Saturday 31 May 2014

Wanafunzi wa chuo kikuu cha STEMUCO waandamana

Wanafunzi Stemuco waandamanaWANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Stella Maris (STEMUCO) mkoani Mtwara, wameandamana juzi wakidai kutolipwa posho za malazi na chakula na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwa miezi mitatu mfululizo.
Maandamano hayo yalianzia chuoni hapo saa 9 alasiri na kuelekea kwa Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali mstaafu Joseph Simbakalia, lakini walipofika maeneo ya Bima yalizuiliwa na polisi na kutakiwa kueleza kilio chao.
Akizungumza kwa jazba, mmoja wa wanafunzi hao, alisema kwa miezi mitatu hawajalipwa fedha ya kujikimu, na hakuna tamko lolote ambalo wameambiwa wakati wana haki kama vyuo vingine.
“Hatujalipwa fedha za malazi na chakula kwa miezi mitatu sasa, ndiyo maana tumechukua hatua hii ya kuandamana, tunakwenda kwa Mkuu wa Mkoa tumuelezee matatizo yetu, kwani yeye ndio rais wa mkoa huu.
“Hakuna mwenye silaha wala hakuna anayetaka kuhatarisha amani hapa, tunaomba msaada wenu polisi, ili tumuone Mkuu wa Mkoa,” alisema mwanafunzi huyo.
Mwanafunzi mwingine alisema mbaya zaidi uongozi wa chuo umekaa kimya, hali inayochangia  baadhi ya wanafunzi kujiuza ili waweze kujikimu.
“Uongozi wa chuo umekaa kimya hadi leo na hawajaongea chochote, na inafikia kipindi hadi watoto wa kike wanajiuza na kama unabisha fanya uchunguzi, pita jioni maeneo ya baa utakuta watoto wa kike wako wengi hadi mahudhurio ya darasani yanakuwa si mazuri,” alisema.
Akizungumza na wanafunzi hao, Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Mtwara, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi,  Ralph Meela, alisema amezungumza na mkuu wa chuo na kuwashauri kukutana na uongozi  huo kukutana na viongozi  wa wanafunzi hao na kuongozana nao katika ofisi wanayotaka kwenda.
Baada ya kukubaliana na wanafunzi hao, aliongozana nao na baada ya kuwapeleka katika ofisi ya mkuu wa mkoa walipelekwa kwa Kamanda wa Polisi Mkoa.

No comments: