Monday 12 January 2015

Luis Suarez maisha yake yawekwa pabaya Barcelona

WAKATI mwingine maisha sio popote. Hali imeanza kuonekana kuwa ngumu kwa mshambuliaji wa Barcelona, Luis Suarez, katika maisha yake ya Catalunya kutokana na kufukuzwa kwa watu wawili muhimu kwake waliompeleka klabuni hapo.
Barcelona imewafukuza Mkurugenzi wa Ufundi, Andoni Zubizarreta pamoja na msaidizi wake, Carles Puyol na hatua hiyo imemweka Suarez katika presha kubwa.
Nyota huyo wa kimataifa wa Uruguay ameanza kutazamwa kwa jicho baya tangu alipohamishwa kwa dau la Pauni 75 milioni kutoka Liverpool Julai mwaka jana na bado hajakirejea kiwango chake cha upachikaji mabao.
Suarez ameifungia Barcelona mabao matatu tu katika mechi 12 na hatima yake imeanza kuangaliwa kwa karibu na klabu kubwa za Ligi Kuu England.
Mara kadhaa Barcelona imekuwa ikichukua maamuzi magumu ya kuwauza mastaa wake katika muda mfupi kama wakishindwa kuonyesha makali.
Barcelona haina mpango wa kumuuza Suarez, lakini anaweza kujikuta katika wakati mgumu katika kipindi cha majira ya joto pindi Barcelona itakapofanya uchaguzi wa kupata viongozi wapya.
Rais wa Barcelona, Josep Maria Bartomeu, juzi Jumatano wakati timu yake ikijiandaa na pambano la jana Alhamisi la Kombe la Mfalme, alitoboa kuwa ataitisha uchaguzi mkuu wa timu hiyo mapema kuliko ilivyo kawaida.
Hata hivyo, hata kama utawala mpya wa Barcelona hautaafiki uwezo wa Suarez, bado haionekani kama Barcelona itakubali kumpoteza Suarez kutokana na timu hiyo kufungiwa kusajili wachezaji, hatua iliyochukuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Soka (Fifa) baada ya kuchemsha katika uhamisho Neymar.
Mpaka sasa Suarez amefunga bao moja tu la Ligi Kuu Hispania katika ushindi wa 5-0 dhidi ya Cordoba kwenye mechi ya Desemba 20 mwaka jana, kabla ya kufunga mabao mawili katika mechi mbili za Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya timu za Apoel Nicosia na PSG.

No comments: