Friday 13 June 2014

Maximo kutua Yanga baada ya mchuano ya kombe la Dunia kuisha

WANACHAMA wapato 250 wa Yanga wamejiorodhesha na kusaini ili kuzuia Mwenyekiti wao, Yusuf Manji, asiendelee kuiongoza klabu, lakini yeye wala hana habari nao, badala yake amempa kazi tatu mmoja wa watu wake aliyeenda Brazil kumaliza kazi juu ya ujio wa kocha wao mtarajiwa, Marcio Maximo.
Tayari Yanga walishamtumia Maximo CD tatu za mechi za Yanga ambazo kocha huyo alizipokea na kuangalia ubora wa nyota wanaoitumikia klabu hiyo kwa sasa, ili akija ajue mahali pa kuanzia.
Taarifa ambazo Ukombozi Mimezipata kutoka kwa mmoja wa mabosi wa juu wa Yanga, imesema Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Nje ambaye ni mtu muhimu katika Kamati ya Usajili, Seif Ahmed ‘Seif Magari’ leo Alhamisi atakuwa ndani ya Uwanja wa Itaquerao jijini Sao Paulo, Brazil kutazama mechi ya ufunguzi ya Kombe la Dunia kati ya wenyeji na Croatia. Seif atatazama mechi zisizopungua tano za michuano hiyo.
Bosi huyo alisema Seif mara baada ya kushuhudia mchezo wa ufunguzi, atakutana na Maximo kujadiliana naye mambo mbalimbali ambayo ndiyo yatatoa picha halisi ya ujio wa kocha huyo mwenye msimamo mkali anayesimamia nidhamu kwa kiasi kikubwa.
Alisema baadhi ya mambo ambayo bosi huyo mwenye uzoefu mkubwa katika kusajili atazungumza na Maximo ni kuhusu ubora wa wachezaji na aina ya wachezaji anaowataka huku ajenda nyingine zikiwekwa siri nzito ingawa Mwanaspoti linajua kuwa hata suala la maandalizi ya kambi ni kitu kitakachojadiliwa katika kikao hicho.
“Hao wanaompinga Manji acha waendelee, bosi huku anaendelea na majukumu yake, Seif ameshaondoka nchini tangu jana (juzi Jumanne) yupo Brazil na kesho (leo Alhamisi) atakwenda kuangalia mechi ya ufunguzi ya Kombe la Dunia na kujadiliana mambo kadhaa na Maximo,” alisema bosi huyo,” kilisema chanzo chetu.
“Mwenyekiti (Manji) hataki maneno, Seif alikuwa anakwenda Brazil kwa safari zake, lakini hapo hapo akaunganishiwa na kazi za kwenda kufanya na Maximo kwa ajili ya timu na hilo linaweza kufanyika wakati wowote baada ya mchezo wa ufunguzi kwa kuwa Seif atakuwa huko kuangalia mechi zisizozidi tano.”
Wakati huohuo, Katibu wa Baraza la Wazee la Yanga, Ibrahim Akilimali, amesema amepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za wanachama 250 kujiorodhesha kwa lengo la kumpinga Manji baada ya kuongezewa muda wa uongozi kwa mwaka mmoja.
“Sisi tulikubaliana tukiwa wanachama 1,663 tena kwa moyo mmoja kwamba Mwenyekiti aendelee kwa mwaka mmoja, sasa iweje hawa waibuke na kupinga?” Alihoji Akilimali.
Akilimali aliwataka wanachama kutulia na kutazama jinsi uongozi unavyofanya kazi kuandaa kikosi kitakachoshiriki msimu ujao wa Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho Afrika.
Alisema Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) nalo halina mamlaka ya kubatilisha uamuzi huo wa mkutano wao kwani haukuwa uamuzi wa Manji binafsi bali ni wa wanachama wa klabu hiyo.

No comments: