Saturday 7 December 2013

STARS YAIVUA UBINGWA UGANDA, YATINGA NUSU FAINALI CHALENJI


TIMU ya Kilimanjaro Stars imefanikiwa kusonga mbele hatua ya Nusu Fainali baada ya kuwatoa Mabingwa watetezi wa Kombe hilo Uganda kwa ushindi wa changamoto ya penalti 3-2 katika michuano ya kombe la Chalenji inayoendelea jijini Nairobi, nchini Kenya lakini shujaa akiwa kipa Ivo Mapunda .
Katika mchezo huo uliopigwa katika Uwanja wa Manispaa ya mji wa Mombasa nchini Kenya, Uganda ndio waliokuwa wa kwanza kupata bao la kuongoza likifungwa na Daniel Sserunkuma katika dakika ya 16 akimalizia krosi ya Khamis Kiiza, bao ambalo halikudumu sana kabla ya Mrisho Ngassa kuisawazishia Stars kwa shuti kali 18.

Baada ya bao hilo Stars walikuja juu na kufanikiwa kupata bao la pili likifungwa na Ngassa kwa mpira wa adhabu uliojaa wavuni katika dakika ya 39, matokeo ambayo yalidumu mpaka mwisho wa kipindi hicho cha kwanza.
Kipindi cha pili Stars inayofundishwa na kocha Kim Poulsen, raia wa Denmark, ilipata pigo katikati ya kipindi hicho baada ya kiungo wake Salum Abubakar 'Sure Boy' kutolewa kwa kadi nyekundu baada ya kucheza rafu, ambapo nafasi hiyo iliwapa nguvu Uganda kupata bao la kusawazisha kupitia Martin Mpuga matokeo ambayo yalibaki hivyo mpaka mwisho wa mchezo na kuzipeleka mpaka kwenye matuta.

Katika mikwaju ya penalti Ivo alikuwa shujaa baada ya kucheza penalti mbili za Waganda ya beki  Khalis Alucho na  ile ya mwisho iliyopigwa na Sserunkuma ambayo ndiyo iliyoivusha stars.
Ifuatayo ni orodha ya waliopiga penalti katika mchezo huo.
Stars                                              Uganda
Erasto Nyoni (kosa)                     Godfrey Walusimbi (kosa)
Mbwana Samatta (kosa)             Emanuel Okwi (pata)
 Amri Kiemba (pata)                    Khalis Alucho (kosa
Athuman Idd (pata)                     Hamis Kiiza (pata)
Kelvin Yondani (pata)                  Sserunkuma (kosa)

No comments: