Friday 25 April 2014

UKAWA wapata mpinzani

KAMATI ya Tanzania Kwanza nje ya Bunge Maalumu la Katiba, inatarajia kufanya maandamano na mikutano nchi nzima wakipinga kitendo cha baadhi ya watu kutumiwa na nchi za Magharibi kwa lengo la kuigawa nchi vipande, kutawala Visiwa vya Zanzibar.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw. Augustino Matefu, alisema lengo la ziara yao nchi nzima ni kutoa elimu kwa wananchi kuhusu upotoshaji unaofanywa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) juu ya mchakato wa kupata Katiba Mpya unaoendelea nchini.
Alisema wao kama vijana wazalendo, wameamua kuweka utaifa mbele vyama baadaye ili kulipinga jambo hilo kwa hoja, gharama zozote kwani baadhi ya watu wanaounda umoja huo, wamefikia hatua ya kuwatusi waasisi wa Muungano, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Abeib Amaan Karume.
"Sisi Tanzania Kwanza nje ya Bunge, tunawasihi Wazanzibari wawakatae UKAWA ambao wamewakashifu waasisi wetu wa Muungano hivyo tuwaone kama wahaini wa Muungano na tutawapinga kwa maandamano na mikutano yao," alisema.
Aliongeza kuwa, mikutano ya hadhara na maandamano ambayo wataifanya, itafanyika kikanda ambapo viongozi wa kanda husika watatoka nje na ndani ya Bunge hilo ambapo Kanda ya Kaskazini itaongozwa na Dkt. Harrison Mwakyembe.
Kanda ya Nyanda za Juu Kusini itaongozwa na Profesa Mark Mwandosya, Kanda ya Magharibi (Mwigulu Nchemba), Kanda ya Kati (Saidi Nkumba) na Kanda ya Kusini (Pandu Ameir Kificho).
Nyingine ni Kanda ya Mashariki (Nape Nnauye), Kanda ya Mwanza (Paul Makonda), Pemba (Hamad Rashid) na Unguja Juma Sadifa.
Bw. Matefu aliongeza kuwa, vyama vingine vya siasa ambavyo vinaiunga mkono Tanzania Kwanza kutoka upinzani ni Chama cha Kijamii (CCK), CHAUSTA, TADEA, TADEA na CHAUMA.
Alisema Bw. Rashid ambaye ni mbunge wa CUF, ataongoza maandamano na mikutano akisaidiwa na Bw. Renatus Muhabi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa CCK.
Kwa upande wake, Bw. Muhabi alisema yeye haiungi mkono UKAWA ila anaungana na Tanzania Kwanza nje ya Bunge hilo na kusisitiza kuwa, Rais alipaswa kutoa fursa kwa wananchi waweze kupigakura ya kuwachagua wajumbe wa Bunge la Katiba badala ya kuwachagua yeye.
"Mimi sipo upande wa UKAWA wala CCM ila ninachotaka ni makundi haya yawe pamoja tuweze kufanya mjadala wa kupata Katiba bora na kuangalia ni jinsi gani Bunge hili linaweza kuendelea bila kuwa na matabaka," alisema.

No comments: