Thursday 10 July 2014

Sumatra walia na wananchi Kilimanjaro

MAMLAKA ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra), Mkoa wa Kilimanjaro, imewaomba wananchi kutoa taarifa kwa askari wa usalama barabarani pale wanapopanda daladala ambazo madereva wake hawazingatii sheria zilizowekwa ikiwamo kutovaa sare.
Akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa, Ofisa Mfawidhi Kanda ya Kaskazini, Fabian Nyang’oro, alisema kati ya mikakati waliyojiwekea mkoani hapa ni pamoja na kufanya ukaguzi kwa magari yote yanayobeba abiria ili kubaini kama yanatekeleza taratibu zilizowekwa na mamlaka hiyo.
Alisema mikakati hiyo itaweza kufanikiwa endapo walengwa watazingatia maagizo hayo, huku akiwaomba wananchi mkoani hapa kushirikiana na mamlaka hiyo kwa kutoa taarifa kwa askari wa usalama barabarani pindi wanapopanda magari ambayo ni mabovu.
“Mikakati tuliyojiwekea kwa kipindi cha mwaka 2014/2015 ni pamoja na kuwachukulia hatua wale wote wanaokiuka sheria za usalama barabarani, dereva na kondakta atakayekutwa hayuko nadhifu, hajavaa sare na breki za gari lake hazina raba, atanyang’anywa leseni yake na gari kuzuiwa kufanya kazi,” alisema.

No comments: