Wednesday, 11 December 2013

Bunge laanza kuchambua ripoti za Kamati

. Mkutano wa 14 wa Bunge, unaendelea mjini Dodoma leo. Inatarajiwa kwamba wabunge wataendelea kutema cheche dhidi ya utendaji usioridhisha wa baadhi ya mawaziri.
Kwa mujibu wa ratiba ya mkutano huo, leo wabunge watachangia ripoti tatu za kamati za kudumu za Bunge zinazosimamia fedha za umma zilizowasilishwa wiki iliyopita.
Ripoti zitakazoendelea kujadiliwa ni pamoja na ya Kamati ya Serikali za Mitaa (Laac), ambayo inaonekana kuwagusa wabunge wengi kutokana na kuibua ufisadi wa kutisha.
Wabunge pia wataendelea kuchangia ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali na Mashirika ya Umma inayoongozwa na Zitto Kabwe (PAC) na ile ya Bajeti inayoongozwa na Andrew Chenge.
Baada ya kukamilika kwa mijadala hiyo, Serikali inatarajiwa kujibu hoja mbalimbali za wabunge ambao wameonyesha kutoridhishwa na utendaji wa baadhi ya mawaziri.
Kuendelea kuwapo kwa vitendo vya wizi, ubadhirifu na ufisadi kwa baadhi ya wizara kunaonekana kuwachefua wabunge hata baadhi yao kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuwawajibisha.
Baadhi ya wabunge waliochangia Ijumaa na Jumamosi iliyopita walimtaka Rais Kikwete kumfukuza kazi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Wengine walimtaka amfukuze kazi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi, Hawa Ghasia, kwa kushindwa kukabiliana na ufisadi.
Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola ndiye aliyekuwa mwiba kwa Pinda akisema amekuwa mpole na hawajibiki ipasavyo. Alisema katika nchi nyingine, wakati Kamati za Bunge zinawasilisha taarifa zake ndipo jicho la wananchi na Serikali linakuwa bungeni lakini kwa Tanzania imekuwa ni tofauti.
Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila alisema taifa lina matatizo makubwa mawili ambayo ni ukusanyaji kodi na matumizi mabaya ya fedha.
“Tunaposema Serikali imechoka maana mbadilishe kikosi, mpaka dakika 90 ziishe? Wabunge wa CCM mtakubaliana nami kwamba hii ni dalili kwamba mmechoka mbadili kikosi,” alisema na kuongeza:
“Waziri Mkuu wetu tumeshamzoea kila suala tunalomwambia anakwambia tunaangalia, tunafuatilia, tuko mbioni yanazungumzika… tumechoka na haya.”
Alisema mawaziri mizigo walitajwa katika ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana wako wanne lakini Pinda ndiye namba moja.

Simba yafuta makosa ya Cannavaro, Yondani

KOSA la kumzuia straika Amisi Tambwe lililofanywa na mabeki wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Kelvin Yondani hadi akapiga pasi kwa mfungaji Betram Mombeki, sasa linafanyiwa kazi na kikosi cha Simba.
Mombeki alifunga bao hilo dakika ya 54 baada ya kupokea pasi murua ya Tambwe ambaye aliwazidi ujanja Yondani na Cannavaro ambao walijipanga vibaya kwa kumzuia Tambwe lakini straika huyo aliwazidi ujanja na kumpa pasi mfungaji.
Katika pambano hilo la Ligi Kuu Bara lililochezwa Oktoba 20, mwaka huu kaika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, Yanga ilikuwa ikiongoza kwa mabao 3-0 hadi mapumziko lakini Simba ilisawazisha mabao yote kipindi cha pili.
Kwa muda mrefu kwenye mazoezi ya Simba mwishoni mwa wiki iliyopita, Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic ameonekana akiwahimiza mabeki wake hasa wa kati kusimama katika nafasi sahihi wakati timu inaposhambuliwa.
Logarusic alionekana akitilia mkazo sehamu ya kusimama mabeki wake na mara kwa mara alikuwa akiwaelekeza kwa ukali baadhi ya mabeki waliokuwa wakirudia makosa ya kutokuwapo sehemu husika. Kocha huyo alienda mbali zaidi kwa kuwafundisha mabeki wake namna ya kusimama wanapokuwa wanakaba jambo lililokuwa likishangiliwa na mashabiki wachache wa Simba waliohudhuria mazoezi hayo.
Muda mfupi baada ya mazoezi hayo, Logarusic raia wa Croatia aliliambia Mwanaspoti; “Beki yeyote mzuri lazima awe anajua mahala sahihi pa kusimama na usimamaji wake unapaswa kuwa madhubuti ndiyo maana umeona nawasisitizia.”

Umoja wa Mataifa wapeleka ndege za Drone Congo.

Umoja wa Mataifa utaanza kurusha ndege zenye kamera zisizotumia rubani-Drones - kwenye anga ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo-DRC hapo Jumanne  ili kuwasaidia walinda amani kuwasaka waasi na kufuatilia mienendo yao.

Mkuu wa walinda amani katika Umoja wa Mataifa, Herve Ladsous yupo mjini Goma kushuhudia uzinduzi huo wa Drones. Alisema Jumatatu kwamba hali huko mashariki mwa Congo ni tofauti sana kutoka mwaka mmoja uliopita wakati kundi la waasi wa M23 walipoiteka miji kadhaa katika eneo hilo.

Mwezi uliopita kundi la M23 lilitangaza kuweka chini silaha zake baada ya jeshi la Congo kuteka ngome ya mwisho ya kundi hilo kwa msaada wa kikosi maalumu cha Umoja wa Mataifa.

Wanamgambo waanza kuondoka Tripoli

Wapiganaji wa jeshi la mgambo huko Libya wanaolaumiwa kwa ghasia mbaya mjini Tripoli tangu kuanguka kwa Moammar Ghadafi walianza kuondoka katika mji mkuu Jumatatu huku vikosi vya jeshi la Libya vikiingia kuhakikisha usalama mitaani.

Wanamgambo kutoka pwani ya mji wa Misrata walianza kuondoka kuelekea mashariki baada ya  kutokea ufyatuaji risasi kwa waandamanaji Ijumaa na kuchochea siku mbili za mapambano ambayo yaliuwa watu wasiopungua 46 na kuwajeruhi mamia wengine.

Pia Jumatatu naibu mkuu wa upelelezi nchini Libya, Mustafa Nuh aliachiwa huru na watekaji nyara wake siku moja baada ya kumkamata wakati akiondoka kwenye uwanja wa ndege wa Tripoli.

Haikufahamika ni nani alimteka Nuh ambaye familia yake inatokea Misrata.

Makamu wa marais na mawaziri waapishwa Sudan

Rais Omar al-Bashir amehudhuria sherehe za kuapishwa kwa makamu wa marais wawili walioteuliwa hivi karibuni pamoja na wasaidizi na mawaziri wapya, ambao wote wanatoka Chama tawala cha National Congress CNP. Mabadiliko ya baraza la mawaziri nchini Sudan yamekuja baada ya nchi hiyo kuendelea kukumbwa na hali ya kukosekana kwa utulivu wa kisiasa. Makundi ya waasi wa Sudan ambao mara kwa mara wanalalamikia hali ya kuwekwa kando na maendeleo yasiyo na uwiano katika maeneo nje ya Khartoum, wanaendelea na mapambano, huku hali ya kuzorota kwa uchumi mjini Khartoum na kupanda kwa bei za bidhaa zikisababisha malalamiko na vifo vya watu wengi katika mwezi Septemba mwaka huu.

Wanajeshi wa UN wapambana na waasi DRC


Kamanda huyo, Generali Carlos Alberto dos Santos Cruz, anasema kwamba wanajeshi wake wanajiandaa kupambana na waasi wa FDLR walio Katika mkoa wa Kivu Kaskazini.

Kamanda wa wanajeshi wa Umoja wa mataifa katika Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo, anasema kuwa wanajeshi wake wameanza kupambana na waasi wa Kihutu kutoka Rwanda pamoja na makundi mengine ya waasi Mashariki mwa nchi.
Kundi hilo, lilianzishwa na wapiganaji wa kihutu waliokimbilia Congo Mashariki kutoka Rwanda wakati wa mauaji ya kimbare mwaka 1994.
Mwezi jana wanajeshi wa UN kwa kutumia nguvu waliweza kuwashinda waasi wa M23 waliokuwawanaendesha harakati zao Mashariki mwa Congo.