Tuesday 29 July 2014

Chadema Yaendelea kujiweka sawa

Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Uchaguzi, Benson KigailaKATIKA kuhakikisha uchaguzi mkuu wa taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), unaendeshwa kwa uwazi na umakini ili kuepuka mitego ya kuchomekewa wasaliti, chama hicho kimejipanga upya na kuusogeza hadi Septemba 14 badala ya Agosti 31.
Hatua hiyo ni baada ya Kamati Kuu kubaini kwamba hakuna chombo cha kuusimamia uchaguzi huo, na sasa imeamua jukumu hilo lifanywe na Baraza la Wazee Taifa.
Kwa mujibu wa ratiba mpya iliyotangazwa jana na Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Uchaguzi, Benson Kigaila, uchaguzi wa Baraza la Wazee ndio utatangulia kufanyika Septemba 6, ili kutoa nafasi kwa chombo hicho kusimamia uchaguzi mkuu.
Kigaila alisema kuwa mkutano mkuu wa kuwachagua mwenyekiti, makamu mwenyekiti Bara na Visiwani, utatanguliwa na chaguzi za mabaraza ngazi ya kitaifa.
“Hadi kufikia Julai 30, uchaguzi wa kata utakuwa umekamilika na Agosti 15, mwaka huu, uchaguzi wa majimbo na wilaya nao unapaswa kukamilika ili kuruhusu uchaguzi ngazi ya mkoa uanze hadi Agosti 30 mwaka huu,” alisema.
Kigaila alisema uchaguzi wa Baraza la Vijana (Bavicha) utafanyika Septemba 10 huku ule wa Baraza la Wanawake (Bawacha) ukipangwa kuwa Septemba 11.
“Baada ya chaguzi hizo za mabaraza kukamilika, Kamati Kuu ya sasa itakutana Septemba 12 kwa ajili ya kuandaa kikao cha Baraza Kuu kitachaofanyika Septemba 13 mwaka huu, ili kuandaa mkutano mkuu wa Septemba 14,” alisema.
Alisema baada ya mkutano mkuu, Baraza Kuu litakaa Septemba 15 kwa ajili ya kumchagua Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu Bara na Visiwani ili Kamati Kuu mpya iweze kutambulishana.
Kigaila aliwataka wanachama wenye nia ya kugombea nafasi mbalimbali za kitaifa kuchukua fomu kuanzia Agosti 10 hadi 25 katika ofisi za majimbo, wilaya, makao makuu ya mabaraza hayo na ofisi za chama.
Alisema fomu hizo zinaweza kupatikana pia katika mitandao ya mabaraza hayo na chama, lakini alionya kwamba lazima fomu hiyo baada ya kujazwa irejeshwe katika makao makuu ya mabaraza hayo na chama ili iweze kulipiwa.
“Gharama zinazotozwa kwa mgombea wa uenyekiti, katibu, mratibu wa uenezi, mweka hazina na mwenyekiti wa kamati ya uratibu kama kwenye wilaya kuna jimbo zaidi ya moja ni sh. 10,000.
“Gharama za kugombea nafasi ya mwenyekiti, makamu wenyeviti, katibu mkuu, naibu katibu Bara na Visiwani ni sh. 50,000… mratibu wa uenezi na mweka hazina ni sh. 30,000, wajumbe wa Baraza Kuu na Mkutano Mkuu ni sh. 25,000,” alisema Kigaila.
Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Antony Komu, alisema CHADEMA inatarajia kutumia sh. milioni 700 katika  uchaguzi huo, hivyo aliwataka wagombea  wote kuhakikisha wanalipia fomu baada ya kujaza.
Hata hivyo, aliwaomba wanachama na wapenzi wa chama hicho kujitolea kwa ajili ya kufanikisha uchaguzi huo ambao alisema utakuwa na watu zaidi ya 1,000 ambao watatoka nje ya Dar es Salaam.
Kaimu Mwenyekiti wa Bawacha, Suzan Lyimo, aliwataka wanawake nchini kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika chaguzi zinazoendelea ili kuwa na uwiano sawa na wanaume.

No comments: