Monday 26 January 2015

Mbozi; Kaya 5000 kupewa msaada

Kaya 5,000 za wakulima na wafugaji katika Kata za Isansa na Igamba, wilayani Mbozi zitaingia kwenye mfumo maalumu wa uchumi utakaohusisha ufugaji ng’ombe wa maziwa kwa lengo kupambana na umaskini.
Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Heifer-Tanzania, Dk Henry Njakoi alisema hayo juzi wakati wa akizindua wa mradi wa kuboresha ustawi wa maisha ya wakulima na wafugaji mjini hapa.
Dk Njakoi alisema mradi huo unatekelezwa chini ya Heifer-Tanzania na kaya 2,000 kati ya 5,000 zitaingizwa moja kwa moja kwenye mpango wa thamani ya maziwa kupitia mfumo wa kitovu cha biashara ya maziwa.
“Mradi huu utawapatia wafugaji wapya ng’ombe wa maziwa 400 na kuwapa mafunzo kwa njia ya shamba darasa wakulima 1,600,” alisema Dk Njakoi na kuongeza:
“Tunataka wananchi wawe na vyanzo zaidi vya mapato ili kukabiliana na hali ngumu ya maisha.”
Alisema kupitia mradi huo, wananchi wa wilaya hiyo wataongeza kipato kwa njia ya kushiriki kazi za uzalishaji maziwa, kupata maji safi na nishati mbadala kwa mahitaji ya nyumbani.
Akizungumza kwa niaba ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Rosemary Senyamle alisema mpango wa sasa wa Serikali ni kutaka kuona wananchi wananufaika na ufugaji.
Alisema Serikali ina mpango wa kuhakikisha maziwa yanazalisha faida katika jamii.
“Niseme tu kwamba, mradi huu unaimarisha sawia juhudi za Serikali kujenga uchumi wa wananchi na kuifanya Tanzania ijitegemee katika kuzalisha na kusindika bidhaa za maziwa,” alisema Senyamle.

No comments: