Tuesday 18 February 2014

Mbeya City wabadili jezi zao

Dar es Salaam. Timu ya Mbeya City inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara imepanga kubadili jezi zao wanazozitumia zenye rangi ya zambarau na nyeupe ndani ya mwaka huu.

Mbeya City ambayo imepanda daraja msimu huu, imeonekana kuwa tishio kwa klabu kongwe nchini za Simba na Yanga kutokana na upinzani mkubwa wanaoutoa katika Ligi Kuu inayoendelea nchini.

Akizungumza na gazeti hili, Mwenyekiti wa timu hiyo, Mussa Mapunda alisema kuwa lengo kubwa ni kubadilisha jezi hizo ili ziwe na mwonekano tofauti kati ya wachezaji na mashabiki wanaoishangilia Mbeya City ndani ya Tanzania na mpakani mwa Malawi na Zambia. Alisema soko la jezi zao hivi sasa limeongezeka tofauti na mwanzoni wakati timu yao inapanda kutoka daraja la kwanza kwenda Ligi Kuu, hivyo wamepanga kuzindua rasmi jezi mpya za Mbeya City ndani ya mwaka huu kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Aliongeza kuwa, wamepanga kuleta kontena zima la jezi likiwa pamoja na bendera, kofia, skafu, soksi zenye rangi ya zambarau na nyeupe zinazoiwakilisha timu hiyo.

“Baada ya soko la jezi kuongeza kwa kasi kubwa ndani na nje ya nchi, hivi sasa tumeona ni bora tubadili muonekano wa jezi ya timu yetu, tunataka jezi za wachezaji na mashabiki zitofautiane kidogo.

“Mpango huo tumepanga kuuanza ndani ya mwaka huu, uzinduzi wake utafanyika kwenye Uwanja wa Sokoine, tayari tumeanza mazungumzo na mawakala wetu wanaotutengenezea jezi waishio nchini China,”alisema Mapunda.

No comments: