Saturday 31 May 2014

Ray C ahitaji mpenzi mzee

Ray C sasa ahitaji mpenzi mzeeMSANII wa muziki wa kizazi kipya, Rehema Chalamila ‘Ray C’, amesema kwa sasa hana mpango wa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mtu, na kama ikitokea basi atamtaka kuwa na miaka kuanzia 60.
Akizungumza katika kipindi cha ‘The Sporah Show’, Ray C alisema anahitaji wanaume wa umri mkubwa, kwa kuwa wanajua wanachokifanya, na kukiri kwamba vijana walichangia katika kurudisha nyuma maisha yake.
Msanii huyo ambaye kwa sasa ameanzisha asasi yake ya kupambana na dawa za kulevya, kutokana na yeye kuwa mmoja wa waathirika wa dawa hizo, alisema katika moja ya mambo anayoyajutia ni kuwa na mahusiano na vijana, jambo ambalo hataki kukumbuka walichomfanyia hadi kudhalilika mbele ya jamii.
Hata hivyo, alitumia fursa hiyo kuwaasa wazazi kutowatenga watoto wao ambao wamejidumbukiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya na badala yake, wawakumbatie na kuwaonyesha njia kama mama yake alivyofanya na kurudia hali yake ya kawaida.
Kuhusu kurudi kwenye muziki, Ray C alisema yupo mbioni na tayari ameshatengeneza nyimbo kadhaa, ambapo hivi sasa atakuwa akiimba miondoko tofauti tofauti, ikiwemo taarabu.
Katika kurudi kwenye muziki, jambo la kwanza alisema anatarajia kupunguza mwili wake kwa kufanya mazoezi, kwani hata daktari wake alishamwambia anatakiwa kupungua kutokana na umri wake kutoendana na kilo alizonazo.
Alipoulizwa mwanamuziki ambaye kwa sasa anamkubali Bongo, Ray C alisema wa kwanza ni AT akifuatiwa na Recho kutoka Jumba la Kukuza Vipaji (THT).

No comments: