Wednesday 17 December 2014

Mwanasheria Mkuu wa serikali ajiuzulu

Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Jaji Frederick Werema amejiuzulu nafasi yake hiyo kuanzia jana, Jumanne, kufuatia sakata la uchotaji wa fedha kutoka akaunti ya ESCROW ambapo zaidi ya dola milioni 120 zilihamishwa.
Mwanasheria mkuu, pamoja na baadhi ya wanasiasa na maafisa waandamizi wa serikali walituhumiwa kuhusika kwa namna moja au nyingine kufanikisha kufanyika kwa miamala haramu ya fedha za Akaunti ya Escrow ya Tegeta.
Leonard Mubali ameandaa taarifa ifuatayo:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Dar es Salaam, imesema Rais Jakaya Kikwete amekubali ombi hilo la kujiuzulu kwa Mwanasheria Mkuu huyo wa Serikali.
Katika barua yake kwa Rais Kikwete, Jaji Werema amesema ameomba kujiuzulu kwa sababu ushauri wake kuhusiana na suala ya Akaunti ya Tegeta Escrow haukueleweka na umechafua hali ya hewa. Rais Kikwete amemshukuru Jaji Werema kwa utumishi wake ulioongozwa na uaminifu na uadilifu.
kamati ya Bunge ya hesabu za Serikali ilipeleka pendekezo kumtaka Jaji Werema kuwajibika
Sakata la Akaunti ya Escrow liliibuliwa bungeni na mmoja wa wabunge wa bunge la Tanzania, David Kafulila na kusababisha mjadala mkali na kuamua Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kupewa jukumu la kuchunguza kashfa hiyo.
Baada ya uchunguzi kuwasilishwa katika mkutano wa bunge uliomalizika mwishoni mwa mwezi Novemba, kamati hiyo ilikuja na maazimio manane kuhusu taarifa ya ukaguzi maalum kuhusiana na miamala iliyofanyika katika akaunti ya Escrow ya Tegeta pamoja na umiliki wa kampuni ya IPTL.
Miongoni mwa maazimio ya bunge yaliwataja baadhi ya wanasiasa, mwanasheria mkuu, maafisa waandamizi wa serikali, majaji, wakuu wa taasisi za umma, viongozi wa dini, mawakili wa kujitegemea na watu binafsi kuhusika katika kashfa hii na hivyo kuagiza mamlaka zinazohusika kuwachukulia hatua za kisheria wahusika na wengine kuondolewa katika nyadhifa zao za kuteuliwa.
Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali, Zitto Kabwe
Kamati hiyo ya Bunge pia ilipendekeza kuwa waziri wa Nishati na Madini, waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, mwanasheria mkuu, katibu mkuu wa wizara ya Nishati na Madini na wajumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Tanesco wawajibishwe kwa kuishauri mamlaka ya uteuzi kutengua uteuzi wao.
Pia maazimio ya Kamati ya kudumu ya bunge ilipendekeza kuwa, kwa miaka mingi mikataba mibovu ya kuzalisha umeme kati ya Tanesco na makampuni binafsi imeisababishia Tanesco hasara ya mabilioni ya fedha na kutishia uhai wake wa kifedha, serikali iwasilishe mikataba husika bungeni au kwenye kamati zake kwa lengo la kutekeleza vema wajibu wake wa kuimamia na kuishauri serikali.
Akaunti ya Escrow ilianzishwa katika Benki Kuu ya Tanzania ili kuhifadhi fedha, baada ya kuibuka kwa mvutano kati ya Shirika la Umeme la Tanzania, Tanesco na kampuni ya kufua umeme ya IPTL kuhusu ongezeko la mtaji wa uwekezaji, huku TANESCO ikilalamika kuwa gharama za kununua umeme kutoka kampuni ya IPTL zilikuwa za juu mno. Fedha hizo zingeendelea kutunzwa katika Akaunti hayo hadi wakati ambapo suluhisho la mvutano wa wabia hao wawili lingepatikana

No comments: