Wednesday 17 December 2014

Nape akiri madudu ya CCM yawanufaisha UKAWA uchaguzi wa serikali za mitaa

Nape
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kilifanya makosa katika baadhi ya maeneo ambayo yamekigharimu na kusababisha wananchi kupiga kura za hasira kukiadhibu katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu matokeo ya uchaguzi huo ambao umeonyesha kuvinufaisha vyama vya upinzani kupitia umoja wao wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Nape alisisitiza kwamba makosa hayo ndiyo yaliyosababisha wapinzani kujinyakulia mitaa kadhaa kwa wepesi.
“Tumejifunza na tumekuwa tunajaribu kila wakati kubadili mfumo wetu wa kura za maoni lakini bado kumekuwa na matatizo. Kwa mfano, kuna Mtaa Mwenge Dar es Salaam, wanaCCM waliamua kumchagua mgombea wa upinzani baada ya jina la waliyempenda kutorudi,” alisema Nnauye na kuongeza:
“Tunajua kwamba kuna maeneo mengi ambayo wapinzani wameshinda. Ukiangalia CCM tulifanya makosa katika kumweka mgombea, hivyo kusababisha hasira ambazo kwa kweli zimewafurahisha wapinzani lakini sisi zimetugharimu,” alisema.
Alisema chama chake kitafanya tathmini ili kubaini kama sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow nalo ni miongoni mwa mambo yaliyochangia kupoteza baadhi ya mitaa.
Hata hivyo, Nape alisema wapinzani hawapaswi kuufurahia ushindi walioupata, bali iwe ni changamoto kwao katika kuhakikisha wanawatumikia wananchi waliowaamini

No comments: