Sunday 1 June 2014

Maandamano ya shika kasi Jordani

Kuendelea maandamano dhidi ya serikali nchini JordanHuku upinzani wa wananchi dhidi ya serikali ukizidi kushika kasi nchini Jordan, askari wa usalama wa nchi hiyo wametumia ukandamizaji katika kujaribu kuzima wimbi la maandamano nchini humo. Wajordan ambao wanapinga siasa za serikali ya Amman hasa katika masuala ya kisiasa na kiuchumi, kuongezeka uhusiano kati ya nchi hiyo na utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na kufuata kibubusa siasa za Marekani katika eneo, wameeendelea kusisitizia upinzani wao kwa viongozi wa serikali. Katika fremu hiyo wakazi wa mji wa Ma'an, kusini mwa nchi hiyo hivi karibuni walifanya maandamano makubwa kwa kumiminika mabarabarani na katika medani kuu za mji huo ambapo sambamba na kusisitiza juu ya matakwa yao ya kimsingi, walitaka pia kukatwa kabisa uhusiano wa nchi hiyo na utawala haramu wa Kizayuni na kadhalika kuondolewa balozi wa utawala huo nchini mwao. Waandamanaji sambamba na kuichoma moto bendera ya utawala huo haramu na ya Marekani, waliitaja serikali ya Washington kuwa chanzo cha kuongezeka mgogoro ndani ya nchi yao. Askari wa usalama wa Jordan kwa kutumia mabomu ya kutoa machozi na risasi hai katika kuwatawanya waandamanaji, waliwapiga na kuwajeruhi makumi kati ya waandamanaji hao sambamba na kutia mbaroni makumi ya wengine. Kabla ya hapo pia, jeshi la nchi hiyo lilimuua kwa kumpiga risasi kijana mmoja baada ya kuwashambulia waandamanaji wa mji huo wa Ma'an, waliokuwa wakiandamana pia kupinga serikali ya nchi hiyo. Kitendo hicho kinatajwa kuwa sababu ya kuitishwa maandamano ya hapo juzi mjini hapo. Sambamba na kuanza kwa mapinduzi ya wananchi huko Tunisia na Misri, Wajordan nao walianzisha maandamano ya kulalamikia hali mbaya ya kimaisha na kutaka kufanyika marekebisho ya kimsingi katika muundo wa uongozi wa taifa hilo la Kiarabu. Upuuzaji wa serikali ya Amman kwa matakwa ya wananchi hasa upinzani wao kwa ufisadi mkubwa uliokita mizizi nchini humo na hatua ya serikali ya kutowachukulia hatua kali wahusika wa vitendo hivyo, ni jambo ambalo limeongeza wimbi la upinzani wa wananchi dhidi ya serikali. Uzembe na udhaifu wa serikali, umepelekea bunge la nchi hiyo hadi sasa kushindwa kuchukua hatua yoyote ya kuboresha hali ya maisha ya wananchi, na badala yake wabunge wamekuwa wakijinufaisha wao na kujaza matumbo yao wenyewe. Aidha kwa upande mwingine ukimya wa baadhi ya makundi ya kisiasa ya upinzani nchini humo, unatajwa kuwa sababu ya changamoto kwa mgogoro wa uchumi wa taifa hilo suala lililomlazimu mfalme Abdullah wa II wa Jordan kutaka kutatuliwa mkwamo wa kiuchumi na kifedha kuinuliwa kiwango cha uwekezaji ili kwa mara nyingine nchi hiyo iweze kushuhudia ustawi wa kiuchumi. Takwa la mfalme huyo linatolewa katika hali ambayo wataalamu wa masuala ya kiuchumi wanaamini kwamba, Abdullah Ensour, Waziri Mkuu wa Jordan hana tajriba ya kutosha kwa ajili ya kutatua mgogoro wa kiuchumi unaoendelea kulikumba taifa hilo. Wanasema waziri mkuu huyo hana uwezo wa kuikwamua nchi hiyo kutokana na mgogoro wa kisiasa unaoendelea kushuhudiwa ndani ya taifa hilo. Uchunguzi wa matukio ya Jordan umebaini kwamba, mabadiliko ya kiserikali yaliyofanyika hivi karibuni nchini humo yalikuwa ya kimaonyesho tu na yaliyofanyika kwa lengo la kuzihadaa fikra za waliowengi na kwamba, matatizo ya nchi hiyo hayawezi kupatiwa ufumbuzi hadi pale wananchi watakaposimama na kudai haki zao za kimsingi.

No comments: