Friday 27 February 2015

Mchezaji wa Simba aitwa TP Mazembe

KAMA dili ikifanyika kwa haraka kabla msimu haujamalizika, Simba inaweza kuandika rekodi nyingine ya kuuza mchezaji kwenye timu kubwa zenye hadhi Afrika tena kwa fedha nyingi.
Kiungo wa Simba aliyeko kwa mkopo kwenye klabu ya Stand United ya Shinyanga, Haruna Chanongo ameitwa kwa majaribio kwenye klabu tajiri ya TP Mazembe na ataondoka nchini wiki ijayo.
Iwapo Chanongo atafuzu na kusaini Mazembe kabla ya msimu huu kumalizika Simba itaula, lakini kama akisaini baada ya msimu kumalizika itakuwa imekula kwa Mnyama kwa vile mkataba wake na mchezaji huyo utakuwa umemalizika na atakuwa huru.
Kuondoka kwa mchezaji huyo huenda kukaipa ahueni Yanga kwa vile atakosa mechi baina ya timu yake ya sasa ya Stand United dhidi ya Jangwani kwenye Uwanja wa Taifa wiki ijayo.
Mazembe ndiyo klabu wanayochezea Watanzania; Mbwana Samata (aliyetokea pia Simba) na Thomas Ulimwengu.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mkurugenzi wa Ufundi wa Stand, Muhibu Kanu alisema kuwa wataweza kumkosa Chanongo kwa kuwa amepata nafasi ya kwenda kufanya majaribio kwenye klabu ya TP Mazembe.
“Kwa sasa kocha wetu anamwandaa kwa ajili ya kufanya majaribio, hivyo amemwandalia programu ya peke yake nia ni kutaka kuona kijana anafuzu kwa kuwa hii ni sifa ya Tanzania nzima kama akiweza kusajiliwa na TP Mazembe,” alisema Kanu.
Alisema pia itakuwa ni pengo kubwa kwao kwani wana mechi mbili kubwa ya Kagera Sugar na Yanga huku tayari tiketi ya ndege ikitarajiwa kutumwa kwa ajili ya safari hiyo.
Meneja wa Chanongo ambaye ni Jamal Kisongo amekiri kuwa mchezaji huyo ataondoka nchini wiki ijayo kuifuata Mazembe huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
“Chanongo ataondoka wiki ijayo na hilo viongozi wa Stand wanalielewa ijapokuwa wamesikitishwa mchezaji huyo kuondoka wakati anahitajika sana katika timu hiyo, lakini kwa ajili ya maendeleo yake lazima akajaribu bahati yake,” alisema.
Meneja huyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Kituo cha Kukuza Soka kwa vijana kinachojulikana kwa jina la ‘Jaki’ kilichopo Mbagala jijini Dar es Salaam, alimtaka Chanongo kutumia vema nafasi hiyo ingawa ataenda kukutana na changamoto ya viungo waliopo Mazembe.
“TP Mazembe wana viungo vya ushindani wa hali ya juu, lakini Chanongo akifanya vizuri ana nafasi kubwa,” alisema.

No comments: