Monday 10 March 2014

Maafisa wa serikali nchini Yemen wamesema kuwa zaidi ya wahamiaji arubaini wa Kiafrika wamezama baharini, baada ya mashua walimokuwa wakisafiria kuzama, katika pwani ya kusini mwa nchi hiyo. Manuwari ya jeshi la Yemen ambalo lilikuwa katika eneo hilo, imefanikiwa kuwaokoa wahamiaji wengine wapatao thelathini.
Wizara ya ulinzi nchini Yemen imesema kuwa mashua hiyo iliyokuwa ikisafirisha wahamiaji haramu, ilizama katika mkoa wa Kusini wa Shabwa, eneo ambako maelfu ya wahamiaji wa Kiafrika huwasili kila mwaka.
Manuwari ya kijeshi ikishika doria katika eneo la Guba
Kwa mujibu wa shirika la Kimataifa la Uhamiaji la IOM, wengi wa wakimbizi wanaojaribu kuvuka guba la Eden, wanatoka Somalia na Ethiopia.
Shirika hilo limesema kuwa wahamiaji hao hufanya safari ndefu na hatari ili kukwepa umasikini, unyanyazaji au vita katika mataifa yao.
Baada ya kuwasili Yemen, wengi wao hutarajia kupata kazi nchini Saudi Arabia na mataifa ya Guba, lakini mamia ya wahamiaji wa Kiafrika hufa kila mwaka wakijaribu kuvuka eneo hilo la Guba wakitafuta maisha bora katika mataifa ya ngambo.

No comments: