Tuesday 29 April 2014

Wanafunzi waliotekwa nyara Nigeria walipelekwa nchi jirani


Jamaa wa wasichana waliotekwa nyara Nigeria
Baadhi ya wasichana waliotekwa nyara na watu wanaoshukiwa kuwa wapiganaji wa kiisilamu wa Boko Haram, wanaaminika kupelekwa katika nchi jirani.
Kiongozi mmoja katika eneo la Chibok ambako wasichana hao walitekwa nyara wiki mbili zilizopita, Pogo Bitrus, ameambia BBC kuwa watu kadhaa wamewaona watu waliojihami wakiwa wanavuka mpaka na washichana hao na kuingia Cameroon na Chad.
Baadhi ya wasichana walikuwa wamelazimishwa kuolewa na wapiganaji hao.
Bwana Bitrus alisema kuwa wasichana 230 bado hawajapatikana tangu tukio la utekaji nyara katika shule ya mabweni mjini Chibok katika jimbo la Borno wiki mbili zilizopita.
Kundi la wapiganaji wa Boko Haram limelaumiwa kwa tukio hilo ingawa bado halijasema chochote.
Bwana Bitrus, ambaye ni kiongozi mmoja wa eneo hilo, alisema kuwa wasichana 43 walifanikiwa kutoroka, wakati wengine 230 bado wanazuiliwa.
Idadi hii bila shaka ni kubwa kuliko taarifa za awali zilizvyosema ingawa hakuwa na uhakika ikiwa idadi hiyo ni sawa.
Wanafunzi hao walikuwa wanajiandaa kufanya mitihani yao ya mwisho wa muhula na kwamba wako kati ya umri wa miaka 16 na 18.
''Baadhi yao wamepelekwa nchini Chad huku wengine wao wakipelekwa nchini Cameroon,'' alisema bwana Bitrus.
Bwana Bitrus alisema kuwa kulikuwa na ripoti kwamba baadhi ya wasichana hao wamefanywa kuwa wake za wapiganaji hao.

No comments: