Sunday 28 May 2017

TAARIFA KWA UMMA KUHUSU KUKANUSHA TANGAZO LA NAFASI ZA KAZI LILILOSAMBAA MITANDAONI.

Katika siku za hivi karibuni kumekuwepo na Tangazo la nafasi za kazi linalosambaa katika baadhi ya mitandao ya kijamii ikiwemo ''Facebook na WhatsApp'' likionyesha kwamba Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma imetoa tangazo la kazi lenye jumla ya nafasi wazi 188 kwa niaba ya waajiri mbalimbali Serikalini.

Watu hao mwenye nia ovu kwa makusudi wameamua kusambaza taarifa za uongo zenye kichwa cha Habari Tangazo la Nafasi za Kazi likiwataka watanzania wenye sifa na uwezo kutuma maombi ya kazi kwenye portal ya ajira kwa ajili ya kujaza nafasi hizo huku wakijua kuwa tangazo hilo sio la kweli kwa kuwa Serikali haijatangaza nafasi hizo hali ambayo imeleta usumbufu kwa jamii na wadau mbalimbali.

Katibu wa Sekretarieti ya Ajira anapenda kuujulisha umma kuwa mtu aliyeanzisha uzushi huo ametumia tangazo la kazi ambalo lilikwishatolewa mwaka jana tarehe 10 Mei, 2016 kwenye tovuti ya Sekretarieti ya Ajira lenye kumb Na. Kumb. Na EA.7/96/01/I/39   ambalo lilikuwa na nafasi wazi za kazi 188 na kulisambaza upya katika mitandao ya kijamii kwa lengo la kuupotosha umma.
Katika tangazo hilo lililokwisha tolewa mwaka jana, nafasi zilizotangazwa ni pamoja na Afisa ufugaji Nyuki daraja la II  nafasi 5, Dereva daraja la II nafasi 31, Mpishi daraja la II nafasi -7, Mlinzi- nafasi -15, Afisa  misitu daraja la II –nafasi-4, Mhifadhi wanyamapori daraja la II –nafasi- 5, Mfugaji Nyuki msaidizi daraji la II –nafasi– 5, Dobi daraja la II– nafasi 1, Mtunza bustani daraja la II - nafasi 3, Afisa wa Sheria daraja la II –nafasi 3,  Msaidizi wa hesabu - nafasi 10, Mwenyekiti wa mabaraza ya ardhi na nyumba ya wilaya -nafasi 1, Fundi sanifu msaidizi (maji) -nafasi 2, Fundi sanifu daraja la II umeme-  nafasi 4, Mchapa hati daraja la II– nafasi 1, Katibu mahsusi daraja la II- nafasi 30, Fundi sanifu mifugo daraja la II – nafasi 5, Msaidizi ustawi wa jamii II– nafasi 2, Mthamini daraja la II–nafasi 7, Fundi sanifu upimaji daraja II-nafasi 3, Mkufunzi msaidizi daraja la II nafasi 4, Mpokezi – nafasi 1, Mhandisi II ufundi– nafasi 20, Fundi sanifu daraja la II  mitambo – nafasi 4 na  Afisa elimu daraja la II –nafasi 1. Hata hivyo nafasi hizi zote mchakato wake ulisitishwa mwezi juni mwaka 2016 kwa ajili ya kupisha zoezi la uhakiki wa watumishi na vyeti feki hadi zitakapotangazwa tena.
Kwa taarifa hii tunapenda kuwataarifu wadau na wananchi wote kwa ujumla kuwa tangazo hilo halina ukweli wowote na linalenga kuupotosha Umma, hivyo wananchi wote wanapaswa kulipuuza. Aidha ifahamike kuwa matangazo ya nafasi wazi za kazi ambayo hutolewa na Serikali kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ni lazima yaonekane kwenye Tovuti ya Sekretarieti ya Ajira www.ajira.go.tz au portal ya Ajira ambayo ni portal.ajira.go.tz pamoja na vyombo vingine vya habari. Matangazo ya fursa za ajira Serikalini yamekuwa yakiendelea kutolewa kupitia tovuti ya Sekretarieti ya Ajira kadri vibali vya ajira vinapopatikana kutoka kwa waajiri mbalimbali.
Tunaendelea kuwasisitiza wadau wetu wote kuwa, wanapoona matangazo ya kazi yanayodaiwa kutolewa na Sekretarieti ya Ajira katika baadhi ya mitandao ya kijamii wasiyokuwa na uhakika nayo wajiridhishe kwa kuangalia katika tovuti na portal ya Sekretarieti ya Ajira kabla ya kuyafanyia kazi.
Sekretarieti ya Ajira inapenda kutoa taarifa kuwa haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote wenye nia ya kuupotosha umma kupitia taarifa zinazosambazwa ambazo hazina ukweli wowote.
Imetolewa na;

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma 22 Mei, 2017.

No comments: