Saturday 26 April 2014

Simba yatema kikosi kizima

Wachezaji wa Simba wakipewa maelekezo na Kocha Logarusic.

Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic amesema analazimika kutema wachezaji wasiopungua 11 ambao ni sawa na kikosi kizima kinachoweza kucheza mechi ya ushindani.
0Share
UKITAKA mafanikio lazima uchukue uamuzi mgumu ambao hakuna anayeweza kufikiria kabla.
Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic amesema analazimika kutema wachezaji wasiopungua 11 ambao ni sawa na kikosi kizima kinachoweza kucheza mechi ya ushindani.
Lengo la Logarusic kufanya hivyo ni ili aweze kujenga upya timu ya ushindani msimu ujao.
Logarusic sasa ana uhakika wa kubaki Simba, baada ya kuhakikishiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu hiyo, Zacharia Hans Pope kwani awali hakuwa na uhakika wa kuendelea kubaki katika timu hiyo kutokana na mkataba wake kumalizika.
Kocha huyo atasaini mkataba wa miaka miwili baada ya ule wa miezi sita kufikia tamati.
Katika ripoti yake kwa uongozi wa timu hiyo, Logarusic amewaeleza wazi viongozi wake kuwa, ili Simba iwe na ushiriki mzuri msimu ujao wa Ligi Kuu Bara lazima nyota 11 wa timu hiyo waachwe ili wapatikane wengine watakaoisaidia timu kufikia mafanikio.
Akizungumza na Mwanaspoti usiku wa kuamkia jana Ijumaa dakika chache kabla ya kupanda ndege kwenda kwao Croatia kwa mapumziko, Logarusic alisema wachezaji anaotaka kuwaacha si kwamba hawana viwango vizuri, tatizo hawana nafasi kikosi cha kwanza.
“Simba inahitaji ubingwa, unawezaje kuupata bila ya kuwa na wachezaji wenye uwezo? Nimekabidhi ripoti yangu tayari kwa uongozi sioni sababu ya kuficha mambo yaliyo wazi ni kwamba nataka kubaki na wachezaji 13 tu katika kikosi cha sasa.
“Nimewaambia viongozi nataka kurudi kuanzia Juni kufanya kazi moja ya kurudisha heshima ya timu hii, katika hilo hao niliowaona hawana nafasi Simba watajua kwa kuwapeleka, chini yangu hawana nafasi, nataka wachezaji wenye uzoefu mkubwa na wanaozitumikia timu za taifa.
“Tazama benchi nina wachezaji wengi kuliko kikosi cha kwanza na ikitokea mchezaji mmoja anaumwa napata presha sina mtu wa uhakika wa kumpanga,’’ alisema Logarusic.
Amemaliza kazi
Logarusic ameshapiga mstari mwekundu katika orodha ya wachezaji 24 walioichezea Simba mzunguko wa pili wa msimu uliopita na kubaki na 13 tu hivyo 11 wataachwa kwa makubaliano maalum au kupelekwa kwa mkopo timu nyingine. Kabla hajaanza kuiongoza Simba, Logarusic alikuwa na wachezaji 36 ambao aliwapunguza na kubaki 24 tu.
 
 
Sababu kubwa ya kupunguza wachezaji hao ambao hakukuwa na hata mmoja aliyesajiliwa na kocha huyo ni uwezo mdogo huku wengi wakionekana kutoweza kupambana uwanjani.
Hata hivyo inadaiwa kwamba baadhi ya wachezaji wenye umri mdogo kati ya 11 wasiotakiwa na Logarusic watarudishwa Simba B ili kukuza viwango vyao.
Wanaobaki
Ingawa nyota watakaochwa imekuwa siri nzito lakini tathimini ya Mwanaspoti imebaini kuwa wenye nafasi kubwa ya kubaki ni Joseph Owino, Donald Mosoti, Nassoro Masoud ‘Chollo’, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ na William Lucian ‘Gallas’ wakati viungo ni Jonas Mkude, Said Ndemla, Ramadhan Singano, Awadh Juma, Amri Kiemba, Haroun Chanongo na mshambuliaji ni Amissi Tambwe pekee.
Watakaoachwa.
Wachezaji walio katika hatari ya kuachwa ni kipa Yaw Berko, Uhuru Seleman, Henry Joseph ambao mikataba yao imeisha. Wengine ni Abuu Hashim na Bertam Mwombeki ambao inadaiwa hawana maelewano mazuri na Logarusic huku Hassan Hatib, Ally Badru, Ramadhan Chombo ‘Redondo’, Abduhalim Humud na Zahoro Pazi wakidaiwa kutojituma na kuonyesha uwezo uwanjani.
Katibu Mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga alikiri kupokea ripoti hiyo na kusema: “Tumepokea ripoti ya kocha, kuna wachezaji amependekeza tuwaache lakini kwa sasa hatuwezi kuweka wazi majina yao.
“Tunataka kwanza kuyafanyia kazi kama viongozi na baada ya hapo tutakutana nao kuzungumza jinsi ya kuachana nao, kazi hiyo tutaifanya Jumatatu (keshokutwa).

No comments: