Friday 13 December 2013

Mjomba wa kiongozi wa Korea anyongwa

Shirika la habari la Korea Kaskazini, KCNA, limetangaza kuwa Jang Song-thaek, mtu mwenye nguvu kisiasa nchini humo na ambaye ni mjomba wa kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, amenyongwa.
Shirika hilo limesema Jang alituhumiwa kutumia vibaya madaraka, kupinga vitendo vya kiwana mapinduzi na kukengeuka kitabia.
Bwana Jang alihukumiwa na mahakama maalum ya kijeshi na kunyongwa papo hapo kama msaliti. Mapema wiki hii, picha za televisheni zilimwoonyesha Jang Song Thaek akiondolewa na walinzi wenye kuvalia sare kutoka katika mkutano wa Chama tawala cha Kikomunisti.
Wachambuzi wa mambo wanaona kunyongwa kwake kama jaribio la kiongozi wa nchi hiyo Kim Jong-un kujiimarisha kiutawala.
Ni tukio kubwa kutokea tangu Bwana Kim amrithi baba yake, Kim Jong-Il miaka miwili iliyopita.
Shirika la habari la Korea Kaskazini, limesema Jang alikiri makosa katika mahakama ya kijeshi Alhamisi, kutaka kuiangusha serikali, na alinyongwa mara moja.
Bwana Jang, ambaye anafikirika kumjenga mpwa wake, wakati wa kipindi cha mpito wa uongozi kutoka kwa Bwana Kim Jong-il kwenda kwa mtoto wake Kim Jong-un mwaka 2011, "alikuwa mbaya kuliko mbwa" limesema shirika hilo.
Alikiri kutumia vibaya nafasi zake za uwajibikaji ili kuunda kikundi cha upinzani dhidi ya serikali na kulinda maslahi yake ya kisiasa, imesema taarifa ya shirika hilo la KCNA.
Kim Jong-un kiongozi wa Korea Kaskazini
Nchini Marekani, Ikulu ya nchi hiyo, imesema haiwezi kuthibitisha ukweli wa taarifa hizo, "lakini halina sababu za kutilia mashaka taarifa hizo"
"Kama itathibitika kuwa kweli, huu ni mfano mwingine wa ukatili uliopita kiasi, unaoendeshwa na utawala wa Korea Kaskazini. Tunafuatilia kwa karibu zaidi taarifa hizo na kushauriana na nchi washirika na marafiki katika eneo hilo.," imesema taarifa ya Ikulu ya Marekani.
Picha ya Bwana Jang akiwa mahakamani, mikono yake ikiwa imefungwa, imetolewa Ijumaa.
Kabla ya kutoweka kwa neema yake, mara kwa mara alipigwa picha akiwa pembeni mwa kiongozi wa nchi hiyo Kim Jong-un
Rais wa Korea Kusini Park Geun-hye amesema Korea Kaskazini imekuwa ikiendesha "utawala wa hofu"
Bwana Jang Song-thaek aliyemuoa dada wa kiongozi wa zamani wa Korea Kaskazini Kim Jong-il ambaye ni baba wa kiongozi wa sasa Kim Jong-un alijiunga na chama cha Kikomunisti mwaka 1972 na kupanda ngazi za uongozi katika chama hicho na pia akipanda ngazi ya juu kijeshi chini ya kiongozi Kim Jong-un.

No comments: