Friday 19 June 2015

Pete ya UCHUMBA ya Mrembo Lulu yawa gumzo mjini

MSHTUKO! Mtoto mzuri Bongo Movies, Elizabeth Michael ‘Lulu’ amezua gumzo ukumbini baada ya kuonekana akiwa amevaa pete iliyoaminika kuwa ni ya uchumba na kusababisha minong’ono miongoni mwa mashabiki wake.

Mpango mzima ulijiri wikiendi iliyopita katika Ukumbi wa Sinema wa Mlimani City (Cinemax) kulipokuwa na uzinduzi wa sinema ya 10 Bora ya washiriki wa Shindano la Tanzania Movie Talent, mwaka jana ijulikanayo kama Mpango Mbaya.
Punde tu baada ya Lulu kuwasili ukumbini hapo mishale ya saa mbili usiku akiwa na mashosti zake, minong’ono iliibukia kwenye zulia jekundu wakati mrembo huyo alipokuwa akifotolewa picha na mapaparazi ndipo wapenda ubuyu walipoanza kusambaziana habari hali iliyosababisha watu wengi kutaka kumuona Lulu.

“Ile ni ya uchumba aise atakuwa amechumbiwa, afadhali Lulu achumbiwe na aolewe sasa japo bado anasoma lakini kwa kuwa ni chuo ni vyema na haki akaendelea na uchumba wake huku akimalizia masomo na kisha ndoa ikafuata,” alisikika mmoja wa mashabiki akiwaambia marafiki zake".


Baada ya watu kuanza kumzingira eneo hilo kutaka kuishuhudia pete hiyo, haraka sana Lulu aliondoka eneo hilo na kwenda kujibanza ukumbini kufuatilia sinema hiyo iliyokuwa imeshaanza kuoneshwa.

Paparazi wetu alifanya jitihada za kuzungumza na Lulu ili aweze kumsikia anazungumziaje pete hiyo iliyopamba kidole chake lakini hakutaka kuzungumzia lolote akidai hayupo tayari kufunguka lolote ukumbini hapo.

Hata baada ya muvi kuisha, paparazi wetu aliendelea kumfuatilia Lulu wakati anatoka ukumbini lakini pia hakutoa ushirikiano ambapo alionekana kukataa kupigwa picha pamoja na kujibu maswali ya waandishi wa habari.

No comments: