Sunday 25 May 2014

CD ya Zakaria Hanspope yaigawanya Simba katika makundi

WAKATI sakata la kuzagaa kwa CD yenye mlengo wa kumpigia kampeni mgombea urais wa Klabu ya Simba, Evans Aveva, likizidi kushika kasi jijini Dar es Salaam, baadhi ya wapenzi na wanachama wa klabu hiyo wamemtaka mwenyekiti anayemaliza muda wake, Ismail Aden Rage, ajibu tuhuma dhidi yake zilizoelezwa katika CD hiyo.
CD hiyo inamnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zakaria Hanspope akizungumza na baadhi ya matawi ya Wilaya ya Kinondoni huku akitoa kauli za kashfa kuwachafua baadhi ya wagombea katika kinyang’anyiro cha uchaguzi huo utakaofanyika Juni 29.
Kwa mujibu wa CD hiyo, Hanspope anasikika akimnadi Aveva kwa vigezo mbalimbali ikiwamo kama mmoja wa vigogo wa Kundi la Friends of Simba, huku akimnanga mmoja wa wagombea urais, Michael Wambura na uongozi unaomaliza muda wake chini ya Rage ‘Tutu Vengere.’
Hanspope ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba, aliyechaguliwa na Rage, ananukuliwa akidai kuwa muda wote waliokuwa madarakani, shughuli zote za usajili alikuwa akiachiwa yeye na kwamba vikao vyao havikuwa vya kimaendeleo zaidi ya Rage (Mwenyekiti), kuwa mtu wa ‘kubagain’.
CD hiyo ambayo inamnukuu Hanspope akizungumza na wanachama hao wa Kinondoni, pia imelalamikiwa na Wambura, akilia dhidi ya kitendo hicho cha mpinzani wake kuanza kupigiwa kampeni kabla ya wakati.
Mmoja wa wanachama wa Tawi la Simba Mtongani, Juma Zozo, ameonyesha kusikitishwa na kauli ya Hanspope kupitia CD hiyo, kwani naye ni miongoni mwa Kamati ya Utendaji inayomaliza muda wake, hivyo alikuwa wapi kuyasema kabla ya kuanza harakati za uchaguzi.
Aliongeza kuwa hivi sasa kuna baadhi ya wanachama wameweka pingamizi dhidi ya kamati nzima inayomaliza muda wake kwa kuvunja Katiba ya Simba, ikiwamo Hanspope kama angekuwa ni mmoja wa wagombea, hivyo anashangazwa na kauli hiyo inayolenga kuwahadaa Wanasimba, wakati naye alikuwa kundini.
Yassin Yussuf, amemtaka Rage aeleze ukweli kuhusiana na madai ya Pope kwamba uongozi wao ulikuwa wa ‘magumashi’ na yeye alikuwa ni mtu wa ‘kubagain’ badala ya kuangalia maendeleo ya klabu.
Alipotafutwa Rage ambaye pia ni Mbunge wa Tabora Mjini jana, simu ilikuwa ikiita bila kupokelewa.
Tayari Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Simba, Dk. Damas Ndumbaro, amenukuliwa akimtaka Wambura kama ana ushahidi wa hayo, aufikishe kwa kamati husika ili hatua ziweze kuchukua mkondo wake.
Kwa upande wa Hanspope, alikiri kuzungumza na matawi hayo na kuongeza kuw, haoni tatizo kwani yeye si mgombea, bali ni mwanachama na haoni kama anahusika na kipengele hicho cha kampeni.
Kamati ya Uchaguzi ya Simba, ilionya watu kuanza kampeni kabla ya muda ambao umewekwa, na kwamba watakaobainika kanuni zitachukua mkondo wake.

No comments: