Sunday 25 May 2014

Chadema yakana Kujitoa UKAWA

WENYEVITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoka mikoa ya Geita, Simiyu, Kagera na Mwanza, wamekanusha taarifa zilizotolewa juzi na vyombo vya habari zikipinga chama hicho kujiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Katika taarifa ya pamoja kwa waandishi wa habari mara baada ya kikao chao cha dharura kilichofanyika katika Hoteli ya Vizano jijini Mwanza, wenyeviti hao walisema hawamtambui mtu huyo aliyejiita Mwenyekiti wa Makatibu Mabaraza Kanda ya Ziwa Magharibi, Fikiri Migiyo.
Walisema kuwa kuonyesha kuwa mtu huyo sio kiongozi na wala hajui mfumo wa utendaji ndani ya CHADEMA, waraka huo umeonyesha kuwa Mkoa wa Simiyu uko katika Kanda ya Ziwa wakati sio kweli.
“Mkoa wa Simiyu umo katika Kanda ya Mashariki, tofauti na  alivyodanganya Migiyo, hivyo hatuko tayari kuacha watu aina ya Migiyo kuendelea kukichafua chama na viongozi wake,”  walisema wenyeviti hao katika taarifa yao.
Mwenyekiti wa Mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo, alisema kutokana na tukio hilo, wameanza kuendesha uchunguzi kumsaka mtu huyo.
Aliongeza kuwa wanafanya mawasiliano na wanasheria wa CHADEMA, kuona hatua watakazochukua dhidi ya vyombo vya habari   vilivyochapisha habari hizo bila kupata ufafanuzi kutoka kwa viongozi wa mikoa na taifa kama maadili ya kihabari yanavyosisitiza.
“Hakuna sehemu yoyote ambapo sisi wenyeviti wa CHADEMA kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa  tumeketi na tukapinga viongozi waandamizi wa kitaifa kujiunga  na UKAWA. Hilo sio tamko letu.
“Tumekagua kwenye kumbukumbu za chama   tukabaini hatuna mwanachama wala kiongozi katika ngazi yoyote  anayeitwa Fikiri Migiyo.
“Hivyo, hawa waandishi walishindwa nini kuwasiliana na uongozi wa juu, na walikuwa na uhakika gani kwamba waliyeongea naye huko Geita ni kiongozi ama msemaji kwa mujibu wa katiba yetu” alisema  Mawazo.
Walisema habari zilizoandikwa na magazeti hayo (sio Tanzania Daima) Mei 22, 2014  zikiwa na kichwa cha habari ‘Mbowe, Slaa  wapewa siku 14 kujitoa UKAWA’ zililenga kuleta mpasuko ndani ya chama na kwa vyama vya upinzani.
Nalo Baraza la Vijana wa CHADEMA mkoani Geita, limeitaka jamii kupuuza habari hizo ilizoziita za kizushi kwa kuwa mkoa hauna katibu mwenye jina hilo.
Baraza hilo limedai kuwa huenda waraka huo umeandikwa na wanasiasa uchwara baada ya kuona nguvu kubwa ya UKAWA inayoungwa mkono na Watanzania wengi.

No comments: