Saturday 20 June 2015

Mbowe awang'ang'ari awatoa wasiwasi wanachama wa chadema Hai

Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amezungumzia hatma yake kisiasa baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Hai, mkoani Kilimanjaro kumtia hatiani katika kesi ya shambulio,  akisema hajapoteza sifa ya kutetea ubunge wake katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
 
Mbowe alihukumiwa juzi na mahakama hiyo kwenda jela mwaka mmoja au kulipa faini ya shilingi milioni moja baada ya kupatikana na hatia katika kesi namba 73 ya mwaka 2011 iliyokuwa imefunguliwa na Mwangalizi wa Ndani wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Nassir Uronu.
 
Hata hivyo, Mbowe alifanikiwa kulipa faini hiyo na kuepuka kwenda jela kutumikia kifungo cha mwaka mmoja.
 Akiwahutubia wakazi wa mji wa Bomang’ombe uliopo wilayani hapa ja  ikiwa ni siku moja tangu mahakama itoe hukumu hiyo, Mbowe alisema: “Nimezungumza na wanasheria makini na wameniambia kwamba siyo tu wanataka kutetea rufaa yangu bali pia kupinga mifumo ya ukandamizaji. Kwa hiyo wanataka kufanya hivyo pia ili kuniondolea doa la uadilifu kama kiongozi.”  
 
Alisema na kuongeza:
“Kuna wakati fulani nilishawishiwa nitoe hongo ili kesi hii imalizike lakini nilikataa na nikasema siwezi kufanya hivyo. Kwangu ni haramu kutoa rushwa na hata hivyo siwezi kuachia ubunge wa Hai, nyie wananchi wangu mnajua, nimewauliza hapa na mmenipa ruhusa kugombea.” 
 
Katika kesi hiyo, Nassir aliyekuwa Mwangalizi wa ndani kutoka Baraza la Waislamu Tanzania (Bakwata) alidai kushambuliwa kwa kipigo akiwa katika kutuo cha kupigia kura cha Zahanati ya Kijiji cha Nshara, kata ya Machame Kaskazini, wilaya ya Hai.
 
Katika mkutano huo wa jana baadhi wa wabunge wa Chadema walihudhuria akiwamo Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini, Wabunge wa Viti Maalum, Rose Kamili, Grace Kihwelu, Cecilia Pareso, Joyce Mukya, Paulina Gekul na Lucy Owenya, huku wakieleza kumuunga mkono Mbowe kutetea kiti chake cha ubunge.
 
Katika mkutano huo, Mbowe aliwakabidhi pia wananchi wa wilaya ya Hai lori la tani 50 aina ya Mercedez Benz ambalo litatumika kuzoa takataka katika maeneo yote ya jimbo hilo, ikiwa ni ahadi yake aliyoitoa wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
 
Kesi hiyo ya uchaguzi mkuu uliopita, imekuwa ikivuta hisia za wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro kutokana na nguvu ya kisaisa aliyonayo mwenyekiti huyo wa Chadema  na na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni. 
 
Katika uchaguzi huo, Mbowe aliibuka mshindi kwa kupata kura 28,585, akifuatiwa na Fuya Kimbita (CCM) kura 23,349, Hawa Kihogo (UDP) 258 na Petro Kisimbo (TLP) kura 135.

No comments: