Sunday 3 August 2014

Pirre Kwizera amaliza ubishi Msimbazi

UBISHI mkubwa uliokuwa umetawala kwenye usajili wa Simba ni kuhusiana na usajili wa vichwa vitatu, straika Elius Maguli wa Ruvu Shooting, Mrundi Pierre Kwizera wa Afad ya Ivory Coast na kiungo wa zamani wa Msimbazi, Shaaban Kisiga. Ubishi huo umekwisha jana Ijumaa kiulainii na vijana hao tayari wako Msimbazi.
Mrundi Pierre Kwizera wa Afad ya Ivory Coast.
Maguli alikuwa na mkataba wa mwaka mmoja na klabu yake ambayo kwa zaidi ya miezi miwili ilikuwa ikikomaa kwamba hauzwi lakini wamelegea baada ya kuonyeshwa fungu la maana na mabosi wa Simba, Kwizera alitua Dar es Salaam jana jioni na barua mkononi ikithibitisha kwamba yeye ni mchezaji huru na leo Jumamosi asubuhi atasaini mkataba wa miaka miwili na Simba. Lakini Kisiga ambaye ni fundi kwenye kiungo akitokea Mtibwa kama mchezaji huru amerejea Simba kwa rekodi ya kuwa mchezaji mzoefu aliyesajili kwa bei chee zaidi Sh 5 milioni tu na hakuna hata chenji iliyobaki.
Kama ubishi huo hautoshi Simba jana ilifunga hesabu ya wachezaji wa kigeni watakaovaa uzi mwekundu msimu ujao na kufuta kabisa uwezekano wa Emmanuel Okwi na Hamis Kiiza kutua Msimbazi kama mmoja wao akitemwa na Yanga kwani tayari Simba ina vichwa vitano.
Mbali na Kwizera, Simba  ina wachezaji wengine wa kigeni ambao ni Amissi Tambwe (Burundi),  Donald Mosoti (Kenya ), Joseph Owino (Uganda) na Paul Kiongera ambaye amewaahidi viongozi kwamba atamalizana na KCB ya Nairobi wikiendi hii na Jumatatu atatua Msimbazi kusaini mkataba ambao tayari wameshapatana bei kwani wiki iliyopita alikuwa Bongo ambapo alifikia Kijitonyama.
KWIZERA
Kwizera ambaye ni bingwa wa kupiga mipira mirefu na kufunga magoli kwa faulo baada ya kutua jana aliiambia ukombozi kuwa: “ Nimekuja kuwapa ubingwa Simba na kazi yangu kubwa ni kuhakikisha ushindi unapatikana na timu inafunga lakini pia hairuhusu goli kwenye lango letu.
“Mimi ni kiungo na ninapenda kucheza nafasi ya kiungo mkabaji zaidi kuliko ile ya kiungo mshambuliaji na zaidi napendelea kucheza mipira mirefu. Hivyo ninachoomba ni muda kidogo wa kuzowea mazingira lakini pia nataka kucheza Simba kwa mafanikio, niko tayari kwani hata nilivyokuja nimetoka kwenye ligi na naamini sitawaangusha Wanasimba.
“Ninachoomba ni michezo miwili ya kujiweka sawa na kumuonyesha kocha kile nilichonacho, tena nitaonyesha kile nilichojifunza nikiwa Ivory Coast na hii itanifanya niwe na nguvu na kuisaidia Simba. Namjua Tambwe kwani tuliwahi kucheza wote timu ya Taifa ya Burundi, anajua kufunga lakini pia ninafuraha kuwa tayari ninajua jinsi anavyocheza na tena nimeifuatilia Simba kwa zaidi ya misimu miwili na kuiona hivyo sina wasiwasi wa kucheza.
MAGULI NA KISIGA
MAKAMU wa Rais wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ aliwatambulisha wachezaji hao jana. Maguli ambaye alishika nafasi ya pili katika ufungaji bora msimu uliopita akiwa na mabao 14 na Tambwe alikuwa mfungaji bora kwa mabao 16.
Kaburu alisema Maguli amesaini mkataba wa miaka miwili na Kisiga mwaka mmoja.
“Tumekamilisha usajili wa Maguli ambaye kwa muda mrefu tulikuwa tunamhitaji, kamati pia imefanikiwa kumalizana na klabu yake ya Ruvu ambao walikuwa na mkataba naye, watu wanaweza kuona mambo yanaenda taratibu, hayo yote yanatokana na ukweli kwamba tunataka kufanya usajili kwa umakini mkubwa,” alisema Kaburu ambaye ni mzoefu wa mambo ndani ya Simba.
MKUTANO NA SIMBA DAY
Akizungumzia kuhusu Mkutano  Mkuu wa Simba, Kaburu alisema utafanyika kesho Jumapili kama ulivyotangazwa na Rais wake Evans Aveva ambao utafanyika katika Bwalo la Maofisa wa Polisi lililopo Oysterbay jijini Dar es Salaam.
Kaburu alisema Zesco United ya Zambia itacheza nao katika siku ya Simba Jumamosi ijayo kwenye Uwanja wa Taifa.
LOGA ANENA
KOCHA wa Simba, Zdravko Logarusic akishakabidhiwa Paul Kiongera, Saady Kipanga na Elius Maguli atalazimika kubadili mfumo na kuchezesha washambuaji wengi zaidi. Logarusic alisema Kiongera, Maguli na Kipanga si washambuliaji kamili hivyo anaweza kuwachezesha nyuma ya mshambuliaji wake mahiri Mrundi Amissi Tambwe kwa kutumia mfumo wa 4-2-3-1.

No comments: