Friday 7 February 2014

Msigwa atiwa mbaroni

MBUNGE wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (48) (CHADEMA), amekamatwa na Jeshi la Polisi mkoani humo akidaiwa kumjeruhi vibaya mkazi wa Itamba mjini humo, Bw. Salum Kaita (33), ambaye ni mfanyabiashara.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Ramadhan Mungi, alisema Mchungaji Msigwa alikamatwa juzi akidaiwa kumpiga nondo kichwani Bw. Kaita ambaye amelazwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa.
Alisema siku ya tukio, kulitokea vurugu katika Kata ya Nduli kwenye kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani zinazoendelea baada ya mtu mmoja anayedaiwa kuwa mfuasi wa CCM akiwa na sare za chama hicho, kuvamia mkutano wa CHADEMA uliokuwa ukifanyika katika Kijiji cha Mgongo.
"Wakati mkutano unaendelea, mama mmoja anayedaiwa kuwa mfuasi wa CCM, alipita eneo hilo ndipo wafuasi wanaodaiwa kuwa wa CHADEMA, walimshambulia wakati mkutano unaendelea.
"Pia kuna gari la CCM na wafuasi wao ambalo lilipita eneo la mkutano huo, kukatokea kutokuelewana na kusababisha ghasia kati ya wafuasi wa pande mbili lakini polisi waliokuwepo eneo la tukio, waliweza kutuliza vurugu hizo," alisema.
Aliongeza kuwa, baada ya polisi kutuliza vurugu hizo, wafuasi wa CCM walikwenda eneo la Nduli ambapo wafuasi wa CHADEMA nao walikwenda eneo hilo wakiongozwa na Mchungaji Msigwa baada ya kupata taarifa kuwa, CCM wanawanunulia pombe wananchi katika moja ya kilabu.
Kamanda Mungi alisema wafuasi wa CHADEMA na mbunge wao walipofika katika kilabu hicho cha pombe, waliwakuta watu wawili waliokuwa wamevalia sare za CCM.
Alisema wafuasi hao waliteremka kwenye gari na kuanza kuwapiga vijana hao wakiongozwa na Mchungaji Msigwa ambapo tukio hilo lilishuhudiwa na mmoja wa askari waliokuwepo katika eneo hilo.
"Askari huyu ni A/INSP Ibrahim, ambaye kwa kushirikiana na askari wengine, walimkamata Mchungaji Msigwa, kumuweka rumande, kijana aliyejeruhiwa yupo mahututi na amelazwa katika Hospitali ya Mkoa," alisema Kamanda Mungi.
Aliongeza kuwa, pamoja na wafuasi wa CHADEMA kumjeruhi kijana huyo, pia waliiharibu pikipiki yenye namba za usajili T 209 AKH aina ya T-Better ambayo ni mali ya Bw. Meshack Idd lakini nao walikamatwa na kufikishwa kituoni.
Alisema katika vurugu hizo, mfuasi wa CHADEMA Bw. Alex Mpiluka, alijeruhiwa kwenye jicho na wafuasi wa CCM, Bw. Mashaka Idd (22) na Bw. Paulo Mapunda (56), ambao wanashikiliwa kwa uchunguzi zaidi.
Msigwa afikishwa mahakamani
Ka t ika ha tua ny ing ine , Mchungaji Msigwa jana alifikishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Iringa kwa tuhuma za kujeruhi.
Mchungaji Msigwa anatuhumiwa kutenda kosa hilo juzi kwa kumjeruhi Bw. Kaita kwenye mkutano wa kampeni ya kumnadi mgombea wa udiwani wa CHADEMA, kata ya Nduli, Bw. Ayub Mwenda.
Akisomewa shtaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Godfrey Isaya, wakili wa Serikali Elizaberth Swai alidai Februari 5 mwaka huu, katika Kata ya Nduli, mtuhumiwa bila kukusudia alimjeruhi Kaita kinyume cha sheria sura ya 16 ya mwaka 2002 kifungu cha 225 cha kanuni ya adhabu.
Hata hivyo, Mchungaji Msigwa alikana kuhusika na kosa hilo ambapo wakili Swai aliiambia mahakama kuwa, upelelezi wa shtaka hilo haujakamilika na kuomba mahakama ipange tarehe ya kusikilizwa tena.
Mahakama ilikubali ombi hilo na kuipanga Machi 10 mwaka huu ambapo Hakimu Isaya alisema dhamana ya mtuhumiwa iko wazi kwa kuwa na wadhamini wawili ambapo Mchungaji Msigwa alitimiza masharti ya dhamana na kuachiwa.
Mchungaji Msigwa alidhaminiwa na Mbunge wa Viti Maalumu, Chiku Abwao na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Iringa Lilian Msomba.
Jeshi la Polisi liliimarisha ulinzi katika Kituo cha Polisi Kati ambako Mchungaji Msigwa aliwekwa rumande pamoja na eneo la mahakama.
Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), wakiwa na mabomu ya machozi, walionekana wakifanya doria eneo la mahakama na kuwataka wananchi wasikusanyike nje ya viwanja hivyo.
Wa f u a s i wa CHADEMA walifurika mahakamani hapo na kukaa vikundi ambapo baada ya Mchungaji Msigwa kutoka katika chumba cha mahabusi kupelekwa kizimbani, wanachama hao walionesha ishara ya vidole viwili.
Baada ya kupewa dhamana, wanachama walitoka haraka nje ya jengo la mahakama ambapo wakati Mchungaji Msingwa akitoka, wafuasi hao walimbeba juu juu na kuanza rasmi maandamano ya kwenda katika ofisi za chama hicho Wilaya zilizopo eneo la Mshindo.
Akizungumza na wafuasi hao, Mchungaji Msigwa alisema; "Nawashukuru sana kwa kuniunga mkono katika kipindi hiki kigumu, naondoka kwenda kujiandaa kwa ajili ya kwenda katika kampeni za udiwani Nduli naomba wale wote wanaotaka kuungana nami wajitokeze," alisema.
Alisema kesi aliyofunguliwa ni ya kisiasa na kwamba yeye wanamuonea kwa kuwa alikuwa akizungumza jukwaani na hakumpiga mtu zaidi ya kulisikia tukio hilo," alisema.

No comments: