Wednesday 11 December 2013

Bunge laanza kuchambua ripoti za Kamati

. Mkutano wa 14 wa Bunge, unaendelea mjini Dodoma leo. Inatarajiwa kwamba wabunge wataendelea kutema cheche dhidi ya utendaji usioridhisha wa baadhi ya mawaziri.
Kwa mujibu wa ratiba ya mkutano huo, leo wabunge watachangia ripoti tatu za kamati za kudumu za Bunge zinazosimamia fedha za umma zilizowasilishwa wiki iliyopita.
Ripoti zitakazoendelea kujadiliwa ni pamoja na ya Kamati ya Serikali za Mitaa (Laac), ambayo inaonekana kuwagusa wabunge wengi kutokana na kuibua ufisadi wa kutisha.
Wabunge pia wataendelea kuchangia ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali na Mashirika ya Umma inayoongozwa na Zitto Kabwe (PAC) na ile ya Bajeti inayoongozwa na Andrew Chenge.
Baada ya kukamilika kwa mijadala hiyo, Serikali inatarajiwa kujibu hoja mbalimbali za wabunge ambao wameonyesha kutoridhishwa na utendaji wa baadhi ya mawaziri.
Kuendelea kuwapo kwa vitendo vya wizi, ubadhirifu na ufisadi kwa baadhi ya wizara kunaonekana kuwachefua wabunge hata baadhi yao kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuwawajibisha.
Baadhi ya wabunge waliochangia Ijumaa na Jumamosi iliyopita walimtaka Rais Kikwete kumfukuza kazi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Wengine walimtaka amfukuze kazi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tamisemi, Hawa Ghasia, kwa kushindwa kukabiliana na ufisadi.
Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola ndiye aliyekuwa mwiba kwa Pinda akisema amekuwa mpole na hawajibiki ipasavyo. Alisema katika nchi nyingine, wakati Kamati za Bunge zinawasilisha taarifa zake ndipo jicho la wananchi na Serikali linakuwa bungeni lakini kwa Tanzania imekuwa ni tofauti.
Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila alisema taifa lina matatizo makubwa mawili ambayo ni ukusanyaji kodi na matumizi mabaya ya fedha.
“Tunaposema Serikali imechoka maana mbadilishe kikosi, mpaka dakika 90 ziishe? Wabunge wa CCM mtakubaliana nami kwamba hii ni dalili kwamba mmechoka mbadili kikosi,” alisema na kuongeza:
“Waziri Mkuu wetu tumeshamzoea kila suala tunalomwambia anakwambia tunaangalia, tunafuatilia, tuko mbioni yanazungumzika… tumechoka na haya.”
Alisema mawaziri mizigo walitajwa katika ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana wako wanne lakini Pinda ndiye namba moja.

No comments: