Saturday 7 June 2014

Maficho ya Makahaba Yajulikana

Idara ya Uhamiaji nchini Tanzania imegundua maficho ya wasichana waliosafirishwa kutoka nchi za India na Nepal mjini Dar es Salaam ambao wanatumikishwa katika biashara zisizo halali katika maeneo mbalimbali jijini humo

Katika siku tano zilizopita, idara ya uhamiaji jijini Dar es salaam inasema imewaokoa wasichana 51 raia wa India na Nepal waliohifadhiwa katika nyumba kadhaa na kutumikishwa katika biashara ya ngono na nyinginezo na kuwakamata wafanyabiashara wenye asili ya kiasia wanaotuhumiwa kusafirisha wasichana hao na kuwatumikisha hapa nchini

Mwishoni mwa mwezi uliopita wasichana wengine 17 walikutwa wamehifadhiwa katika nyumba moja eneo la Msasani jijini Dar es salaam kwa zaidi ya miezi mitatu huku wakidaiwa kutumika kwenye biashara ya ngono huku wengine 34 wakikamatwa jana  eneo la Mwananyamala jijini humo.

Wafanyabiashara waliotiwa nguvuni wanadai kuwa waliwaleta nchini humo wasichana hao kushiriki kucheza ngoma za asili kutoka mataifa yao katika club mbali mbali za usiku maarufu-Mujra na walikuwa wamehifadhiwa katika jengo moja huku pasi zao za kusafiria zikiwa zimechukuliwa na aliyetambuliwa kama meneja wao

Afisa Uhamiaji Mkaguzi wa mipaka  Doto Selasini amesema wasichana hao wenye umri wa chini ya miaka 26 waliingizwa nchini kwa njia halali kwa ahadi ya meneja wao kukaa nchini kwa siku 14 kwa ajili ya kushiriki ngoma za utamaduni wa mataifa yao, lakini wamekuwa wakitafutiwa wateja na baadae kulazimishwa kufanya vitendo vya ngono na kwamba wamefanikiwa kupata taarifa zao kupitia raia wema

Meneja wa wasichana hao Savio Menes ambaye naye ametiwa mbaroni na maafisa wa uhamiaji amesema wasichana hao aliwaingiza nchini kupitia wakala aliyeko nchini India na kudai kuwa walikuja kushiriki ngoma za utamaduni za bara la Asia

Hata hivyo wasichana wenyewe walipohojiwa na maafisa wa uhamiaji walikiri kuishi katika mazingira magumu na kufanya biashara isiyo halali na kwamba wako tayari kurejeshwa makwao India na Nepal. Wamedai kuwa wamekuwa chini ya ulinzi mkali huku wakitolewa usiku na kupelekwa katika mahoteli na kurejeshwa alfajiri na hawakuruhusiwa kuwa na mawasiliano na mtu yeyote.

Taarifa zilizopatikana  baadaye zilieleza kwamba wasichana 17 waliokamatwa Mei 30 wamesafirishwa na kurejeshwa makwao India na Nepal huku wafanyabiashara waliowaleta wakisubiri taratibu za kufunguliwa mashtaka

No comments: