Saturday 25 January 2014

Mtoto aliyepigwa na baba yake kisa hafanani naye afariki

hospital ya wete

Mtoto Mwaru Lunard Sabil (9) aliyepigwa na kuumizwa vibaya na baba yake mzazi na kisha kulazwa katika Hospitali ya Wete, Pemba akipatiwa matibabu amefariki dunia na baba huyo anashikiliwa na polisi kutokana na tukio hilo. Baba huyo mkazi wa Junguni Gando, Pemba, anadaiwa kumpiga na kumjeruhi vibaya mtoto huyo kwa madai kuwa hafanani naye sura hivyo si mtoto wake.

Taarifa ilizopata NIPASHE jana na kuthibitishwa na Daktari wa Wodi ya Watoto katika Hospitali ya Wete, Sada Juma Mbwana zilisema mtoto huyo amefariki dunia kutokana na maumivu makali aliyoyapata. Alisema mtoto huyo alifikishwa katika hospitali hiyo Januari 16 mwaka huu majira ya saa nne asubuhi na mama yake mzazi, akidai kwamba mwanawe anasumbuliwa na maradhi ya kukohowa.

Alisema taarifa kwamba mtoto huyo alipigwa zilibainika baada ya askari polisi kufika hospitalini hapo wakiwa na fomu ya matibabu na baada ya kumdadisi mama mzazi alifichua kwamba mwanawe amepigwa na baba yake.

“Mtoto alipofikishwa hospitalini tuliambiwa anasumbuliwa na kifua (anakohoa) lakini mambo yalikuwa mengine baada ya polisi kufika wakiwa na fomu ya PF3 ndipo mama mzazi alipoeleza kwamba mwanawe amepigwa na baba yake ” alisema Sada. Alisema wakati wakimfanyia uchunguzi mtoto huyo, walibaini kwamba alikuwa na alama za fimbo mgongoni na Jumatano iliyopita walilazimika kumuongeza damu kutokana na hali ya afya yake kubadilika.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, Shakhan Mohammed Shakhan, amesema Jeshi la Polisi linamshikilia baba mzazi wa mtoto huyo mwenye umri wa miaka 39 kutokana na tukio hilo.

Aliongeza kusema kuwa mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumatatu ijayo kujibu tuhuma zinazomkabili . Kamanda Shekhan amewataka wananchi kuacha kujichukuliwa sheria mikononi bali wavitumie vyombo vya sheria ambavyo vipo kwa ajili ya kulinda, kutetea na kusimamia haki za wananchi wote.

No comments: