Saturday 9 April 2016

Mrema amwomba Mh Magufuli akumbuke ahadi yake ya kumpatia kazi


Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP) taifa, Augustine Mrema amemuunga mkono Rais John Mgufuli kwa kasi yake ya kupambana na ufisadi na kumuomba ampe kazi ili amsaidie kutekeleza jukumu hilo.

Mrema alimuomba Rais Magufuli atambue uzoefu wake kwa kukumbuka jinsi alivyopambana na mafisadi wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri Mkuu.

Huku akieleza CV yake hiyo, Mrema alimkumbusha Rais kuhusu ahadi aliyompa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana, ya kumpa kazi katika Serikali ya Awamu ya Tano ikiwa atashinda na kuwa Rais.

Akizungumza na waandishi wa habari wa blog yet kijijini kwake Kiraracha mkoani Kilimanjaro, Mrema alisema kuwa anasikitishwa na ukimya wa Rais Magufuli kwa sababu aliamini kuwa angetekeleza ahadi hiyo ya kumpa kazi muda mfupi baada ya kutangaza Baraza la Mawaziri, jambo ambalo hadi sasa hajalifanya.

Alisema, alikutana na Rais Magufuli mwaka jana katika kampeni jimboni Vunjo kwenye eneo la Njia Panda lililopo ndani ya mji mdogo wa Himo na kuambatana naye kwenye mkutano wa hadhara, ambapo alimwombea kura kwa wafuasi wake na kuahidiwa ajira.

“Katika kampeni, Dk Magufuli alifika kwenye mkutano wangu nikamwombea kura kwa kuwaambia watu wangu wamchague kwa kuwa ni mchapakazi na mwadilifu. Aliahidi kunipatia kazi katika Serikali na sasa namkumbusha na kumuuliza mbona yupo kimya?” Mrema alieleza na kuhoji.
Alipoulizwa ni kazi gani inayomfaa katika Serikali ya Magufuli, alisema yeye alishawahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri Mkuu hivyo yuko tayari kufanya kazi yoyote itakayomfaa ila alitamani zaidi kupangwa sehemu nyeti ili amsaidie kutumbua majipu.

Mrema alimpongeza Rais Magufuli kwa jitihada binafsi za kutumbua majipu anazozifanya na alijigamba kuwa yeye ndio mwenye uzoefu wa kupambana na mafisadi kutokana na rekodi yake nzuri ya kipindi cha Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi.

Katika hatua nyingine, Mrema alikanusha taarifa ya kuhongwa fedha ili kufuta kesi ya kupinga matokeo aliyoifungua dhidi ya Mbunge wa jimbo hilo, James Mbatia.

Alisema, taarifa hizo ni za kupuuzwa kwa sababu zinalenga kumpaka matope kwa wananchi wake wa Vunjo.

Mrema alieleza kuwa walifikia maridhiano ya pamoja kuhusu kuondoa kesi hiyo mahakamani na kwamba, hilo lilifanywa kwa kuzingatia maslahi ya wananchi. 

Pamoja na hayo, alikiri kumlipa Mbatia Sh mil 40 ikiwa ni sehemu ya kupunguza gharama alizotumia katika kesi hiyo, ikiwemo malipo ya mawakili wake.

No comments: