Wednesday 31 December 2014

Kiongozi wa juu wa Al-shabab auwawa

Askari wa Somalia wakifanya ulinzi huko Mogadishu, Somalia.
Serikali ya Somalia, inasema mkuu wa ujasusi wa Al-Shabab aliuwawa katika shambulizi moja la anga la Marekani, karibu na mji wa Saakow.
Taarifa iliyotolewa na idara ya usalama wa taifa ya Somalia, na idara ya ulinzi  Jumanne, imesema Abdishakur Tahlil aliuwawa na watu wengine wawili katika shambulio la Jumatatu.
Taarifa hiyo inaendelea kusema kuwa, Tahlil alikuwa anasafiri kati ya Saakow na kijiji cha Jawari ambapo gari lake lilishambuliwa na kuharibika vibaya.
Kundi hilo lenye uhusiano na Al-Qaida, la Al-Shabab, linajaribu kuiondoa serikali ya Somalia, na kuifanya nchi hiyo kuwa nchi ya Kislam yenye msimamo mkali.
Msemaji wa Marekani alisema Jumatatu, kwamba maafisa hawaamini kama kulikuwa na raia yoyote katika shambulio hilo.
Mwezi September, shambulizi lingine la anga la Marekani liliua kiongozi wa Al-Shabab Ahmed Abdi Godane.
Majeshi ya Somalia, na Umoja wa Afrika, yamefanikiwa kuwashambulia na kuwarudisha nyuma wanamgambo wa Al-Shabab, katika miaka ya hivi karibuni.

No comments: