Saturday 2 August 2014

Maximo ampa majukumu mazito Shadrack Nsajigwa


Kocha mpya wa timu ya vijana ya Yanga, Shadrack Nsajigwa (katikati) akiwaelekeza wachezaji wake pamoja na wachezaji wa timu ya wakubwa, walipokuwa wakifanya mazoezi ya pamoja kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola, Dar es Salaam jana.

Katika hali inayoonekana kuwa na hofu ya  kuchafua rekodi yake mapema Kocha mkuu wa Yanga, Marcio Maximo ameikacha  michuano ya Kagame kwa kumpa jukumu kocha wa timu ya vijana, Shadrack Nsajigwa ‘Fuso’  kuhakikisha anarudi na ubingwa wa Kombe la Kagame.
Maximo ambaye ameinoa Yanga tangu mwezi uliopita aliliambia gazeti hili kuwa ameshagawa timu mbili kwa malengo tofauti, moja iliyo na vijana wengi na baadhi wazoefu itakwenda Kagame na nyingine atabaki nayo yeye kambini Pemba kujiandaa na ligi.
“Nimeshateua timu itakayokwenda Rwanda na itakuwa chini ya kocha Nsajigwa na Leonardo Neiva  wakati nyingine nitabaki nayo mimi na Salvatory ambayo tutakwenda Pemba,  lengo ni kuhakikisha naiandaa timu kikamilifu kwa ajili ya Ligi Kuu.”
Maximo ameamua kuipeleka timu ya vijana kwenye michuano hiyo mikubwa Afrika Mashariki na Kati  itakayoanza Agosti 8,  huku akiongeza wachezaji  sita kutoka timu ya wakubwa.
“Nitaongeza mchezaji mmoja au wawili kati ya  wale walioko Taifa Stars ambaye naye atakwenda kwenye michuano ya Kagame kuongeza nguvu  ingawa siwezi kumtaja ni mchezaji gani kwa sasa,” alisema Maximo.
Katika mazoezi ya wiki hii Maximo alionekana kuiandaa kikamilifu timu itakayoshiriki michuano ya Kagame huku akiamini kuwa itafanya vizuri na kurudi na ubingwa.
Kwa mujibu wa mazoezi hayo wachezaji wa timu kubwa watakaoongozana na timu ya vijana ni Nizar Khalfan, Omega  Seme, Hussein Javu, Rajab Zahir, Said  Bahanuzi na kipa Ali  Mustapha ‘Barthez.’
Yanga imepangwa kundi moja na  Rayon Sports ya Rwanda, Atlabara na KMKM ya Zanzibar.

No comments: