Saturday 24 May 2014

Mwibara Lugola (CCM) ahatarisha ubunge wake

MBUNGE wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), ameuweka rehani ubunge wake kwa kutishia kujiuzulu endapo Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Titus Kamani ataonyesha fedha alizotenga kwa ajili ya ruzuku ya wavuvi.
MBUNGE wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM)
Sambamba na hilo, Lugola alisema kuwa ataandika hundi ya sh milioni 50 endapo waziri huyo ataonyesha mahala alipotenga fedha hizo kwa ruzuku kwa wavuvi.
Lugola alitoa kauli hiyo jana wakati akichangia mjadala wa hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
Huku akionyesha msisitizo, Lugola alisema amefikia hatua ya kuuweka rehani ubunge wake baada ya waziri katika hotuba yake kudai serikali ina mpango wa kutoa ruzuku kwa wavuvi.
“Nimesikia hotuba ya Waziri wa Uvuvi na Mifugo na mpango wake wa kutaka kutoa ruzuku kwa wavuvi wadogo, nimeangalia vitabu vyote sioni mahala alipotenga fedha hizo kwenye bajeti yake kwa mwaka huu wa fedha.
“Waziri akinionyesha mahala zilipo fedha hizo alizotenga kwa ruzuku, naandika barua ya kujiuzulu leo hii jioni na nitaandika hundi ya sh milioni 50 kumpa waziri,” alisema Lugola.
Mbunge huyo alimlaumu Waziri Kamani na naibu wake kwamba walipokuwa wabunge walikuwa wakiilaumu sana wizara hiyo, lakini leo baada ya kuwa mawaziri wamegeuka kuwa wababaishaji.
Alisema wavuvi wadogo hawahitaji ruzuku, bali wanahitaji kuwezeshwa kwa kuwajengea mazingira mazuri ya uvuvi kwani wana changamoto nyingi zikiwemo za kuibiwa nyavu na vifaa vyao vya uvuvi.
Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba (CCM), alisema tatizo linaloikabili serikali katika kuendeleza sekta ya uvuvi na mifugo ni mipango dhaifu.
Alisema Tanzania ina kila kitu kuendeleza sekta ya mifugo na uvuvi, lakini haina mipango ya kuzifanya sekta hizo zikue na kuleta tija katika kukuza uchumi wa taifa.
“Hebu tujiulize, tusingekuwa na ng’ombe, kuku, mbuzi, tungetumia kiasi gani kuagiza nyama kutoka nje?” alihoji Serukamba na kuongeza kuwa viongozi wasipobadili fikra, Watanzania wataendelea kulalamikiana.
Akitolea mfano wa nchi ya Ethiopia, Serukamba alisema wamefanikiwa sana katika sekta ya mifugo ambayo inaingiza pato kubwa la uchumi wa taifa hilo na kutaka Watanzania wajiulize Ethiopia wamewezaje.

No comments: