Friday 31 January 2014

Polisi wapambana na wananchi Karatu


Mamia ya wananchi wenye hasira katika Kijiji cha Bashay kilichoko wilayani hapa wamepambana na polisi kwa kuwarushia mawe kwa kile walichodai kuishinikiza Serikali kuweka matuta katika Barabara ya Karatu hadi Ngorongoro.

Tukio hilo lililotokea saa 4 asubuhi baada ya watoto wawili Priska John(5) na Happiness Filbert (5) walipogongwa na gari wakati wakivuka barabara ambapo mmoja alifariki dunia papo hapo huku Priska akikimbizwa hospitali.


Wananchi hao walifikia uamuzi huo wa kufunga barabara na kuzuia magari yakiwamo ya watalii kwa nia ya washinikiza mkuu wa wilaya kwenda kuwasikiliza na ndipo polisi walipojaribu kuondoa mawe hayo bila mafanikio.

“Tumechoka kuwaona polisi wakiokota maiti za watoto wetu barabarani kama wanaokota mizoga ya mbwa na leo(jana) tunawapiga mawe mpaka wakitumwa tena kuja kuchukua maiti ya aliyegongwa na gari wakatae,”alisikika mama mmoja akipaza sauti kwa uchungu.

Vurugu kati ya wananchi na polisi zilianza huku wananchi wakiporomosha mawe pasipo kujali wanarushia polisi au magari yaliyokuwa yakipita huku polisi walipambana kwa kurusha mabomu ya machozi kwa takribani saa mbili.

Hata hivyo katika vurugu hizo hakuna aliyeripotiwa kuumia huku wananchi wakiitupia lawama Serikali kwa kushindwa kuweka matuta katika barabara hiyo ambapo mara kwa mara ajali zimekuwa zikiripotiwa kutokea katika Barabara ya Karatu hadi Ngorongoro.

Akizungumzia tukio hilo Mtendaji wa Kijiji cha Bashay, Joseph Surumbu alikiri kutokea kwa tukio hilo ambapo alisema, ajali katika eneo hilo zimekuwa zikitokea mara kwa mara huku akiitupia lawama Seriklai kwa kushindwa kuweka matuta katika eneo hilo.

Hili ni tukio la pili kutokea kwa kipindi cha miezi mitatu kwa wananchi kupambana na polisi baada ya watoto kugongwa wakishinikiza barababa hiyo kuwekwa matuta.

Daktari kiongozi wa Hospitali Teule ya Wilaya, Daniel Simpa alithibitisha kuupokea mwili wa mtoto Happiness Filbert huku mwenzie akiwa amejeruhiwa na anaendelea na matibabu.

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

No comments: