Saturday 8 November 2014

Phiri amtetea Jonas Mkuda

Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Phiri amemshauri kiungo wake  chipukizi, Jonas Mkude asiondoke ndani ya timu hiyo kwa sasa na  kumwambia akienda Yanga amekwisha.
Mkude  ambaye amebakiza miezi sita kwenye mkataba wake anahusishwa  kisheria kufanya mazungumzo na hata kujiunga na Yanga au Azam  ambao wameonekana kumfuatilia kwa karibu kutokana na kiwango chake kikubwa uwanjani.
Phiri alisema jana kuwa siyo wakati mwafaka kwa Mkude kuondoka Simba kwani  bado anahitaji  kuimarisha kipaji chake na  kujikuza kiakili.
Kocha huyo ambaye ameshahakikishiwa usalama wa ajira yake na uongozi wa klabu hiyo, alisema  endepo mchezaji huyo ataondoka kwenda Azam au Yanga, basi atakwenda kumaliza kipaji chake.
“Mimi kama kocha sikubali kumwachia mchezaji kama Mkude kwani bado ana umuhimu na ni kijana mwenye uwezo mkubwa na kocha yeyote angependa kuwa naye kikosini. Lakini, ninachomshauri asiwe na haraka ya kuondoka ndani ya Simba kwani bado anatakiwa  kubaki na kuimarisha zaidi  kipaji chake na kukuza akili ili hapo baadaye  aweze kwenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi,” alisema.
Aliongeza: “Kama akienda Yanga au Azam ataharibu kipaji chake kwani Simba ndio sehemu pekee inayowapa kipaumbele vijana.”
Katika hatua nyingine, suala  la kuwajadili wachezaji waliosimamishwa, Shaban Kisiga, Amri Kiemba na Haruna Chanongo limewekwa kiporo baada ya Kamati ya Utendaji kuamua kwa pamoja kulisogeza mbele na sasa wanashughulikia suala moja tu la kuhakikisha timu yao inapata ushindi  dhidi ya Ruvu Shooting.
Wachezaji hao walisimamishwa kwa sababu tofauti baada ya Simba kutoka sare ya bao 1-1 na Prisons jijini Mbeya wiki mbili zilizopita.
Kisiga alisimamishwa kwa utovu wa nidhamu kwa madai ya kuwajibu lugha chafu viongozi wake wakati Kiemba na Chanongo wanatuhumiwa  kucheza chini ya kiwango.
Imeelezwa kuwa kamati hiyo ikiongozwa na rais wa klabu hiyo, Evans Aveva iliamua kuachana na suala hilo baada ya kutokamilika kwa baadhi ya mambo na hivyo kuona hakuna haja ya kuendelea kulijadili.

No comments: