Sunday 22 June 2014

Sita wafariki Dunua 12 wajeruhiwa

Wananchi wakiangalia daladala linalofanya safari kati ya Makumbusho na Kunduchi lililopata ajali eneo la Lugalo jijini Dar es Salaam jana. Watu sita walifariki dunia papohapo na 12 kujeruhiwa.

Watu sita wamefariki dunia na wengine 12 kujeruhiwa baada ya kutokea ajali iliyohusisha magari matatu, eneo la Lugalo, jijini Dar es Salaam jana.
Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Kipolisi Kinondoni Camillius Wambura, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kueleza kuwa ilitokea baada ya gari la abiria aina ya DCM kupoteza mwelekeo na kuhama njia, kisha kuligonga gari jingine la abiria lililokuwa upande wa pili, ambalo nalo liligonga gari lililokuwa mbele yake.
 “Kati ya waliofariki dunia, watatu ni wanawake na watatu wengine ni wanaume. Majeruhuri wanane kati ya 12 ni wanaume, wanne ni wanawake na wawili kati yao wamepelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi,” alisema Kamanda Wambura na kubainisha kuwa baada ya ajali hiyo madereva wa magari yote walikimbilia kusikofahamika.
Mkuu wa Hospitali ya Lugalo, Brigedia Jenerali Dk. Josiah Mekere alisema kuwa amepokea maiti za watu sita na majeruhi 12 na kwamba wawili walihamishiwa katika hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu zaidi akieleza kuwa wameumia zaidi maeneo ya kichwani.
‘’Wengi wamepata madhara kichwani, waliopelekwa Muhimbili (wawili) ni kwa ajili ya matibabu na uchunguzi zaidi kwa kuwa wanahitaji kufanyiwa kipimo cha CT scan,’’ alisema Dk. Mekere.
Akisimulia ajali ilivyotokea David Jailos, mkazi wa Tegeta aliyejeruhiwa mdomo na mguu katika ajali hiyo alisema: “Nikiwa katika daladala kutoka Ubungo kwenda Tegeta iliyokuwa katika mwendo kasi, dereva alitaka kulipita gari lililokuwa kulia kwake, lakini alipotokeza ili apite, akakuta kuna gari na kushindwa kurudi eneo lake kutokana na mwendo kasi, hivyo kuligonga kwa nyuma gari la mbele yake.
Alifafanua kuwa baada ya kuligonga, gari hilo nalo likagonga gari la mbele yake, hivyo ajali hiyo kuhusisha magari matatu, mawili ya abiria yaliyokuwa yakienda Kunduchi na jingine Tegeta.
Majeruhi mwingine, Jamila Mohamed mkazi wa Kigamboni aliyeumia mkono na bega alieleza kwa uchungu kuwa mtoto (Nasseri Nassoro) ni miongoni mwa abiria sita waliofariki kwenye ajali hiyo. Alisema kuwa alishtukia kioo kimemwangukia kikiwa kimesambaa na mtoto wake aliyekuwa amekaa naye kiti kimoja akiwa amemwangukia na baada ya kutolewa ndani ya gari, ndipo alipobaini kuwa amefariki dunia.
“Gari yetu ilikuwa imesimama, sikuelewa kilichoendelea zaidi ya kusikia mtikisiko mkubwa na mwanangu akaniangukia, baada ya hapo sikufahamu kilichoendelea hadi nilipofikishwa hapa hospitalini na kuona mwanangu ni miongoni mwa waliofariki katika ajali, ambayo siwezi kuielezea, “alisema Jamila.

No comments: