati Teule kuchunguza ufisadi huo, wabunge hao kwa nyakati tofauti walitaka serikali ichunguze kifo cha aliyekuwa Waziri wa Fedha na Uchumi, William Mgimwa, kwani wakati fedha hizo zinakwapuliwa, waziri huyo alikuwa Afrika Kusini akiugua na alishakata kauli.
Msimamo wa wabunge hao, uliungwa mkono na Mbunge wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Christopher Ole Sendeka, ambaye alilitaka Bunge kuunda Kamati Teule kubaini ukweli wa kashfa hiyo.
Wabunge kwa nyakati tofauti waliwasha moto huo jana bungeni wakati wa mjadala wa hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa Fedha 2014/2015.
Akiwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Msemaji Mkuu wa Kambi hiyo, Mnyika, alisema kuwa wezi wa fedha za Escrow wako ndani ya Bunge hilo na maelezo yoyote kuwa  taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ifanye uchunguzi haitaungwa mkono na kambi ya upinzani kutokana na historia yake.
Huku akiungwa mkono na wabunge wote wa kambi ya upinzani, alisema Takukuru iliwahi kutumika kusafisha sakata la Richmond, hivyo hawana imani kama inaweza kuja na matokeo ya uchunguzi sahihi ya kashfa hiyo.
Alisema Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa (CAG), nayo ilihusika kumsafisha aliyekuwa Katibu Mkuu David Jairo, katika kashfa ya kugawa fedha kwa wabunge ili waiunge mkono na kupitisha Bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Akaunti hii ilifunguliwa ili fedha ambazo Tanesco ilipaswa kuilipa IPTL kwa ajili ya tozo za uwekezaji ‘Capacity Charge’ ziwekwe hadi pale mgogoro huo utakapomalizika.
Mnyika, alisema kwa mujibu wa taarifa ya Gavana wa Benki Kuu, Benno Ndullu, aliyotoa katika kikao cha Kamati ya Uchumi ya Bunge kilichofanyika Bagamoyo, alikiri kuwa alibanwa na viongozi wa juu kiasi cha kushindwa kufurukuta.
Alisisitiza kuwa kauli za viongozi waandamizi wa serikali na Shirika la Umeme nchini kwa nyakati tofauti  kuhusu sakata hilo, zimezidisha utata na kuchochea dhamira ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kutaka iundwe Kamati Teule ya Bunge kuchunguza.
Mnyika alihitimisha hoja yake kwa kukumbusha kwa mujibu wa Mtume Muhamad (SAW) aliyesema kuwa mnafiki ni mtu mwenye nyuso mbili, ndani yake na nje yake ni tofauti na alama zake ni tatu: akizungumza husema uongo, akiahidi hatimizi na akiaminika hufanya hiyana.
“Mheshimiwa Spika, unafiki uachwe kwenye mjadala wa mwaka huu tuweze kuishauri na kuisimamia serikali kwa niaba ya wananchi kwa kuzingatia maoni nitakayowasilisha.
“Mosi, spika aruhusu kabla ya mjadala huu kuendelea ziwekwe mezani nakala ya ripoti zote za kamati za uchunguzi kwenye sekta ya nishati na madini zilizoundwa na matokeo yake kutowasilishwa bungeni mpaka sasa.
“Pili, Wizara ya Nishati na Madini itakiwe kabla ya mjadala huu kuwasilisha kabrasha la majibu ya michango ya wabunge juu ya makadirio ya mwaka 2013/2014.
“Tatu, mara baada ya hoja hii kuamuliwa, naeleza kusudio la kuwasilisha hoja binafsi ya kutaka kuundwe kamati teule ya kuchunguza masuala tete na tata tuliyoyaeleza katika maoni haya ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
“Nne, Waziri Mkuu kwa mamlaka na madaraka yake kwa mujibu wa ibara ya 52 ya katiba ya nchi atakiwe katika mkutano huu wa Bunge kuelekeza serikali iwasilishe taarifa bungeni juu ya maazimio ya Bunge kufuatia uchunguzi uliofanyika kwa nyakati mbalimbali juu ya masuala yanayogusa sekta za nishati na madini kama tulivyoyaeleza,” alisema Mnyika.
Wakichangia hoja hiyo, Kafulila, alisema kama Waziri Muhongo na wenzake waliotuhumiwa katika kashfa hiyo ni wasafi, hawana sababu ya kuogopa kuundiwa Kamati Teule kuwachunguza.
Mbunge huyo ambaye ndiye aliyeibua kashfa hiyo bungeni, alisema ana ushahidi wa kutosha kuhusu kashfa hiyo na alipotakiwa na Spika Anne Makinda kuwasilisha ushahidi alionao, aliinua begi zima lenye nyaraka alizodai zinahusu namna wizi huo ulivyofanyika.
“Mheshimiwa Spika, hakuna dhambi mbaya duniani kama unafiki. Kama kweli Bunge hili linataka kujua ukweli, tuunde Kamati Teule, watu wametoa bilioni 200 kumpa Singasinga ambaye kule Kenya alikumbwa na skandal ya Goldenberg iliyoiangusha Serikali ya Kenya.
“Ushahidi ninao, lakini kila nikitaka kuuleta spika anakatakata kona,” alisema Kafulila.
Alisisitiza kuwa kuunda Kamati Teule kuchunguza jambo hilo sio kumsaka mchawi, hivyo Waziri Muhongo na wenzake hawana sababu ya kuwa na wasiwasi.
Kafulila, ambaye aliwasilisha ushahidi wa tuhuma hiyo, alisema kwa nchi makini, serikali pia ilitakiwa kufanya uchunguzi wa kifo cha Waziri Mgimwa, kwani wakati amezidiwa na ugonjwa nchini Afrika Kusini, huku nyuma fedha hizo zilichotwa kwenye akaunti hiyo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Simanjiro, Ole Sendeka, alipigilia msumari kutaka Bunge liunde Kamati Teule kuchunguza ufisadi kwenye akaunti ya Escrow.
Sendeka ambaye ni mbunge pekee wa CCM mwenye msimamo unaofanana na kambi rasmi ya upinzani kwenye kashfa hiyo, alieleza jinsi fedha hizo zilivyohamishwa Benki Kuu kwenda Benki ya Standard Chartered na jinsi zilivyochotwa.
“Mheshimiwa Spika, kuna ushahidi wa namna vigogo walioshiriki kuchota fedha hizo, walihamisha dola milioni 5, (sawa na sh bilioni 8), siku nyingine watu wenye uhusiano na vigogo humu ndani walichota dola milioni 2, sawa na bilioni tatu), mara tano kwenye mifuko ya rambo na kusafirisha kinyume cha sheria ya kutakatisha fedha,” alisema Sendeka.
Huku wabunge wa CCM wakimshangaa, Sendeka kwa kujiamini zaidi alisema atawashangaa sana wabunge wa CCM watakaopinga kuundwa kwa tume hiyo ili kujua ukweli.
Jioni, Sendeka alisema ana ushahidi wa wezi wa Tanzania ambao badala ya kuwajibishwa wamekuwa wakipandishwa vyeo na wengine wamo ndani ya Bunge akiwemo Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wake, Eliakim Maswi.
“Ninao ushahidi hapa unaonyesha fedha zilizochotwa Tanesco, wizara, BoT na hata nikipigwa risasi nitaendelea kushikilia msimamo huo… nitakupa  ushahidi huo,” alisema.
Mnyika awasilisha ushahidi
Baada ya kutakiwa na spika kuwasilisha ushahidi mezani, Mnyika aliwasilisha nyaraka mbalimbali kuthibitisha kashfa hiyo ya akaunti ya Escrow.
Utoaji wa fedha za Escrow
Fedha za Escrow zilizotokana na malipo ya ‘capacity charges’, zilikuwa katika makundi mawili; moja ni fedha za Kitanzania na za dola za Marekani.
Kufikia Novemba 25, 2013, salio katika dola za Marekani, pamoja na faida lilikuwa ni dola 22,198,544.60, wakati salio katika fedha za Kitanzania lilikuwa ni sh 161,389,686,585.34, likijumuisha na faida katika uwekezaji ambayo ilikuwa sh 5,297,550,682.04.
Ulipaji wa fedha za Escrow kwa IPTL
Kutokana na maelekezo ya IPTL, Novemba 28, 2013 fedha taslimu, dola za Marekani 22,198,544.60 na shilingi 8,020,522,330.37 zililipwa katika akaunti iliyotolewa na IPTL.
Desemba 5, 2013 BoT ilihamisha Hati Fungani (Treasury Bond) yenye thamani ya sh  153,369,164,254.97 kwenda IPTL na kuhitimisha jukumu la BoT la kuwa wakala wa Escrow.
Desemba 19,  2013, BoT iliiomba Wizara ya Fedha kufunga rasmi akaunti ya Escrow kwa vile madhumuni ya kufunguliwa kwake yalifika mwisho.
Malipo ya Tanesco kwa IPTL
Wakati wa kufunga akaunti ya Escrow Desemba, 2013 Tanesco ilikuwa ikidaiwa na IPTL  dola za Marekani milioni 79.05 sawa na shilingi bilioni 125.04 zilizotokana na ununuzi wa umeme (Capacity Charge) ambazo hazijalipwa.

Friday 30 May 2014

Boko haramu wateka viongozi wawili

Watu  wenye  silaha wanaoshukiwa  kuwa  ni  kutoka  kundi la  Kiislamu  la  Boko  Haram wamewateka  nyara  viongozi wawili wa   kikabila  wa  Kiislamu  kaskazini  mashariki  ya Nigeria  leo.  Watu  hao  wenye  silaha  wamewateka mtawala  wa  eneo  la  Gwoza, Alhaj Idriss Timta , na mtawala  wa  Uba, Alhaj Ismaila Mamza, waliokuwa  katika magari  yao  katika  mji  wa  Zhur, eneo  la  ndani  katika eneo  la  kusini  mwa  jimbo  la  Borno. Duru  za  kiusalama na  afisa  wa  jimbo  la  Borno  ameliambia  shirika  la habari  la  Reuters  kuwa  watu  hao  walikuwa  wakielekea katika  mazishi.  Duru moja  ilisema  kuwa  jeshi  limewekwa katika  eneo  hilo  kuwatafuta  mateka , licha  ya  kuwa ujumbe  kama  huo  kila  mara  huambatana  na  hatari kubwa.

Matumizi ya Mabavu yasika kasi Afrika ya Kati

Hali inatisha katika mji mkuu wa jamhuri ya Afrika Kati-Bangui ambako vizuwizi vimewekwa majiani na mapigano kuripotiwa kati ya vijana na vikosi vya polisi huku maelfu wakiandamana kudai serikali ya mpito ijiuzulu.
Wananchi wanafuatilizia hali namna ilivyo nchini mwao kupitia Radio
Mizinga kadhaa imefyetuliwa katika eneo la kati la mji mkuu wa jamhuri ya Afrika Kati -Bangui,karibu na kasri la rais katika wakati ambapo makundi ya waandamanaji waliongozana majiani.Kwa mujibu wa shirika la habari la Ufaransa AFP,hali ilitulia kidogo saa moja baadae baada ya waandamanaji kulihama eneo hilo.
Katika mitaa mengine na hasa karibu na uwanja wa ndege,mikururo ya watu wanaandamana wakidai serikali ya mpito ijiuzulu,wanajeshi wa kigeni waihame nchi hiyo na hasa wale wa kutoka Burundi wanaotuhumiwa kuwachia matumizi ya nguvu dhidi ya waumini wa dini ya kikristo.Watu wawili wanasemekana wameuwawa na wengine kadhaa kujeruhiwa kufuatia mapigano kati ya waandamanaji na vikosi vya kulinda amani vya kutoka nchi za Afrika Misca mjini Bangui.
Mji mkuu Bangui umejiinamia
Vifo na Majeruhi kufuatia mapigano mjini Bangui
 Vikosi vya jeshi na polisi vimefyetua risasi hewani kuwatawanya waandamanaji.Vizuwizi vimewekwa majiani katika mitaa kadhaa ya mji mkuu.Hakuna magari yanayozunguka na,maduka yamefungwa.Mji mkuu mkuu huo umejiinamia helikopta ya kijeshi ya Ufaransa tu ndio inayopiga doria.Vikosi vya Ufaransa Sangaris na vile vya Misca vya kutoka nchi za Afrika vimeonya "vitapambana kikamilifu na aina yoyote ya mapendeleo".Vikosi hivyo vimetoa wito waa utulivu mjini Banguii.
Matumizi ya nguvu yamepamba moto tangu siku kadhaa sasa katika mji mkuu huo wa jamhuri ya Afrika Kati.Vizuwizi kadhaa viliwekwa katika njia muhimu na mapigano kuzuka kati ya vijana na vikosi vya nchi za Afrika kufuatia shambulio la kanisani lililoangamiza maisha ya watu wasiopungua 15.
Waziri mkuu André Nzapayéké anasema kuzidi nguvu machafuko "ni njama iliyoandaliwa" na "wanasiasa walio karibu na serikali."
"Kuna baadhi ya wanasiasa wanaoingia majiani wakidai serikali ijiuzulu,watu walio karibu na serikali,na karibu na rais wa mpito na baraza la mawaziri"Anasema waziri mkuu huyo.
Miito ya walimwengu dhidi ya matumizi ya nguvu
Rais wa mpito Sanba -Panza na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon wakihudhuria mkutano wa kilele Kati ya Umoja wa ulaya na Afrika,mapema mwezi uliopita wa April
Umoja wa Ulaya unasema umeingiwa na wasi wasi wasi kutokana na hali namna ilivyo na kuwataka viongozi waendeleze bila ya kuchoka juhudi za kuleta suluhu ya taifa.
Kwa upande wake katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Ban ki-Moon amelaani vikali mashambulio yanayoendelea ikiwa ni pamoja na lile dhidi ya kanisa kuu la Fatima mjini Bangui.

Marekani ya sisitiza kuwa itaendelea kusaidia upinzani Syria

marekani-yaendelea-kuunga-mikono-upinzani-syKatibu wa Jimbo la Marekani Jhon Kerry alisema kwenye Televisheni ya PBS kwamba Marekani itaendelea Kusaidia upinzani na aliongeza kuwa Rais Bashar al-Assad hana mahali katika siku zijazo ya Syria.

 Kerry  aliongeza kuwa Marekani itakuwa inaongeza msaada wake  kusaidia upinzani  na kuwa mchakato wa uchaguzi ambayo ilianza katika Syria hauna uhalali.
Wakati huo huo,  ndege za kivita za Syria zinaendelea kurushia  mabomu kwenye  eneo  linalodhibitiwa na  upinzani katika Syria na kuleta uharibifu mkubwa.
Umoja wa Mataifa  ilisema kuwa  kufanya uchaguzi katika mazingira hayo ya machafuko  itawezesha mvutano zaidi katika nchi

Mchawi Mtanzania ahukumiwa kifungo cha Miaka 3 Kenya

Vifaa walivyopatikana navyo washukiwa walipokamatwa na polisi

Mchawi kutoka Tanzania amehukumiwa kifungo cha miaka mitatu nchini Kenya kwa kumlaghai mwanamke mfanyabiashara mkenya na kumwibia shilingi milioni tisa.
Mchawi huyo alimhadaa mama huyo kuwa kwa kupitia njia za kichawi angeweza kuzifanya pesa hizo kuwa maradufu yaani milioni 18.
Bwana Amos Chipeta pia ataongezwa kifungo cha miezi tatu kwa kupatikana na vifaa vinavyoumiwa kufanya uchawi kama vile chupa, visu na ngozi ya Paka.
Kwa mujibu wa mtandao wa Daily Nation, Chipeta alihukumiwa pamoja na mwenzake bwana Peter Christopher aliyepatikana na hirizi zinazotumika kufanyia uchawi.
Bwana Chipeta alimlaghai Bi Catherine Njeri hela zake tarehe tofauti tofauti kati ya mwezi wa Agosti na Decemba 2012 baada ya mwanamke huyo kuwaendea na kumwomba wazifanye pesa hizo ziwe maradufu
Walijitetea kwa kusema kuwa mwanamke huyo aliwaendea ili wampe nguvu za kichawi aweze kuwashinda wapinzani wake wa kisiasa
Maafisa wa polisi walipata hirizi hizo na vifaa walivyotumia kwa uchawi mwezi Februari 1, 2014 katika nyumba ya kukodisha iliyo kando ya barabara ya Juja viungani mwa mji mkuu Nairobi.
Hakimu aliyesikiliza kesi hiyo alisema kuwa wanaume hao waliona mwanamke huyo kuwa mjinga na basi kumnafiki kwa urahisi na kuwa hawana majuto au toba.

Thursday 29 May 2014

Abdel Fattah El Sissi anatarajiwa kushinda uchaguzi wa rais Misri.

Mkuu wa zamani wa jeshi Misri Abdel Fattah El Sissi anaongoza katika kura za rais wa Misri.Mkuu wa zamani wa jeshi Misri Abdel Fattah El Sissi anaongoza katika kura za rais wa Misri.


Matokeo ya awali ya uchaguzi wa rais huko Misri yanaonyesha mkuu wa zamani wa jeshi Abdel Fattah El Sissi anaelekea kupata ushindi mkubwa.

Matokeo ya kwanza yamempa Sissi kiasi cha asilimia 93 ya kura wakati mgombea mwingine mwenye mrengo wa kushoto Hamdeen Sabahi ana kiasi cha asilimia 3.

Waliojitokeza kupiga kura walikuwa wachache kiasi cha asilimia 44 hata baada ya wapiga kura kupewa siku moja ya ziada kuweza kupiga kura.Matokeo kamili yanatarajiwa wiki ijayo.

Chama cha Muslim, Brotherhood kiliwasihi  watu wagomee uchaguzi.Kinamshutumu Sissi na washirika wake kwa wizi wa kura na ujanja. Wameita urais wa Sissi ni muendelezo wa jeshi kuchukua madaraka huko Misri ambayo yalianza  mwaka jana wakati jeshi lilipomtoa madarakani  Mohamed Morsi.

China yaruhusu wananchi wake kuzaa watoto wawili badala ya Mmoja


Serikali-Kila Mchina sasa ruhsa kuzaa zaidi ya mtoto mmoja
Uchina imeanza kulegeza sheria zake za mpango wa uzazi, na sasa inapiga kampeni yenye lengo la kuongeza angalau watoto millioni mbili zaidi wanaozaliwa kila mwaka.
Serikali itaongeza wakunga na wahudumu sambamba na kupanua nafasi hospitalini na kuongezwa idadi ya vitanda na vifaa nyenginevyo.
Kwa mda mrefu Uchina imeendeleza sera kali ya mpango wa uzazi ya kulazimu familia kuwa na mtoto mmoja tu huku wanaokiuka wakichukuliwa hatua kali jambo linaloshutumiwa kimataifa.
Lakini mwaka jana serikali iliianza kulegeza kamba kwa kusema iwapo mmoja wa wazazi amekuwa mtoto wa pekee katika familia basi anaweza kuzaa mtoto wa pili.
Japo hatua za awali zilichukuliwa kukabiliana na idadi kubwa ya watu nchi humo, sasa kumetokea mapungufu ambayo yanahitaji kusawazishwa.
Baadhi ya wachina katika kituo cha reli wakisubiri usafiri. Uchina ina idadi kubwa zaidi ya watu duniani zaidi ya watu billioni moja.
Wapanga sera wamependekeza juhudi hizo za kuongeza idadi ya watoto zichukuliwe sasa la sivyo Uchina itajikuta na upungufu mkubwa wa nguvu kazi za vijana,huku idadi ya wazee na wanaostaafu ikiwa kubwa kiasi chakuzorotesha uchumi wa taifa hilo kubwa duniani.Japo bado umaskini unakumba baadhi ya raia wake,Uchina imepata mafanikio makubwa ya kiuchumi mnamo siku za hizi karibuni na sasa ndilo taifa la pili kwa utajiri duniani,baada ya Marekani.
Hatua hiyo mpya pia huenda ikaleta afueni kwa wengi kwani sera hiyo ya mtoto mmoja kwa familia ilikabiliwa na changamoto nyingi.
Visa na mateso kwa baadhi ya wazazi na watoto huripotiwa huku watoto vilema, wagonjwa au wa jinsia isiyopendelewa na wazazi wao kubaguliwa na kutelekezwa.

Wednesday 28 May 2014

watu 40 wauawa katika mji wa Donetsk ; UKRAINE

Mwanaharakati anaeunga mkono urusi, katika mji wa Donetsk, mashariki mwa Ukraine.
Mwanaharakati anaeunga mkono urusi, katika mji wa Donetsk, mashariki mwa Ukraine.

Watu 40, wakiwemo wapiganaji 38 na raia wawili wameuawa jumanne hii katika mapigano kati ya jeshi na waasi wa Ukraine yalioanza jumatatu wiki hii katika jitihada za kujaribu kilia upande kudhibiti uanja wa ndege wa Donetsk katika eneo la mashariki, mkuu wa manispa ya jiji la Donetsk amethibitisha.


Helikopta ya jeshi la Ukraine aina ya Mi-24 ikitumiwa katika mapigano ili kujaribu kuondoa uwanja wa ndege wa Donetsk mikononi mwa waasi waliyouteka hivi karibuni, Mei 26 mwaka 2014.
Viongozi wa Kiev wamethibitisha kwamba wameurejesha kwenye himaya ya utawala uwanja huo.
Wakati huo huo Urusi imetoa wito wa kusitishwa kwa mapigano haraka iwezekanavyo katika mji wa Donetsk, mashariki mwa Ukraine.
“ Jukumu la kwanza na mshikamano wa viongozi wa

Waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi, Sergueï Lavrov akitolea wito pande zote kusitisha mapigano nchini Ukraine.
Kiev, kufuatia matokeo ya uchaguzi wa urais, ni kusitisha kutumia jeshi kwa kukandamiza raia pamoja na pande zote mbili kusitisha machafuko, amesema waziri wa mambo ya kigeni wa urusi”, Sergueï Lavrov.
Hato yakijiri waziri mkuu wa Ukraine Arseni Iatseniouk, ametupilia mbali uwezekano wa kuanzisha mazungumzo ya moja kwa moja na Urusi ili kujaribu kukomesha machafuko ambayo yanaendelea kuathiri taifa la Ukraine, bila hata hivo kuweko kwa wasuluhishi kutoka mataifa ya magharibi.

Waziri mkuu wa Ukraine Arseni Iatseniouk amekataa katakata mazungumzo na Urusi.
“Kwa sasa mazungu kati ya Urusi na Ukraine hayawezekani iwapo Marekani na Umoja wa Ulaya havitaashirikishwa” amesema Iatseniouk katika kikao cha baraza la mawaziri, huku akibaini kwamba wanahofia kudanganywa na Urusi iwapo wataketi pamoja kwenye meza ya mazungumzo.
Jumatatu wiki hii rais mpya wa Ukraine Poroncheko amethibitisha kwamba amekua na matumaini ya kukutanakwa mazungumzo na rais wa Urusi Vladimir Putin, na mkutano huo ungeliandaliwa katikamwezi ujao.

UDA yawavua wabunge nguo

 Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe SAKATA la umiliki wa Shirika la Usafiri jijini Dar es Salaam (UDA), limeiingiza serikali katika aibu ya mwaka, huku mawaziri na wabunge ‘wakivuana nguo’ bungeni.
Hali hiyo iliyosababisha baadhi ya wabunge kuishambulia serikali, ilitokea juzi wakati wa mjadala wa hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
Waliohitimisha mnyukano huo kwa kauli za kuumbuana ni Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe na Naibu Spika Job Ndugai.
Dk. Mwakyembe, akihitimisha mjadala huo, alisema suala la umiliki wa UDA halina uhusiano na wizara yake, hivyo alimlaumu Naibu Spika Ndugai, kuruhusu mjadala huo kwenye wizara yake, huku Naibu Spika huyo akifoka na kusisitiza wizara hiyo inahusika.
Awali kabla ya mzozo wa UDA haujaanza juzi, Waziri Mwakyembe, wakati akijibu hoja za Waziri Kivuli na Msemaji Rasmi wa Kambi ya Upinzani wa wizara hiyo, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), aliyehoji sakata la UDA, aliweka bayana kwamba suala la umiliki wa shirika hilo halihusu wizara yake.
Hata hivyo, pamoja na kuweka angalizo hilo mapema na wakati Bunge likiendelea, Mbunge wa Nzega, Dk. Khamis Kingwangala (CCM), aliliibua sakata hilo na kusema kuwa mmiliki wa UDA, Robert Kisena, alinunua kihalali.
Dk. Kingwangala, alitoa kauli hiyo akijua fika kwamba siku chache zilizopita, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alilipeleka suala la UDA mbele ya Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge kumhoji Kisena kwa kauli yake kwamba wabunge waliopinga umiliki wa UDA, wamehongwa na mwekezaji wa nje anayetaka kuinunua.
Sambamba na hilo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Frederick Werema, amepata kuliambia Bunge wiki iliyopita kuwa sakata la umiliki wa UDA limepelekwa tena mbele ya Taasisi ya Kudhibiti na Kuzuia Rushwa (Takukuru) na Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kwa hatua zaidi za kisheria.
Mbali na viongozi hao, Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Adam Malima, wiki iliyopita wakati akijibu swali la Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (CHADEMA), alisema UDA inamilikiwa na serikali kwa asilimia 49 ya hisa na Jiji la Dar es Salaam asilimia 51, na kwamba mmiliki wa sasa, Kampuni ya Simon Group chini ya Kisena hana umiliki wa hisa.
Akijenga hoja yake juzi bungeni, Dk. Kingwangala, alisema mmiliki wa UDA, Kisena amekuwa akinyanyaswa kutokana na kauli tata za serikali.
Huku akisoma nyaraka za kuhalalisha umiliki wa UDA kwa Kisena, mbunge huyo alitaka serikali itoe kauli juu ya sakata hilo na kama asingepata majibu ya kuridhisha, angekwamisha Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi.
Hoja hiyo iliungwa mkono na wabunge wengi, akiwemo Mbunge wa Mwibara, Kange Lugola (CCM), aliyemshangaa Waziri Mwakyembe kwamba suala la UDA halihusiani na wizara yake.
Lugola, alisoma moja ya barua ya Wizara ya Uchukuzi wakati huo ikiitwa Wizara ya Miundombinu, ikitoa maelekezo kuhusu suala la UDA, hivyo alisisitiza kuwa wizara hiyo inahusika na kumtaka waziri atoe kauli juu ya mzozo huo.
Huku akishangiliwa na baadhi ya wabunge, Lugola alisema mwekezaji huyo amekuwa akizungushwa kama mchezo wa ‘Joyce Wowowo’ huku wizara husika zikitupiana mpira.
Alisema wenye hisa, yaani Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wameamua kuuza hisa zao kwa Kisena, lakini aliishangaa serikali imekuwa ikitoa maelezo aliyoyaita ya kukengeuka.
Wakati mzozo ukiendelea, Waziri Malima alisimama kutoa ufafanuzi wa kauli yake ya awali ya umiliki wa hisa za UDA ambapo alisisitiza kuwa serikali haimtambui Kisena kwani alilinunua shirika hilo kiujanja.
Mpira wa hoja hiyo ulimrukia Mbunge wa Kilwa Kaskazini, Multazar Magungu (CCM), aliyesema kama mnunuzi alikosea, serikali imlipe fidia na kulirudisha shirika hilo mikononi mwake na kisha kuliuza upya.
Alisema kwa sasa wanaomtetea Kisena, wana maslahi yao na wanaopinga pia wana maslahi yao, hivyo serikali ikae chini kupata ufumbuzi wa tatizo hili.
Mbunge wa Kasulu Mjini, Moses Machali (NCCR-Mageuzi), alisema kama Kisena alinunua UDA kwa bei ya kutupwa, wa kulaumiwa ni serikali na sio mmiliki wake.
Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe, alisema kama kuna jambo limeivua nguo serikali, hili la umiliki wa UDA ni aibu ya mwaka.
Mbowe, alisisitiza kuwa jambo hili limeivua nguo serikali kwani kauli za viongozi wake zinagongana na kamati tano za Bunge zilizoshughulika na suala hilo, kila moja inasema lake.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, sijawahi kuona serikali imenywea kama leo kwenye hoja hii. Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji wa UDA ameingiza magari 300, serikali inamwona, kauli za viongozi wa serikali zinagongana, kamati tano kila moja inasema lake, leo mnakuja kuvuana nguo hadharani, hii ni aibu kwa serikali hii sikivu ya CCM.
“Ushauri wangu, kaeni chini mmalize utata huu badala ya kuvuana nguo bila sababu maana wananchi wa Dar es Salaam wanahitaji usafiri,” alisema Mbowe.
Kuona mzozo unazidi kuwa mkubwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema serikali haijajivua nguo katika suala hilo kwani maelezo yake yako wazi.
Alisema Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali (CAG), ipo na imesema wazi kwamba kuna utata wa umiliki wa UDA.
“Lakini pia si mnajua suala hili lipo Takukuru na kwa DPP. Pili Mnyika alilitolea mwongozo na jambo hili lipo mbele ya Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge kwa hatua zaidi,” alisema Lukuvi.
Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba (CCM), hakuridhika na majibu ya serikali ambaye katika mchango wake aliishangaa kusema haimjui mwekezaji Kisena wakati imetoa msamaha wa magari 300 aliyoyaingiza nchini bure bila kodi.
“Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Kingwangala kuhusu mmiliki wa UDA. Mwekezaji huyo ameingiza magari 300, yakatolewa bure bila kodi, leo serikali hii hii inasema haimjui. Mmeenda mahakamani, ameshinda kesi, mahakama imewaachia huru. Hili suala liangaliwe upya, huyo mwekezaji ni mwenzetu, ngozi nyeusi (Mzawa), tumwache,” alisema Serukamba.
Sakata la UDA lilihitimishwa kwa malumbano makali kati ya Naibu Spika Ndugai na Waziri Mwakyembe.
Ndugai, alipompa nafasi Mwakyembe kujibu hoja za wabunge kuhusu UDA, waziri huyo aling’aka huku akikunja sura kwamba wizara yake haihusiki na UDA.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nieleze masikitiko yangu kwa kuruhusu mjadala wa UDA ambao hauhusiani kabisa na hoja yangu. Mimi sijawahi kuliona faili la UDA likija mezani pangu, unataka nijibu nini hapa? Hatuhusiki ndio maana tangu awali nilisema hili halituhusu.”
Kuona hivyo, Ndugai alisimama kwenye kiti chake na kufoka: “Suala hili linahusu Wizara ya Uchukuzi na mada iliyopo inahusu uchukuzi ndiyo maana leo wamekuja madereva wa malori, kwa hiyo linawahusu. Lakini jambo hili linatuhusu sote, kwa hiyo serikali ikae ije na majibu kumaliza utata huu,” alisema Ndugai na kufunga mjadala wa UDA.
Mjadala nje ya Bunge
Baada ya mjadala wa UDA kumalizwa bungeni kwa kufuata ushauri wa Mbowe aliyeitaka serikali ikae chini kumaliza utata huo, nje ya ukumbi wa Bunge kulikuwa na vituko vyake.
Baadhi ya wabunge na mawaziri walisimama kwenye vikundi kujadili kilichojiri bungeni kuhusu suala la UDA.
Mshangao wa kwanza ulielekezwa kwa Naibu Spika kuruhusu mjadala huo huku akijua fika kwamba Spika Makinda, alishalitolea maamuzi na serikali kupitia kwa AG Werema ilieleza kwamba jambo hili lipo Takukuru.

Wanamgambo 11 wa Boko Haramu wauwawa


Wasichana wanaozuiliwa na Boko Haram
Taarifa kutoka mjini Buni Yadi katika jimbo la Yobe Kaskazini mwa Nigeria, zinasema kuwa watu 24 wakiwemo wanajeshi 11 wameuawa katika shambulizi dhidi ya kambi za wanajeshi.
Inaarifiwa kuwa kundi la Boko Haram ndilo linashukiwa kufanya mashambulizi hayo.
Wakaazi wanasema washambuliaji waliwasili katika eneo hilo kwa magari kumi ya kawaida na gari moja la kijeshi.
Waliwaambia wanakijiji kutokuwa na hofu kwani nia yao haikuwa kuwadhuru raia bali maafisa wa usalama.
Wanajeshi 11, polisi 13 akiwemo mwanamke mmoja waliuawa.
Pia waliteketeza majengo na magari ikiwemo makazi ya kiongozi mmoja wa kijadi na kituo kimoja cha polisi.
Taarifa zaidi bado zinajitokeza pole pole hasa kwa kuwa mawasiliano yamekuwa magumu kutokana na miundo mbinu mibovu.
Jimbo la Yobe ni moja ya majimbo matatu ambayo serikali imeweka sheria ya kutotoka nje usiku. Licha ya sheria hiyo mashambulizi ya mara kwa mara yamekuwa yakishuhudiwa mengi yakifanywa na Boko Haram.

Tanzania yahushisha M23 na Rwanda kwa mara nyingine


Waasi wa M23
Tanzania kwa mara ya Kwanza imesema inayo uhakika kuwa waasi wa M23 walioondolewa nchini Jamuhuri ya Kongo ni ni raia Rwanda.Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Benard Membe ameliambia Bunge la Tanzania kuwa anao uhakika kuwa waasi M23 walitokea nchini Rwanda.
Hii ni Mara kwanza kwa Tanzania kukiri hadharani kuwa inao uhakika kuwa waasi hao ni raia wa Rwanda.
Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimepeleka majeshi Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambayo kwa kushirikiana na yale ya umoja wa Mataifa yaliwaondoa waasi hao DRC
Benard Membe Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania

Matamshi hayo ya Waziri huyo aliyatoa wakati alipokuwa akiwasilisha hotuba ya Bajeti ya Wizara yake ambapo pia alikiri kuwa bado uhusiano wa Tanzania na Rwanda sio mzuri.
Hata hivyo upande wa Upinzani mlishambulia Waziri huyo wa Mambo ya nje Benard Membe wakidai kwamba Waziri huyo anachochea kuvurugika kwa uhusiano wa Watanzania na Rwanda kwa kuhisi kuwa M23 ni Wanyarwanda nahata kutaka achukuliwe adhabu kali.
Mbali na tuhuma hizo Waziri Membe alizidi kusisitiza kuwa waasi wa M23 ni raia wa Rwanda akisema hiyo ni ripoti ya Umoja wa Mataifa.
Mbali na waziri baadhi ya wabunge wanamuunga mkono waziri Membe kuwa waasi wa M23 ni raia wa Rwanda wao.
Matamshi haya Waziri wa Tanzania kuhusu M23 bado haijulikana ni kwa namna gani utaathiri uhusiano wa Tanzania na Rwanda kama utakuwepo huenda ukajulikana hapo baadae.

Membe amponda wenje


Huwezi kusimama hapa mtu na macho yakakutoka halafu unaanza kulizungumzia taifa lingine ambalo siyo lako, hivi unatoa wapi ujasiri huo au wanakulipa,”alihoji Membe na kuongeza

Wakati Bunge likipitisha bajeti ya makadirio ya matumizi Sh191.91 bilioni ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa mwaka wa fedha 2014/15 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, alitumia nafasi hiyo ‘kumchana’ Ezekiel Wenje na kusema kuwa anatumiwa na mataifa ya nje.
Mbali na hivyo aliwaita watu wanaotoa kauli za uchonganishi kuwa ni wapumbavu na akataka waache tabia za kipumbavu kwani hawatavumiliwa hata kidogo.
Membe alitoa kauli hiyo jana jioni wakati akitoa majumuisho katika michango ya wabunge kwenye hotuba ya mapato na makadirio ya wizara hiyo kwa mwaka 2014/15.
Wenje ambaye ni Waziri Kivuli wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa jana asubuhi katika hotuba yake, alimshambulia Membe kuwa ni waziri mzigo ambaye hajui wajibu wake.
Sakata hilo liliibuliwa kwenye uhusiano baina ya Tanzania na nchi ya Rwanda ambalo Wenje alilizungumzia zaidi.
Akijibu hoja hizo Membe, alisema: “Kwanza nikubaliane na kauli ya wabunge wengi kuwa uhusiano wa Tanzania na Rwanda siyo mzuri kwani kila upande haumuamini mwenzake,” aliema Membe.
Alisema kinachowaumiza pande zote ni kuwa kila upande unapozungumza na mahasimu wa mwenzake, wanahisi kuwa anataka kuipindua Serikali yao hivyo bado hawajakubaliana kwa jambo lolote lakini akasema yote yatakwisha salama.
“Huwezi kusimama hapa mtu na macho yakakutoka halafu unaanza kulizungumzia taifa lingine ambalo siyo lako, hivi unatoa wapi ujasiri huo au wanakulipa,”alihoji Membe na kuongeza.
“..Mimi naweka rehani uwaziri wangu hapa kwamba ukileta vielelezo kamili mimi nitakuwa tayari kuachia nafasi yangu, je na wewe nikitoa vielelezo utakuwa tayari kuwajibika.”
Alimtaja Wenje kwa jina kuwa alichokifanya hakifai kuwa alitoa kauli ambayo siyo nzuri kwa siri za taifa na akasema mtu kama huyo akipata nafasi hata kama nchi itakuwa vitani, yuko tayari kutoa siri.
Aliyataja makundi ya ya M23 kuwa ni moja ya kundi ambalo linaundwa na Banyamulenge waliokuwa chini ya Roral Nkunda pamoja na kundi la FDRA ambalo liliua watu wengi kwamba linaundwa na Wahutu bila ya ubishi.
Membe alimpongeza mbunge Alli Keissy kuwa alichokizungumza jana asubuhi kuhusu Rwanda na DRC Kongo ni sahihi na ndiyo maana alimshangilia kwa nguvu zote.

Obama asema wanajeshi 10,000 kubakia Afghanistan

Rais Obama akitangaza kubakia kwa wanajeshi 10,000 katika Ikulu ya White House Mei 27, 2014.
Rais Barack Obama ametangaza kuwa Marekani itaendelea kuwa na wanajeshi 10,000 nchini Afghanistan baada ya mwisho wa mwaka 2014.
Alitangaza kuwa Marekani kisha itaendelea kuwapunguza wanajeshi hao ili kufikia mwaka 2016 kuwe kumebakia na wanajeshi wachache sana.
Rais Karzai amekuwa akipinga kila hatua au pendekezo linalotolewa na maafisa katika utawala wake hasa kuhusiana na uwezekano wa kuendelea kuwepo na wanajeshi wa Marekani nchini humo baada ya mwisho wa mwaka huu.
Wakuu wake wa kijeshi, washauri wa maswala ya usalama na Mawaziri wake wengi, wangalitia sahihi mapatano ya usalama na Marekani mwaka uliopita.
Lakini yeye, hata baada ya kuitisha mkutano wa wazee uliotazamiwa kuidhinisha mapatano hayo alikiuka matarajio ya wengi na kusema kuwa hatii sahihi mapatano hayo.
Wagombeaji wa Urais wawili waliosalia kwenye kinyanganyiro cha Urais kuchukua nafasi yake Karzai wanaunga mkono mapatano ya usalama na Marekani na hiyo ndiyo sababu Rais Obama ametoa tangazo lake kuhusu wanajeshi watakaobakia nchini humo, ikiwa yamebakia majuma mawilli kabla ya awamu ya mwisho ya upigaji kura nchini humo.
Hata hivyo kusita kwa Rais Karzai kutia sahihi mapatano hayo kumeimarisha kampeni ya wale nchini Marekani wasiotaka kuendelea kuwepo wanajeshi wa Marekani nchini Afghanistan.
Sasa wanajeshi watakaobakia Afghanistan watakuwepo kwa mwaka mmoja pekee kabla ya kupunguza idadi hiyo kwa nusu halafu baadaye kupunguza hadi sufuri ifikapo mwisho wa mwaka 2016.
Maoni ya wengi hapa ni kuwa ni heri wanajeshi wa Marekani waendelee kuwa nchini humu kwa muda mrefu zaidi.
Mapigano yametokea nchini humu mara kwa mara hivi kwamba kuwepo kwa wanajeshi wa kigeni nchini kungetoa hakikisho zaidi kwa wananchi.

Tuesday 27 May 2014

Wapiganaji 30 wauawa nchini Ukraine

Wapiganaji wanaounga mkono Urusi wakijinadaa kuvamia uwanja wa ndege wa Donetsk
Takriban wapiganaji 30 wanaounga mkono Urusi,wameuawa katika mapigano yaliyozuka katika uwanja wa ndege mjini Donetsk,Mashariki mwa Ukraine.
Mapigano yalizuka baada ya wapiganaji hao waliokuwa wamejihami wakiunga mkono kujitenga kwa mji wa Donetsk kutoka kwa Ukraine
Wapiganaji hao walijaribu kuuteka uwanja huo mnamo siku ya Jumatatu.
Waandishi walio karibu na uwanja huo wanasema walisikia milio ya risasi hata baada ya mashambulizi na ufyatulianaji wa risasi ingawa msemaji wa jeshi alisema kuwa hali ilikuwa imetulia.
Rais mpya Petro Poroshenko aliahidi Jumatatu kuwa operesheni dhidi ya makundi ya kile alichoita magaidi itakamilika baada ya saa chache wala sio miezi.
Mwakilishi wa mji wa Donetsk ambao tayari umejitangza kuwa taifa,  kwa taarifa ya vifo vya watu 30 ni za kweli.
Makabiliano makali katika uwanja wa ndege wa Donetsk
Mmoja wa wapiganaji aliambia shirika la habari la AP, kuwa miili hiyo ilipelekwa katika hospitali iliyo katibu na eneo la vita.
Waziri wa mambo ya ndani Arsen Avakov, amesema kuwa hapakuwa na majeruhi upande wa wanajeshi wa Ukraine.
Makabiliano yaliyozuka Jumatatu, yalianza baada ya wapiganaji wanaotaka kujitenga na Ukraine kuvamia uwanja wa ndege wa Sergei Prokofiev Donetsk mapema asubuhi.
Wakati huohuo,maafisa wa Ukraine wamedhibiti uwanja wa ndege mjini Donetsk mashariki mwa nchi hiyo huku idadi kubwa ya watu wakifariki. Hata hivyo, wandishi  walio nje ya kambi ya jeshi wanasikia milio ya risasi
Siku moja tu baada ya ushindi wa Rais mpya Petro Poroshenko, hali ya suitofahamu bado inaenea Mashariki mwa Ukraine.
Afisa mmoja wa serikali amesema kuwa operesheni dhidi ya wapiganaji hao itaendelea huku walinzi wa mipakani wakisema kuwa magari yenye wapiganaji waUk

Ziara za CCM zimejaa ufisadi

Ziara za CCM mikoani zikitumia fedha za HalmashauriWIMBI la matumizi mabaya ya fedha za umma limezidi kukiandama Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo hivi sasa kinatuhumiwa kutumia fedha za umma katika ziara na ukaguzi wa miradi.
Tanzania Daima imedokezwa kuwa kila ziara ya CCM inakofanyika, mkurugenzi wa halmashauri husika hutoa magari au fedha za kuwakirimu wahusika.
Imedokezwa kuwa miongoni mwa ziara ambazo zinatumia fedha za halmashauri ni inayofanywa hivi sasa mikoani na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
Inaelezwa kuwa ziara hizo hazipaswi kugharimiwa na fedha za serikali kupitia halmashauri mbalimbali kwakuwa zinatokana na wananchi wenye itikadi tofauti pamoja na wasio na itikadi.
Michango hiyo ndiyo inadaiwa kuwapa nguvu vigogo wa CCM na kuacha kupitisha bakuli kuomba misaada kwa makada wake kama ilivyozoeleka siku za nyuma.
Tanzania Daima limedokezwa kuwa vyama vya upinzani na CCM vimekuwa na utaratibu wa kuomba misaada kwa makada wao au wahisani, wafadhili wa ndani na nje ya nchi.
Hata hivyo, katika siku za hivi karibuni utaratibu huo unaonekana kutumiwa zaidi na wapinzani kutokana na kutokuwa na uwezo wa kuwaamrisha au kuwashawishi wakurugenzi wa halmashauri kugharimia ziara zao.
Ukombozi  iliwasiliana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, ambaye alisema kuwa taarifa hizo zinalenga kukichafulia jina chama tawala.
“Madai hayo ni ya kiupuuzi na kwamba misafara yetu inawaumiza viongozi wa CHADEMA, sisi tunapoamua jambo tunakuwa na mipango sambamba na kujitosheleza,” alisema.
Hata hivyo, Tanzania Daima limepata taarifa kuwa baadhi ya halmashauri ambazo Kinana na timu yake wameshapita ziligharamia malazi, chakula na usafiri wa ndani ikiwemo magari ya serikali kutumika.
Halmashauri ambazo taarifa zake zimekusanywa na gazeti hili ni pamoja na Nzega, Igunga na Uyui zilizopo mkoani Tabora na Iramba iliyopo mkoani Singida huku wakurugenzi wake wakikiri kutumia magari ya serikali na baadhi ya watumishi kuhudhuria katika ziara hiyo.
Katika Wilaya ya Igunga, msafara wa Kinana ulikaa kwa muda wa siku tatu ambapo halmashauri kupitia viongozi wa CCM wa wilaya hiyo waligharimia usafiri wa ndani, chakula na malazi pamoja na kukodisha pikipiki 50.
Pikipiki hizo zilitumika kumpokea Kinana na magari 10 yaliyotumika kuwabeba wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo waliotakiwa kuhudhuria mkutano wa hadhara uliofanyika mjini Igunga.
Mbali na gharama hizo, pia ziara hiyo inaelezwa kusimamisha kazi mbalimbali za kiutendaji katika maeneo wanayopita kutokana na watendaji wa serikali kutakiwa kuwa sehemu ya ziara hiyo.
Chanzo kutoka ndani ya Halmashauri ya Igunga, kilieleza kuwa mbali na gharama ya malazi, vyakula, usafiri na malazi, pia hakukuwa na malipo iliyolipwa na chama hicho kwa kutumia ukumbi wa halmashauri kufanya mikutano yake ya ndani.
Chanzo hicho kilieleza kuwa msafara wa Kinana ulikuwa na magari zaidi ya 28 na kila gari likiwekewa lita 80 za mafuta kutembelea maeneo mbalimbali.
Kigogo mmoja wa CCM, alidokeza kuwa walitakiwa kuandaa chakula cha watu 200 huku sahani moja ya chakula ikiuzwa kwa shilingi 5,500.
Alisema walikodisha pikipiki 42 kwa sharti la kila mwenye pikipiki aliyehudhuria mapokezi ya Kinana, atalipwa sh 7,000 na kuwekewa lita mbili ya mafuta.
Alibainisha pia walitakiwa wahakikishe msafara wa Katibu Mkuu unapatiwa malazi.
“Sisi chama tulibeba jukumu lile kwa kuwa ni ugeni wa chama, lakini hakuna hata senti moja tuliyotumia kutoka mfuko wa chama zaidi ya fedha hizo kutoka ndani ya halmashauri yetu,” alieleza mtoa habari wetu kutoka Igunga.
Katika Wilaya ya Nzega, Uyui na Iramba, msafara wa Kinana ulipatiwa mafuta ya magari na chakula kwa fedha zilizotoka katika halmashauri na kukabidhiwa viongozi wa CCM wa wilaya, huku suala la malazi likiachwa kuwa jukumu la waliokuwa katika msafara.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, wakurugenzi wa wilaya zilizofanyiwa uchunguzi walikanusha kugharamia ziara hizo, lakini wakikiri kutoa magari yaliyozunguka katika miradi iliyokuwa ikikaguliwa na Kinana.
Mkurugenzi wa Wilaya ya Igunga, Rusika Turuka, alipoulizwa juu ya halmashauri yake kugharamia ziara ya Kinana, alitaka apewe muda kwa maelezo kuwa yupo katika mkutano na hata alipopigiwa tena simu hakupokea.
Mkurugenzi wa Wilaya ya Nzega, Abraham Mndeme, alikiri ofisi yake kutoa magari yaliyowabeba watumishi wa serikali na madiwani wa CCM kuongozana na Kinana katika ziara hiyo wilayani mwake.
Mndeme, alisema ugeni uliofika katika wilaya yake ni wa kitaifa, na kwamba miradi iliyohitaji kukaguliwa ni ile iliyosimamiwa na halmashauri ya wilaya.
“Walioambatana na msafara wa Kinana ni madiwani na sisi tulitoa magari ya kuwasafirisha kwenda kwenye miradi na kwa watendaji mimi nilitumia gari moja na mhandisi wa manispaa,” alisema Mndeme.
Mkurugenzi wa Wilaya ya Uyui, Hadija Mkauani, alipoulizwa juu ya kugharamia ziara ya Kinana, alimuomba mwandishi akutane nae ofisini na alipoambiwa simu inapigwa kutoka Dar es Salaam alikata simu.
“Baba naomba tuonane ofisini tuweze kuongea vizuri hayo mambo au umtume mwakilishi wako hapa mkoani si mnaye huku, tutaongea vizuri tu,” alisema Mkauani.
Kaimu Mkurugenzi wa Iramba, Mariam Mpita, alisema gharama za ziara hiyo zilibebwa na CCM huku yeye, watendaji wa halmashauri hiyo waliambatana na Kinana kukagua miradi ya maendeleo.
Nape afafanua
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, badala ya kujibu hoja ya ziara zao kutumia fedha za umma aliilaumu CHADEMA.
Alisema ziara zao zinawaumiza CHADEMA waliokuwa wakifanya ziara za aina hiyo ili kujiimarisha, lakini sasa wanaona zinafanywa na CCM wanahofia kuanguka mwaka 2015.
“Hata mtoto wa darasa la kwanza akisikia hayo madai atajua ni upuuzi, lakini ulizeni halmashauri iliyochangia hata shilingi moja. Najua ziara hizi zinawaumiza sana CHADEMA,” alisema.
Alipoulizwa kama ziara yao ina lengo la kuwaumiza CHADEMA au kuangalia changamoto zinazowakabili wananchi, na CCM itakavyoishauri serikali kutatua yatakayobainika, Nape alisema swali aliloulizwa ni fikra za kijinga za CHADEMA.
Nape alisema CHADEMA hawana ujanja wa kukwepa kifo chao, huku akisema uzushi na uongo hautawasaidia kupona.
Wakati Nape akikana halmashauri hizo kugharamia ziara za chama hicho, wiki iliyopita katika kikao cha Baraza la Madiwani wa Jiji la Arusha, Mkurugenzi wa jiji hilo, Juma Idd, alikiri kufanya hivyo.
Idd, alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu maswali ya madiwani wa jiji hilo waliohoji sababu za ziara za madiwani au viongozi wa CCM kutumia magari ya halmashauri.
Idd, alisema walitoa magari hayo ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya serikali iliyotaka viongozi wa CCM kupita kukagua utekelezaji wa ilani yao.
Alisema kuwa jiji walitoa wataalamu na gari kwa ajili ya kwenda kutoa ufafanuzi juu ya miradi hiyo.

walipo fichwa wasichana waliotekwa NIgeria yajulikana

sehemu-walipofichwa-wasichana-waliotekwa-nyarMkuu wa wafanyakazi nchini Nigeria, Alex Badeh alitoa taarifa

Mkuu wa wafanyakazi nchini Nigeria, Alex Badeh amesema kulingana na wanamgambo wa Boko Haram wameonyesha sehemu walipowaficha wasichana.
Katika taarifa aliyoitoa kwa waandamanaji waliojikusanya mjini Abuja, Badeh "tunajua walipo mabinti zenu ila hatutowaambia nyinyi. Hatuwezi kuwapatia siri za kijeshi. Tunafanya kazi, na tutawapatia mabinti wenu." Alisema. Ili kuweka maisha yao katika usalama, jeshi linapanga operesheni kabambe na ya ustadi ya uokoaji, alibainisha Badeh. "Hatutakiwi kumuambia mtu yeyote kwamba jeshi litafanya nini", alisema.
Kwa upande mwingine, Shirika la Utangazaji la Uingereza, BBC, limeeleza kuwa serikali ya Nigeria imefikia mazungumzo baina yake na Boko Haram. Kwa mujibu wa BBC, katika mazungumzo, ili kuwaacha wasichana huru, wametaka wanachama 100 wa Boko Haram waachiwe huru kutoka gerezani. Hata hivyo serikali ya Nigeria ilikataa mpango huo.

Monday 26 May 2014

Ulimboka mwakingwa amshangaa Julio kugombea umakamu Rais

Jamhuri Kihwelo ‘Julio’
 MIONGONI mwa wachezaji wenye heshima kubwa na wanaokubalika miongoni mwa wanachama wa Simba katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, yumo Ulimboka Mwakingwe.
Straika huyo wa zamani ambaye kwa sasa anaishi Morogoro na familia yake, ameibukia na kudai kushtushwa kwake na uamuzi wa kocha mahiri wa zamani wa Simba, Jamhuri Kihwelu ‘Julio’ kuwania Umakamu wa Rais wa klabu hiyo.
Mchezaji huyo amedai kwamba beki huyo wa heshima wa Simba, bado hajaiva kiasi cha kuwa kiongozi wa timu kubwa kama Simba.  Ulimboka alidai kushangazwa na uamuzi wa Julio wa kuwania nafasi hiyo bila kujipima kwani anaamini hana sifa stahili.
Ulimboka alisema: “Namuheshimu Julio kwa kuwa ni kocha wangu wa zamani na kaka yangu lakini uamuzi wake wa kuamua kugombea nafasi ya makamu wa rais ni kufurahisha nafsi yake ambayo kamwe ndoto yake haiwezi kutimia hata kidogo.”
“Nina mashaka na washauri wake ambao ndiyo waliomshawishi kuchukua fomu, najua hawezi kuambulia lolote katika uchaguzi huo. Tuache utani jamani kwenye mambo ya msingi, Julio anawezaje kuwa kiongozi wa Simba?
“Kila mtu anajua tabia ya Julio hasa sisi Simba, inawezekanaje baadaye aonekane kiongozi Simba? Nafikiri washauri wake hawakumshauri vizuri hadi akachukua fomu mbaya zaidi anagombea nafasi kubwa kama hiyo ya makamu wa rais.”
Julio ambaye anakubalika Simba kutokana na kunusuru benchi la ufundi kila makocha wanapotimuliwa, anawania nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu wa Simba utakaofanyika Juni 29, mwaka huu akichuana na Swed Mkwabi, Wilbard Mayage, Geofrey Nyange ‘Kaburu’, Joseph Itang’are ‘Mzee Kinesi’ na Bundala Benedict.
Alipotafutwa Julio alisema: “Kila mtu ana maoni na mtazamo wake, mimi natumia haki yangu kugombea.”

Mbeya city waanza vyema Michuano ya CECAFA wachapa 3 2 Academie Tchite

IMG_7961 WAGONGA Nyundo wa jijini Mbeya, Mbeya City fc jana walitoka  kushinda mabao 3-2 dhidi ya Academie Tchite ya Burundi katika mchezo wa kundi B wa michuano ya CECAFA Nile Basin Cup inayoendelea mjini Khartoum nchini Sudan.

Mbeya City fc waliofika Khartoum siku moja kabla ya mechi walianza kufungwa bao katika dakika ya 10 baada ya Rashid kumtungua kipa wao, lakini walirudi mchezoni baada ya Paul Nonga kusawazisha bao hilo dakika 5 baadaye. 


Dakika ya 27, nahodha wa Mbeya City fc, Mwegane Yeya kama ilivyo kawaida yake alifunga bao la pili kwa njia ya kichwa. Them Felix `Mnyama` alihitimisha karamu ya mabao dakika ya 37 baada ya kufunga bao safi na kuwapeleka Mbeya City mapumziko wakiwa na furaha.

Kipindi cha pili, Waburundi walikuja na Presha kubwa na katika dakika ya 68  Manirakiza alifunga bao la pili.

IMG_8009

Kocha wa Mbeya City fc, Juma Mwambusi aliwapongeza vijana wake kwa ushindi na kuahidi kufanya vizuri mchezo unafuata.

“Vijana walipunguza kasi kipindi cha pili, lakini nawasifu kwa kuvuna pointi tatu muhimu”. Alisema Mwambusi.

Mpinzani wake,  Ndayizeye Jimmy aliwapongeza  Mbeya City kwa soka safi.

Wafungaji wa mabao: Academie Tchite: (Rashid Patient-10’, Manirakiza 68’).

Mbeya City: (Nonga paul-15’, Mwagane Yeya 27’ and Themy Felix 37’).

Mchezo mwingine ulipigwa kuanzia majira ya saa 2:00 usiku na kushuhudia AFC Leopard ya Kenya ikiibuka na ushindi mabao 2-0 dhidi ya Etincelles.

Wamisri waanza kupiga kura kuchagua rais wao mpya

Aliyekuwa mkuu wa majeshi wa Misri, Abdel Fatah al-Sisi ambaye anapewa nafasi kubwa ya kushinda uchaguzi wa mwaka huu.
Aliyekuwa mkuu wa majeshi wa Misri, Abdel Fatah al-Sisi ambaye anapewa nafasi kubwa ya kushinda uchaguzi wa mwaka huu

Wananchi wa Misri, leo Jumatatu na kesho Jumanne wanapiga kura kuchagua rais mpya, kwenye uchaguzi ambao aliyekuwa mkuu wa majeshi wa nchi hiyo, Jenerali Abdel Fatah al-Sisi anatarajiwa kushinda.

Al-Sisi anapewa nafasi kubwa ya kushinda kwenye uchaguzi wa mwaka huu kutokana na kuwa na uungwaji mkono karibu nchi nzima kufuatia mapinduzi aliyoyaongoza ya kumuondoa madarakani Mohamed Morsi wa chama cha Muslim Brotherhood.

Abdel Fatah al-Sisi aliyekuwa mkuu wa majeshi wa Misri na anawania kiti cha urais

 
 Jenerali Sisi anatarajiwa kumsinda mpinzani wake wa karibu anayepewa nafasi ya kutoa upinzani kwa kiongozi huyo, Hamdeen Sabbahi ambaye kwenye uchaguzi uliopita alikuwa mshindi wa tatu.
Mamia ya wananchi wa Misri wameonekana wakiwa kwenye misururu mirefu ya watu wakisubiri kufunguliwa na kisha kuanza kupiga kura kwenye vituo mbalimbali vilivyoko nchi nzima.
Al-Sisi mwenyewe amepiga kura kwenye kituo cha Heliopolis ambako alikutana na mamia ya wafuasi wake wanaomuunga mkono na kuanza kumzonga wakati akipiga kura yake.
Mji wa Cairo kwa mara ya kwanza ukilinganisha na uchaguzi uliopita umeshuhudia maelfu ya wananchi wakijitokeza kwenye vituo vya kupigia kura mapema zaidi licha ya hofu ya kiusalama ambayo imekuwepo katika mji huo hivi karibuni.
Sisi mwenyewe wakati wa kampeni zake aliahidi kuwa iwapo ataingia madarakani atahakikishakuwa analeta mabadiliko makubwa ya kiuchumi kwenye taifa hilo ambalo katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita imekuwa vigumu kusimama kiuchumi.

Hamdeen Sabbahi kiongozi wa chama cha upinzani anayepewa nafasi ya kutoa upinzani kwa Jenerali, Al-Sisi
Kwaupande wake, Hamdeen Sabbahi ambaye amekuwa mshirika wa karibu wa Serikali ya Syria, amesema kuwa atahakikisha kunakuwa na usawa nchini humo pamoja na kumaliza utawala wa kijeshi ambao yeye mwenyewe aliunga mkono wakati rais Morsi akiondolewa madarakani.
Kwenye uchaguzi wa mwaka huu kilichokuwa chama kikuu cha upinzani chenye nguvu cha Muslim Brotherhood kimepigwa marufuku kushiriki kwenye uchaguzi wa mwaka huu baada ya kudaiwa kuhusika na makundi ya kigaidi nchini humo.
Uchaguzi huu unatarajiwa kumaliza miaka mitatu ya mzozo wa kisiasa nchini humo toka rais Morsi alipoangushwa madarakani ambapo kumekuwa na hali ya sintofahamu kuhusu suala la demokrasia nchini humo.

Aliyekuwa mkuu wa majeshi wa Misri, al-Sisi akisalimiana na rais wa Urusi Vladmir Putin alipofanya ziara nchini humo
Wananchi wa taifa hili wanashiriki uchaguzi huu huku kukiwa na kumbukumbu ya kuuawa kwa wafuasi zaidi ya 1400 wa aliyekuwa rais wa taifa hilo Mohamed Morsi ambaye anakabiliwa na kesi ya uhaini na kuchochea machafuko nchini humo.
Hata hivyo mashirika ya kutetea haki za binadamu nchini humo yanasema kuwa licha ya mapinduzi yaliyofanyika bado nchi hiyo itasimama kidemokrasia na kwamba hivi sasa maisha ni mazuri zaidi ukilinganisha na hali ilivyokuwa wakati wa utawala wa Hosni Mubarack.

Lisu aanika wabunge walioomba Rushwa

 Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu



Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amewataja kwa majina mawaziri na wabunge aliosema bungeni kuwa wamekuwa ombaomba katika mifuko ya hifadhi ya jamii.
Baadhi ya waliotajwa ni pamoja na Mbunge wa Kongwa ambaye pia ni Naibu Spika, Job Ndugai; Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu wa Bunge), William Lukuvi; Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angela Kairuki na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Pindi Chana na wabunge Betty Machangu (Viti Maalumu), Livingstone Lusinde (Mtera), John Komba (Mbinga Magharibi), Eugen Mwaiposa (Ukonga) na Gudluck Ole Medeye (Arumeru Magharibi).
Hata hivyo, gazeti hili halijawataja majina mawaziri na wabunge wengine waliomo kwenye orodha hiyo ya Lissu kwa kuwa hawakupatikana jana kujibu tuhuma hizo.
Mbali na kuwataja kwa majina, Lissu pia ametoa vielelezo vinavyoonyesha jinsi walivyokuwa wakiidhinishiwa malipo kwa nyakati tofauti na Mfuko wa Pensheni kwa Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (LAPF), kwa sababu mbalimbali.
Lissu alimwambia mwandishi wetu jana kuwa licha ya kiwango cha fedha kutokuwa kikubwa, lakini kinaweza kusababisha mgongano wa kimasilahi kati ya wajibu wa wabunge kwa umma na masilahi yao binafsi.
“Hali hii inaweza kusababisha Bunge likashindwa kutimiza wajibu wake wa kikatiba wa kuisimamia Serikali na taasisi zake,” alisema Lissu huku akisisitiza azimio lake la kuwasilisha hoja binafsi kwa Spika wa Bunge ili iundwe tume kuchunguza suala hilo.
Mkurugenzi Mkuu wa LAPF, Eliud Sanga jana alikiri kuwa shirika hilo liliidhinisha malipo kwa mawaziri na wabunge hao kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo.
Hata hivyo, alisema shirika hilo halitoi fedha taslimu, bali hununua vitu ambavyo viliombwa na viongozi hao kwa ajili ya kusaidia wananchi na si kufanya biashara.
Sakata lenyewe
Akizungumzia jinsi mawaziri na wabunge hao walivyosaidiwa, Lissu alisema LAPF ilitoa Sh2.5 milioni kwa ajili ya mradi wa madarasa Jimbo la Kongwa linaloongozwa na Ndugai.
Alipoulizwa kuhusu madai hayo, Ndugai alisema hakuna tatizo lolote kwa mbunge kupewa msaada na mfuko wa kijamii.
“Huyo Lissu ana upungufu mkubwa. Hivi LAPF ikisaidia Sh2 milioni kwa ujenzi wa darasa unaogharimu Sh10 milioni ni tatizo hilo? Nchi hii inakwenda wapi jamani, siyo kila kitu wanachozungumza wapinzani ni hoja, kama LAPF wangekuwa wanatoa fedha lingekuwa tatizo lakini wanasaidia vifaa tu.”

Ndugai alisema hiyo ni mara ya kwanza Jimbo la Kongwa kupatiwa msaada na shirika hilo huku akihoji juu ya Lissu katika jambo hilo ambalo alisema ni la kawaida mno.
Pia Lissu alisema LAPF ilitoa Sh1.6 milioni kwa ajili ya kuisaidia Shule ya Isimani iliyopo katika jimbo la Waziri Lukuvi.
Alipoulizwa jana kuhusu madai hayo, Waziri Lukuvi alisema asingeweza kuzungumza lolote kwa sababu alikuwa akiuguza huko Iringa. Shirika hilo liliidhinisha Sh1.5milioni kwa ajili ya mradi wa maabara wa Jimbo la Arumeru Mashariki.
Lissu alisema Waziri Kairuki aliidhinishiwa fedha kwa ajili ya ununuzi wa kompyuta mpakato (Laptop) mbili kwa ajili ya vyama vya wafanyakazi. Akizungumzia tuhuma hizo Kairuki alisema: “Sina la kusema katika hilo pengine ungewauliza LAPF watakuwa na ufafanuzi zaidi kuhusu fedha wanazozitoa kwa ajili ya kusaidia masuala mbalimbali.”
Lissu pia alisema LAPF iliidhinisha Sh2.5milioni kwa Waziri Chana ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu kwa ajili ya taasisi ya Iringa Constituency Development Account.
Kuhusu madai hayo Chana alisema: “Mifuko ya kijamii ina idara za kusaidia jamii. Mtu yeyote anaweza kuomba msaada katika mifuko hii na akasaidiwa.”
Alisema hakuna sheria zinazombana mbunge kuomba msaada kwa ajili ya kusaidia wananchi wa jimbo lake na kusisitiza kuwa hata Rais huwa anaomba msaada.
“Sijui huyo Lissu anasaidiaje wananchi wake jimboni. Kuna mifuko ya kusaidia watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi. Sijaelewa dhambi iko wapi katika hili. Benki ya NMB hivi karibuni ilitoa msaada wa mashuka Wilaya ya Ludewa, sioni tatizo,” alisema.
Kuhusu Mbunge wa Ukonga, Lissu alisema Aprili 5 mwaka jana, LAPF iliidhinisha malipo ya Sh500,000 kwa ajili ya taasisi ya Ukonga Constituency Development Trust Fund inayoongozwa na Mwaiposa.
“Hiyo Saccos ipo mpaka leo na kuomba siyo kosa. Sisi kama wabunge tuna dhamana ya kushirikiana na wananchi katika shughuli za maendeleo. Si dhambi kuomba fedha za ujenzi wa madarasa,” alisema Mwaiposa.
Lissu ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa Chadema alisema Februari 2013, uongozi wa LAPF uliidhinisha Sh2.8 milioni kwa Machangu kwa ajili ya taasisi inayoitwa Iyana Education Trust.
Hata hivyo, Machangu alipoulizwa kuhusu suala hilo alisema: “Ni muongo kabisa (Lissu) yeye inamhusu nini hiyo?”

Lissu alisema nyaraka alizonazo zinaonyesha kuwa Agosti, 2013 LAPF iliidhinisha fedha za kununulia pikipiki mbili kwa ajili ya vituo vya afya vya Jimbo la Mtera linaloongozwa na Lusinde.
Kama ilivyokuwa kwa Mwaiposa, Lusinde naye alisema kuomba si kosa na kwamba amekuwa akiomba misaada sehemu mbalimbali kwa ajili ya kulisaidia jimbo lake.
“Fedha hizo tumeshapata na pia tuliomba nyingine katika Kiwanda cha Saruji cha Wazo bado hatujapata,” alisema Lusinde na kusisitiza kuwa mbunge hawezi kuona mambo hayaendi katika jimbo lake kisha akakaa kimya.
Lissu pia alisema LAPF ililipa Sh1.5 milioni kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo kwa ajili ya Mfuko wa Nyasa Foundation uliopo katika eneo la jimbo linaloongozwa na Komba ambaye pia ni mlezi wa mfuko huo.
Komba alifafanua kuhusu fedha hizo na kusema: “Zilikuwa za Harambee na tuliomba sehemu nyingi lakini mimi siyo niliyeomba. Wao ndiyo waliomba na hata hundi walichukua wao.”
Lissu pia alisema LAPF iliidhinisha Sh1.5 milioni kwa ajili ya mradi wa maabara wa Jimbo la Arumeru Magharibi la Medeye madai ambayo mbunge huyo aliyewahi kuwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, alisema ili ayajibu anataka mwandishi awe pamoja na Lissu na wakae wote watatu kwa pamoja.

20 wafa kwa ajali ya tren India



Maafisa wa huduma za treni nchini India wanasema kuwa takriban watu 20 wanahofiwa kufariki katika ajali ya gari moshi katika jimbo la Uttar Pradesh.
Treni hiyo ya kubeba abiria iligongana na treni ya jizigo iliyokuwa imeemgeshwa katika kituo cha treni cha Chureb.
Mabehewa sita ya treni hiyo ya Gorakhdham Express yaling'oka kutoka kwenye treni hiyo.
Waokozi wanajaribu kuwaokoa abiria waliokuwa ndani ya treni hiyo na ambao bado wamekwama.
Treni hiyo ilikuwa inasafiri kutoka mjini Gorakhpur hadi katika jimbo la Hisar Haryana

Maiti yatumwa kwa njia ya posta China


Mwanamke huyo aliandika kwenye Facebook kuwa alikuwa anaenda kumtembelea rafiki yake kabla ya kuuawa
Polisi nchini Japan wanachunguza kisa cha kushangaza ambapo maiti ya mwanamke aliyeuawa ilitumwa kutoka Osaka hadi Tokyo kwa njia ya posta.
Inaaminika mwanamke huyo, Rika Okada, alidungwa kisu na mwili wake kuwekwa ndani ya sanduku ambayo ilitiwa kibandiko na karatasi iliyosema kuwa sanduku hiyo ilikuwa imemeba mwanasesere.
Sanduku hiyo, iligunduliwa ikiwa katika sehemu ya kuhifadhi vitu katika kituo cha posta.
Polisi wanasema kuwa sehemu ambako sanduku hiyo ilipatikana imewekwa, ilikuwa imekodishwa kwa kutumia kadi ya benki ya mwanamke huyo.
Polisi wanasema kuwa mwanamke huyo alitoweka tangu mwishoni mwa mwezi Machi, alipotuma ujumbe wa mwisho kwenye ukurasa wake wa Facebook kwamba alikuwa anaenda kukutana na rafiki yake wa muda mrefu ambaye alikuwa hajamuona kwa miaka mingi.

Sunday 25 May 2014

Shiboli niko tayari kucheza timu yoyote

 Ali Ahmed 'Shiboli'
MCHEZAJI mahiri wa soka aliyewahi kung’ara na timu ya taifa ya Zanzibar ‘Zanzibar Heroes,’ KMKM na Simba, Ali Ahmed ‘Shiboli’, amesema bado yupo katika kiwango bora cha kucheza Ligi Kuu.
Shiboli aliyetikisa msimu wa 2010/11 baada ya kugombewa na klabu za Simba na Yanga, amesema yu tayari kujiunga na timu ya Ligi Kuu baada ya kupumzika vya kutosha.
Alisema aliamua kupumzika kwa muda baada ya kushindwa kumalizana na KMKM iliyokuwa ikijiandaa na michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, mapema mwaka huu.
Akizungumza kwa simu kutoka jijini Tanga, Shiboli alisema bado ana uwezo wa kucheza Ligi Kuu Bara na kwamba anaaamini atapata timu ya kuicheza msimu ujao.
“Muda mrefu nilikuwa najifua pale Vingunguti, niliamua hivyo kutokana na kuwa na matatizo na viongozi wangu wa KMKM. Sitaki kuzungumzia hilo kwa sasa, naangalia maisha yangu ya baadaye,” alisema Shiboli.
Alisema kwa umri wake na mazoezi anayoyafanya, vinamruhusu kucheza ligi ya ushindani kama ilivyo ya Bara, hivyo yu tayari kusajili klabu yoyote kama watafikia muafaka kwa maana ya maslahi.
Jina la Shiboli lilivuma zaidi katika michuano ya Kombe la Chalenji mwaka 2010, baada ya kuwindwa vikali na timu kubwa za Simba na Yanga, wakati huo akichezea Zanzibar Heroes.
Wakati nyota huyo akiwaniwa na Yanga, Simba walimkatia denge na kufanikiwa kupata saini yake, jambo ambalo lilikuwa gumzo kubwa kwa wapenzi na mashabiki wa klabu hizo mbili.

CD ya Zakaria Hanspope yaigawanya Simba katika makundi

WAKATI sakata la kuzagaa kwa CD yenye mlengo wa kumpigia kampeni mgombea urais wa Klabu ya Simba, Evans Aveva, likizidi kushika kasi jijini Dar es Salaam, baadhi ya wapenzi na wanachama wa klabu hiyo wamemtaka mwenyekiti anayemaliza muda wake, Ismail Aden Rage, ajibu tuhuma dhidi yake zilizoelezwa katika CD hiyo.
CD hiyo inamnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zakaria Hanspope akizungumza na baadhi ya matawi ya Wilaya ya Kinondoni huku akitoa kauli za kashfa kuwachafua baadhi ya wagombea katika kinyang’anyiro cha uchaguzi huo utakaofanyika Juni 29.
Kwa mujibu wa CD hiyo, Hanspope anasikika akimnadi Aveva kwa vigezo mbalimbali ikiwamo kama mmoja wa vigogo wa Kundi la Friends of Simba, huku akimnanga mmoja wa wagombea urais, Michael Wambura na uongozi unaomaliza muda wake chini ya Rage ‘Tutu Vengere.’
Hanspope ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba, aliyechaguliwa na Rage, ananukuliwa akidai kuwa muda wote waliokuwa madarakani, shughuli zote za usajili alikuwa akiachiwa yeye na kwamba vikao vyao havikuwa vya kimaendeleo zaidi ya Rage (Mwenyekiti), kuwa mtu wa ‘kubagain’.
CD hiyo ambayo inamnukuu Hanspope akizungumza na wanachama hao wa Kinondoni, pia imelalamikiwa na Wambura, akilia dhidi ya kitendo hicho cha mpinzani wake kuanza kupigiwa kampeni kabla ya wakati.
Mmoja wa wanachama wa Tawi la Simba Mtongani, Juma Zozo, ameonyesha kusikitishwa na kauli ya Hanspope kupitia CD hiyo, kwani naye ni miongoni mwa Kamati ya Utendaji inayomaliza muda wake, hivyo alikuwa wapi kuyasema kabla ya kuanza harakati za uchaguzi.
Aliongeza kuwa hivi sasa kuna baadhi ya wanachama wameweka pingamizi dhidi ya kamati nzima inayomaliza muda wake kwa kuvunja Katiba ya Simba, ikiwamo Hanspope kama angekuwa ni mmoja wa wagombea, hivyo anashangazwa na kauli hiyo inayolenga kuwahadaa Wanasimba, wakati naye alikuwa kundini.
Yassin Yussuf, amemtaka Rage aeleze ukweli kuhusiana na madai ya Pope kwamba uongozi wao ulikuwa wa ‘magumashi’ na yeye alikuwa ni mtu wa ‘kubagain’ badala ya kuangalia maendeleo ya klabu.
Alipotafutwa Rage ambaye pia ni Mbunge wa Tabora Mjini jana, simu ilikuwa ikiita bila kupokelewa.
Tayari Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Simba, Dk. Damas Ndumbaro, amenukuliwa akimtaka Wambura kama ana ushahidi wa hayo, aufikishe kwa kamati husika ili hatua ziweze kuchukua mkondo wake.
Kwa upande wa Hanspope, alikiri kuzungumza na matawi hayo na kuongeza kuw, haoni tatizo kwani yeye si mgombea, bali ni mwanachama na haoni kama anahusika na kipengele hicho cha kampeni.
Kamati ya Uchaguzi ya Simba, ilionya watu kuanza kampeni kabla ya muda ambao umewekwa, na kwamba watakaobainika kanuni zitachukua mkondo wake.

Hakimu Kortin kwa kupokea rushwa

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wilayani Bunda, Mara imemfikisha mahakamani Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Kibara A, Witness Lameck (38) kwa tuhuma ya kuomba na kupokea rushwa kutoka kwa wavuvi.
Ofisa mtendaji huyo ameunganishwa kwenye kesi hiyo inayomkabili pia Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Kewnkombyo, Emmanuel Mng’wale (37), aliyefikishwa mahakamani hapo Mei 19 mwaka huu, kwa tuhuma hiyo.
Akiwasomea mashitaka yao mbele ya Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Bunda, Hamad Kasonso, Mwanasheria wa Takukuru, Eric Kiwia alisema washitakiwa wote walitenda kosa hilo kati ya Aprili 22 na 23 mwaka huu.
Kiwia alidai hakimu huyo aliandika hati bandia na kugonga mhuri wa mahakama na sahihi yake na kisha kumpatia ofisa mtendaji huyo, ili azipeleke kwa wavuvi kwamba wanashitakiwa kwa makosa ya uvuvi haramu.
Alidai kuwa hati hizo zililenga kuwabambikizia kesi wavuvi hao na kuwatisha ili watoe rushwa kati ya sh 60,000 hadi 150,000.
Ilidaiwa mahakamani hapo na wakili huyo kwamba ofisa mtendaji huyo alizisambaza hati hizo kwa wavuvi hao huku akiwaomba watoe kiasi hicho cha fedha, ili kesi zao zifutwe, vinginevyo wangehukumiwa kifungo ch miezi sita jela.
Kwa mujibu wa wakili huyo, baadhi ya wavuvi walitoa kiasi hicho cha fedha huku wengine wakitoa taarifa Takukuru, ambako uchunguzi ulibaini kuwa hati hizo ni bandia kwa vile watuhumiwa hawakuwa na kesi zinazowahusu.
Washitakiwa wote walikana mashitaka yao na kupewa dhamana hadi Juni 16 mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena mahakamani hapo.
Kwa mujibu wa Takukuru wilayani hapa, wavuvi waliotoa rushwa hiyo inasadikika ni wengi na kuongeza kuwa taasisi hiyo imeamua kushirikisha wavuvi watano kwa ajili ya ushahidi katika kesi hiyo.

Chadema yakana Kujitoa UKAWA

WENYEVITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoka mikoa ya Geita, Simiyu, Kagera na Mwanza, wamekanusha taarifa zilizotolewa juzi na vyombo vya habari zikipinga chama hicho kujiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Katika taarifa ya pamoja kwa waandishi wa habari mara baada ya kikao chao cha dharura kilichofanyika katika Hoteli ya Vizano jijini Mwanza, wenyeviti hao walisema hawamtambui mtu huyo aliyejiita Mwenyekiti wa Makatibu Mabaraza Kanda ya Ziwa Magharibi, Fikiri Migiyo.
Walisema kuwa kuonyesha kuwa mtu huyo sio kiongozi na wala hajui mfumo wa utendaji ndani ya CHADEMA, waraka huo umeonyesha kuwa Mkoa wa Simiyu uko katika Kanda ya Ziwa wakati sio kweli.
“Mkoa wa Simiyu umo katika Kanda ya Mashariki, tofauti na  alivyodanganya Migiyo, hivyo hatuko tayari kuacha watu aina ya Migiyo kuendelea kukichafua chama na viongozi wake,”  walisema wenyeviti hao katika taarifa yao.
Mwenyekiti wa Mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo, alisema kutokana na tukio hilo, wameanza kuendesha uchunguzi kumsaka mtu huyo.
Aliongeza kuwa wanafanya mawasiliano na wanasheria wa CHADEMA, kuona hatua watakazochukua dhidi ya vyombo vya habari   vilivyochapisha habari hizo bila kupata ufafanuzi kutoka kwa viongozi wa mikoa na taifa kama maadili ya kihabari yanavyosisitiza.
“Hakuna sehemu yoyote ambapo sisi wenyeviti wa CHADEMA kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa  tumeketi na tukapinga viongozi waandamizi wa kitaifa kujiunga  na UKAWA. Hilo sio tamko letu.
“Tumekagua kwenye kumbukumbu za chama   tukabaini hatuna mwanachama wala kiongozi katika ngazi yoyote  anayeitwa Fikiri Migiyo.
“Hivyo, hawa waandishi walishindwa nini kuwasiliana na uongozi wa juu, na walikuwa na uhakika gani kwamba waliyeongea naye huko Geita ni kiongozi ama msemaji kwa mujibu wa katiba yetu” alisema  Mawazo.
Walisema habari zilizoandikwa na magazeti hayo (sio Tanzania Daima) Mei 22, 2014  zikiwa na kichwa cha habari ‘Mbowe, Slaa  wapewa siku 14 kujitoa UKAWA’ zililenga kuleta mpasuko ndani ya chama na kwa vyama vya upinzani.
Nalo Baraza la Vijana wa CHADEMA mkoani Geita, limeitaka jamii kupuuza habari hizo ilizoziita za kizushi kwa kuwa mkoa hauna katibu mwenye jina hilo.
Baraza hilo limedai kuwa huenda waraka huo umeandikwa na wanasiasa uchwara baada ya kuona nguvu kubwa ya UKAWA inayoungwa mkono na Watanzania wengi.

UKAWA yainyima CCM usingizi

Waziri  Sophia Simba na Naibu Waziri Janet MbeneUMOJA wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), ulioanzishwa wakati wa Bunge la Katiba, umekuwa mwiba kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndani na nje ya Bunge,

Tayari umoja huo unaoundwa na vyama vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi, umeshaweka wazi dhamira yake ya kusimamisha mgombea mmoja katika ngazi tofauti kwenye uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika mwakani.
Kauli hiyo inaonekana kuzidisha hofu kwa CCM, ambayo kwa miaka mingi imekuwa ikifurahia msambaratiko wa upinzani ili ipate nafasi ya kutawala.
Kuimarika kwa UKAWA, kumetishia chama hicho tawala ambacho kinadaiwa kupanga mikakati ya kuwadhoofisha, ikiwemo kuwatumia makada wanaotoka kwenye vyama vinavyounda umoja huo.
Mabadiliko yaliyofanywa na kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, Freeman Mbowe, katika baraza lake la mawaziri vivuli kwa kuwaingiza wajumbe kutoka NCCR-Mageuzi na CUF, yamezidisha hofu kwa CCM.
Awali baraza kivuli liliundwa na wabunge wa CHADEMA, lakini baada ya UKAWA kuanzishwa, viongozi wa vyama husika waliamua kuimarisha umoja wao.
Uimara wa UKAWA umeanza kutishia mijadala ya Bunge la  Bajeti linaloendelea Dodoma, ambako wabunge wake wamekuwa mwiba kwa mawaziri wanaowasilisha hotuba za bajeti zao.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa UKAWA wamekuwa na ushirikiano mkubwa kuanzia wakati wa kuandaa hotuba za bajeti zao kivuli wakati wa mijadala na hata kuuliza maswali.
Kama sio wingi wa wabunge wa CCM kupitisha hoja zao kishabiki, baadhi ya bajeti za wizara zilizokwishasomwa na kupitishwa, zingekwama.
Baadhi ya mawaziri waliowasilisha bajeti zao, wamekiri walipomaliza hotuba zao kwamba wamepata wakati mgumu kwa UKAWA kuliko wakati mwingine wowote.
Mmoja wa mawaziri hao, Sophia Simba ambaye ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, alisema nje ya ukumbi wa Bunge mara baada ya kupitishwa kwa bajeti yake kwamba hajawahi kupata wakati mgumu kama mwaka huu alivyopata kutoka kwa UKAWA.
“Bajeti yangu imepita, lakini wale wabunge wa UKAWA walinibana sana, waliniweka pabaya sana, nashukuru Mungu imepita,” alisema Waziri Simba wakati akipongezwa na baadhi ya mawaziri, wabunge na maofisa wa wizara yake.
Hata baadhi ya mawaziri ambao hawajawasilisha bajeti zao, hofu yao imekuwa kwa wabunge wa UKAWA ambao hutumia muda mwingi kusoma na kuibuka na hoja nzito ambazo mara nyingi zimekuwa mwiba.
Spika wa Bunge, Anne Makinda, ni miongoni mwa makada walioonekana kutishwa na mabadiliko ya baraza kivuli ambapo alisema jambo hilo limefanyika kwa kuchelewa.
Makinda, alimnanga Mbowe kuwa amefanya mabadiliko hayo kwa kuchelewa kwa kuwa alishawahi kumshauri aunde baraza lenye muungano wa wabunge wa upinzani, lakini alipuuza na kuteua wa CHADEMA pekee.
Spika huyo aliifananisha hatua hiyo ya Mbowe, sawa na kukumbuka kujifunika shuka wakati kumeshakucha.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa walibainisha kauli hiyo ilionyesha kiongozi huyo ameanza kujawa na hofu juu ya mustakbali wa chama chake.
Makinda pia amekuwa akiwakataza wabunge kutoka umoja huo kujitambulisha wanatoka UKAWA bali wajitambulishe kutoka kambi rasmi ya upinzani.
Kiongozi huyo amekuwa akiwaambia wabunge wa UKAWA kuwa umoja wao uishie kwenye Bunge Maalumu la Katiba na wasiuingize kwenye Bunge la Bajeti.
Hofu kwa CCM
UKAWA wamekuwa gumzo kiasi cha kuwafanya vigogo wa CCM, wanaofanya ziara zao mikoani kutumia muda mrefu kuwazungumzia huku wakiulaani umoja huo.
Katika ziara hizo zinazoongozwa na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, UKAWA wameteka mijadala ya wanachama, viongozi na mashabiki wanaohudhuria mikutano ya chama tawala.
Katika mikutano hiyo, Nape amekuwa akipinga kufanywa kwa mazungumzo yenye lengo la kuwashawishi wajumbe wa umoja huo warejee kwenye Bunge la Katiba walilosusia vikao vyake mwezi uliopita.
Wataka viongozi kuelekea uchaguzi mkuu mwakani
Viongozi wa vyama vinavyounda umoja huo, wako kwenye ziara mikoani wakifanya mikutano ya hadhara kuelimisha umma namna mchakato wa katiba mpya unavyohujumiwa na CCM.
Viongozi wa UKAWA wamegawanyika katika makundi, moja likishambulia kwa mikutano ya hadhara katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini likiongozwa na Mwenyekiti wa CUF taifa, Profesa Ibrahim Lipumba.
Kundi jingine liko mikoa ya Kanda ya Kaskazini wakitoa elimu kuhusu mchakato wa katiba.
Katika mikutano yao ya hadhara, UKAWA walipata maelfu ya watu na kuna wakati polisi wamekuwa wakitumika kuidhibiti.
Duru za siasa zinasema kuwa hofu ya CCM kwa sasa ni kama ushirikiano huo utaendelea hadi 2015 ambapo UKAWA wamepanga kusimamisha mgombea mmoja kuanzia ngazi ya urais, ubunge na udiwani, kwamba chama hicho tawala kitakuwa na wakati mgumu.
Ni kutokana na kasi hiyo, CCM imepanga kupitia kwenye maeneo yote ambayo UKAWA wamepita, kujibu mapigo.