Saturday 26 April 2014

Jaydee anapiga karate hatari

WAKATI sherehe za miaka 41 ya Chuo cha Karate cha Okinawa Goju Ryu cha Dar es Salaam zikifanyika leo Jumamosi, mmiliki wa Bendi ya Machozi, Lady Jaydee atatunukiwa mkanda mweupe baada ya kufanya vyema katika mafunzo.
Kwa mujibu wa mkuu wa chuo hicho, Sensei Wilfred Malekia, shehere za chuo hicho zimepangwa kuanza saa 12 jioni Shule ya Zanaki, Dar es Salaam.
Malekia alisema katika sherehe hizo mambo mbalimbali yatafanyika ikiwamo kuadhimisha kumbukumbu za muasisi wa chuo hicho, marehemu Camara Bomani Goju Ryu Jundokan aliyefariki mwaka 2009.
“Hii ni sherehe muhimu kwetu, itawakutanisha watu mbalimbali waliopitia mafunzo katika chuo hiki ambao wanafanya shughuli zao nyingine,” alisema Malekia.
Akimzungumzia Lady Jaydee, Malekia alisema kuwa mwanamuziki huyo amejiunga na chuo hicho  miezi sita iliyopita na amekuwa akifanya vyema katika mafunzo yake.
Mbali na Lady Jaydee ambaye pia anafahamika kwa jina la Komando, wanawake wengine watatu nao watavishwa mkanda mweupe.
“Mafunzo haya ni muhimu sana katika maisha ya kila siku, ndiyo maana katika chuo chetu, kuna wanafunzi wa rika mbali mbali ambao wanafanya mafunzo hapa,” alisema.
Kwa upande wake, Jaydee alisema kuwa ameamua kujiunga na mafunzo hayo kwa sababu mbalimbali ikiwamo kumpa stamina katika kazi yake ya kuimba na kujilinda.
Alisema kuwa mazoezi hayo yanamfanya awe na uwezo wa kufanya shoo zake mbali mbali tokea mwanzo hadi mwisho bila kuchoka.

No comments: