Thursday 8 January 2015

Raia wa Kuwait wakamatwa na Kenge 149 Mwl Nyerere Airport

uwanja wa Mwalimu Nyerere
Jeshi la Polisi la   Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)linamshikilia raia wa Kuwait kwa tuhuma za kukutwa na viumbe hai aina ya Kenge 149 wenye thamani ya Sh 6.3 milioni.
Kamanda wa Polisi wa JNIA, Khamis Suleiman alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Hussain Ahmed Ally Mansour(34), raia wa Kuwait ambaye alikamatwa uwanjani hapo jana  majira ya saa 5 usiku wakati akijiandaa  na safari ya  kuelekea nchini Kuwait  kupitia Dubai  na Shirika la Ndege la Emirates  .
Kamanda  Selemani alisema Mansour alikamatwa na wanyama hao ambao aliwahifadhi  kwenye mifuko midogo midogo ilivyowekwa katika begi kubwa lenye rangi nyeusi.
“Kenge waliwekwa kwenye mifuko midogo midogo 15 na kila mmoja kuna kenge 15 na mifuko mingine walikaa wawili,”alisema kamanda Selemani.
Alisema kati ya Kenge hao, 15 walikufa na walio hai walikuwa 134 ambao  walikuwa wamefichwa kwenye mifuko hiyo.
Seleman alisema wakati wanafanyiwa upekuzi ndipo  walipogundua kuna vitu ambavyo vinafanana na nyoka  na kuamua  kuwashirikisha wataalamu wa maliasili ambao walibaini kuwa begi hilo lilikuwa na Kenge.
“Huyu mtuhumiwa alikuja nchini Januari 6,alitiliwa mashaka na polisi wa JNIA  na tulimuamuru akae pembeni kwa upekuzi zaidi  na kugundua anasafirisha kenge bila Kibali,”alisema Selemani.
Selemani alisema walipoendelea kumuhoji mtuhumiwa huyo alidai kuwa alikuja nchini kwa ajili ya kuchukua viumbe aina ya ndege lakini baada ya kuwakosa aliamua kubeba Kenge hao.
Kamanda Selemani aliwaomba wananchi kuwa na uzalendo wa nchi yao wanapoona mtu anasafirisha rasilimali za nchi watoe taarifa katika jeshi la polisi.
Alisema polisi  wataendelea kuimarisha  ulinzi katika maeneo ya mipakani na viwanja vya ndege ili kudhibiti aina hiyo ya utoroshaji wa nyara.
Julai 31, mwaka jana raia wa Vietnam, Dong Van (47)  naye alikamatwa  uwanjani hapo akiwa na meno 65 na kucha 447 za simba zenye thamani ya Sh189.4 milioni.

No comments: