Saturday 20 June 2015

Mgosi atua kwa mbwembwe Msimbazi

STRAIKA mpya wa Simba, Mussa Hassan ‘Mgosi’ aliyezifunga Yanga, Simba na Azam msimu uliopita, amesema hana shida kabisa na nafasi atakayopangwa kucheza Msimbazi kwani yuko fiti kucheza nafasi zote za ushambuliaji.
Mgosi amesajiliwa na Simba akitokea Mtibwa Sugar ya Morogoro ambako alicheza zaidi nafasi ya winga msimu uliopita licha ya kuzoeleka kucheza nafasi ya straika alipokuwa Simba miaka ya nyuma.
Mfungaji Bora huyo wa mwaka 2010, alisema anaweza kufanya vizuri akicheza straika, winga kwa pande zote mbili pamoja na kiungo mshambuliaji, hivyo kocha atakavyoamua ndivyo atakavyoitumikia timu yake.
“Sina wasiwasi na uwezo wangu, kama ulivyoona msimu uliopita nilicheza zaidi kama winga na niliifanya kazi yangu vizuri, kocha akiamua nicheze straika ama kiungo mshambuliaji bado naweza.
“Kikubwa ninachohakikisha kwa sasa ni kuuweka mwili wangu vizuri kwa ajili ya changamoto hiyo. Licha ya kwamba nimecheza kwa muda mrefu, bado nina uwezo wa kumudu nafasi hizo zote,” alisema Mgosi.
Straika huyo amerejea Simba miaka minne baada ya kutimka klabuni hapo kwenda kujaribu bahati ya soka la kulipwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kabla ya kurejea nchini na kujiunga na Mtibwa aliyoitumikia tangu mwaka 2012.
Katika hatua nyingine, Simba imepanga kuanza mazoezi yake Julai Mosi, lakini haijafahamika itakluwa wapi na programu gani zitaanza na chini ya makocha wapi.
Kocha msaidizi wa Simba, Selemani Matola, alisema anachojua yeye ni kuanza mazoezi Julai ila hajajua ni uwanja gani.
“Nimeambiwa mazoezi Julai Mosi, sijaambiwa ni wapi ndani au nje ya nchi, lakini siku zikikaribia kila kitu kitakuwa wazi lakini kwa sasa suala hilo lipo juu ya uongozi,” alisema.
Matola alisema anaamini watafanya maandalizi mazuri kwa ajili ya msimu ujao kwani wanachokihitaji wao ni kuona Simba inakuwa na mabadiliko ya kufanya vizuri.
“Kila kitu kitakwenda sawa tutafanya maandalizi kama wengine ili kuweza kuwa kwenye ushindani wa hali ya juu katika msimu ujao wa Ligi Kuu Bara,” alisema.

No comments: