Tuesday 21 January 2014

Tambwe,Ramadhani Singano'" Messi"' warejea Simba



Wakati kikosi cha Simba jana jioni kiliendelea na maandalizi ya mechi za mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara ambayo itaanza Jumamosi kwenye viwanja mbalimbali nchini, hatma ya kambi ya timu hiyo iko mikononi mwa kocha Zdravko Logarusic, imeelezwa jana jijini Dar es Salaam.

Pia wachezaji nyota ambao hawakuwapo katika mechi ya kirafiki dhidi ya Mtibwa Sugar Jumamosi wakiongozwa na kipa Ivo Mapunda, Ramadhani Singano 'Messi', Amri Kiemba, Haroun Chanongo, Joseph Owino, Issa Rashid na Amisi Tambwe, jana walianza mazoezi pamoja na wachezaji wenzao.

Akizungumza na gazeti hili jana, kocha msaidizi wa Simba, Selemani Matola alisema Loga alikuwa hataki wachezaji waingie kambini lakini benchi la ufundi limemkatalia.
Matola alisema baada ya kumueleza hali halisi ya wachezaji wa Kitanzania, kocha huyo alisema kwamba jana jioni ndiyo wangefanya uamuzi.

"Kocha hataki kambi, ila tumemueleza ukweli kuhusu wachezaji wetu, leo (jana) jioni baada ya mazoezi tutakutana na kuamua, akikubaliana na mawazo yetu, wachezaji wataingia kambini Jumatano," alisema Matola.

Alisema wanashukuru wanaanza mazoezi wakiwa na wachezaji wote tofauti na ilivyokuwa wakati wanajiandaa kuivaa Mtibwa Sugar Jumamosi.

"Kikosi kimekamilika, wale wachezaji waliokuwa wagonjwa na majeruhi wamepona, sasa ni kikazi zaidi, wengi walichoka baada ya kutoka Zanzibar lakini wamesharejesha nguvu," aliongeza kiungo huyo wa zamani wa Simba.

Simba itaanza mzunguko wa pili Jumapili kwa kuikaribisha Rhino Rangers kwenye Uwanja wa Taifa.

No comments: