Sunday 2 November 2014

Chadema yaanzisha programu mpya Sasa kujiunga, kupata habari, kuchangia ni kwa simu

Hafla ya uzinduzi wa program tatu za kujieneza kwa njia ya mtandaoKATIKA kujipanga kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimezindua program tatu za kujieneza kwa njia ya mtandao huku wakikibeza Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba bila ya kutegemea msaada wa vyombo vya dola, chama hicho ni sawa na karatasi nyeupe.
Kauli ya CHADEMA ilitolewa juzi usiku jijini Dar es Salaam katika hafla ya uzinduzi wa program hizo, ambapo kuanzia sasa wafuasi wa chama hicho wanaweza kujiunga, kupata taarifa za chama na kuchangia kwa njia ya mtandao wa simu popote watakapokuwa.
Akitambulisha teknolojia hiyo mpya, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe alisema kuwa program hizo zinatambulika kama e-membership, CHADEMA Media na e-payment.
Mbowe alisema kuwa kwa kupitia mtandao wa simu, sasa wananchi wanaweza kujiunga na kuwa wanachama wa CHADEMA na kuasajiliwa popote pale walipo.
“Na kwa njia hii ya CHADEMA Media, wafuasi wetu na wananchi kwa ujumla watapata taarifa zote kuhusu chama na viongozi wao wakati wowote kupitia simu zao mapema kabisa na hata kabla ya habari hizo hutangazwa kwenye vyombo vingine vya habari,’ alisema.
Kuhusu program ya e-payment, Mbowe alisema kuwa, wanachama na wapenzi wa CHADEMA wataweza kuchangia chama kwa njia hiyo ya mtandao ambapo mchangiaji anayetumia mtandao wa Vodacom anapiga *150*00# kisha anachagua kipengele cha nne cha malipo, kisha anaweka namba ya kampuni ambayo ni 213040, halafu anaingiza namba ya kumbukumbu ambayo ni M4C kisha anamalizia kwa kuweka namba yake ya siri, tayari mchango wake unapokelewa.
“Baada ya mchangiaji kufikia hatua ya mwisho ya kutuma mchango wake, atapokea ujumbe wa shukrani na kwa wale wanaotaka majina yao yafahamike, ukifika kipengele cha kuingiza namba ya kumbukumbu ya M4C, anaweka na jina lake bila kuacha nafasi (mfano: M4CMbowe),” alisema.
Waiponda CCM
Mbowe aliawatoa hofu wafanyabiashara na wewekezaji akisema kuwa wasitishike kuviunga mkono na kuvisaidia vyama vya upinzani kwa hofu kwamba salama yao iko ndani ya CCM.
Alisema kuwa salama ya wafanyabiashara hao na wawekezaji ni kufanya shughuli zao katika mazingira halali ya kutokwepe kodi.
“Kwa sababu tunaunga mkono uwekezaji wenye usawa, usio na rushwa wala urasimu na umangi meza, sisi kama CHADEMA na hata UKAWA kwa ujumla tutashirikiana nao wakati wote,”alisema.
Mbowe alisisitiza kuwa CCM wamechoka, na kwamba uthibitisho wa hilo ni kauli ya Rais Kikwete hivi karibuni akiwa nchini China aliposema kuwa amechoka anataka kupumzika.
“Sasa kama mwenyekiti wao, Rais Kikwete anasema amechoka, nyie mtafanyaje? Alihoji Mbowe na kusema kuwa CHADEMA kwa kushirikiana na UKAWA wana uwezo wa kuunda serikali adilifu itakayorejesha heshima ya Tanznaia.
Naye Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alitamba kuwa kuwa bila msaada wa vyombo vya dola, CCM ni wepesi mithiri ya karatasi nyeupe.
Alisema kuwa CHADEMA imekuwa ikikua kila wakati kulingana na takwimu za matokeo ya viongozi wa ngazi zote wanayozidi kuyapata kila uchaguzi.
Dk. Slaa ambaye alianza kwa kuelezea historia ya CHADEMA akisema anataka wasiotambua waweze kuelewa ili kuondosha upotoshaji unaoenezwa kwamba chama hicho ni cha Wachaga wa kanda ya Kaskazini, alisema kuwa kwa sasa wana viongozi wa serikali za mitaa, vitongoji, vijiji, madiwani na wabunge kila kona ya nchi.
Alisema kuwa nchi imekuwa maskini kutokana na ufisadi wa viongozi ambao unawanyiwa wananchi fursa ya kuzitumia rasilimali zao.
“Mzee Edwin Mtei, muasisi wa CHADEMA, alitofautiana na hayati baba wa Taifa, mwalimu Julius Nyerere kwa sababu ya kupigania ili kila Mtanzania ashiriki keki ya Taifa.
“Leo tunachangishana fedha za kujenga maabara katika sekondari kwa sababu hiyo ya umaskini unaotokana na ufisadi. Ufisadi wa fedha za EPA tulioufichua kwa lengo safi, Kikwete aligusa tu kipengele kimoja lakini ufisadi wenyewe ulikuwa mkubwa,” alisema.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, fedha hizo ndizo zilipaswa kununulia dawa hospitalini, kujengea shule na maabara, kuleta huduma ya maji safi na salama na huduma zingine za kijamii badala ya serikali ya CCM kuwashurutisha wananchi kwa michango.
“Wakati huo mageuzi yanaanza ukizungumza upinzani, inabidi kwanza augeuke nyuma kuona nani anakutazama, lakini leo tunatembea vifua mbele,” alitamba.
Mchakato wa katiba
Dk. Slaa alidai kuwa Rais Kikwete aliingilia ilani ya CHADEMA kuhusu mchakato wa katiba mpya lakini akaitafsiri vibaya kwamba walisema wataandika katiba mpya ndani ya siku 100.
“Sasa kama mtu mzima hawezi kusoma akaelewa kilichoandikwa, unamfanyaje? Sisi kwa katiba hii mpya inayopendekezwa ambayo imechakachuliwa, tunasema hapana…hapana…hapana. Safari ya kuandika katiba mpya ndiyo inaanza,” alisema Dk. Slaa.
Naye alitamba kuwa kama CCM walifikiri wamemaliza kazi ya mchakato wa kuandika katiba mpya, basi watakutana nao kwa wananchi.
“Kura walipiga wenyewe, wakahesabu wenyewe, wakachakachua wenyewe, wakajiibia wenyewe, wakabebana wenyewe, wakatekenyana wenyewe, wakacheka wenyewe, wakatangaza matokeo wenyewe, wakashangilia wenyewe na kucheza wenyewe kwenye ukumbi wa Bunge,”alisema.
Mbatia anena
Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema Watanzania wanapaswa kuungana kwa pamoja ili kumwokoa mama Tanzania ambaye amezingirwa na watu wabaya hasa mafisadi.
Alisema kwa pamoja bila kuangalia itikadi, dini na rangi zao, Watanzania wanapaswa kuhakikisha wanaiondoa CCM katika uchaguzi wa Serikali za Mtaa na uchaguzi mkuu ujao.
“Mara nyinyi napenda kuiita Tanzania mama lakini watu hawanielewi ni kwa sababu gani … namaanisha namna mama alivyo mkarimu kwa mtoto wake wakati ananyonyesha maziwa na namna avyoilea familia na jamii kwa huruma na upendo, hivyo ndivyo watanzania tunavyotakiwa kumpenda mama Tanzania kwa vitendo” alisema Mbatia.
Mwenyekiti huyo alisema wengi wasiomtakia mema mama Tanzania walishtushwa na muungano wa UKAWA wa Oktoba 26 mwaka huu, hasa walidhani hawatafikia kuaminiana, lakini waliweza kuwa wamoja.
Alisema kinachofanywa na UKAWA sasa ni kumsaidia kila mtu kutumia uwezo wake katika kusukuma gurudumu la mabadiliko na mafanikio ili CCM ikiwa inaendelea kujifisadi wao wanaendeleza mapamabano ya maendeleo.
“Nadhani UKAWA tunatakiwa kuutunza na kuuheshimu muungano wetuu…yoyote atakeyetaka kuuvuruga tumkabidhi kwa kaka zetu na vikongwe wa siasa za vyama vingi Prof. Mwesiga Baregu na Wakili Mabere Marando,”alisema.
Akifunga hafla hiyo, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Marando alisema watanzania wanapaswa kufurahia ushindi kwa maana watashinda katika ndoto waliiota katika viwanja vya Jangwani.
“Katika viwanja vya Jangwani juzi nilitokwa na machozi baada ya kuwaona Mbowe na Mbatia wakisaini makubalianao ya kushirikiana kisiasa…nakumbuka walikuwa wadogo sana wakati tunaanza siasa za mageuzi, kumbe leo mabadiliko yametimia,” alisema Marando.
Alisema wakati wa kumsimamisha mmoja aweze kugombea nafasi mojawapo ya uongozi, watawafungia wagombea wote wa UKAWA katika chumba kimoja ili wamchague mmoja wenyewe katika mapambano na CCM.
Marando alitoa Rai kwa watanzania na wana UKAWA kwamba atakaporejeshwa mmoja kwa ajili ya kinyang’anyiro, wahakikishe wanampigania ili aiondoe CCM madarakani kwa maendeleo yao.

No comments: