Sunday 8 June 2014

Simba yasajili wasaidizi wa Tambwe wawili


KUNDI la wanachama matajiri wa Simba, Friends of Simba limegawanyika katika makundi mawili, moja linahangaikia usajili na lingine lipo bize na uchaguzi.
Lile linalopambana na usajili lina habari njema, muda wowote kuanzia leo Jumamosi litashusha nchini vifaa viwili kutoka Uganda tayari kwa mazungumzo ya mwisho ya usajili.
Chini ya Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Zacharia Hans Poppe na rafiki yake Geofrey Nyange ‘Kaburu’ ndiyo wanaotajwa kusimamia kazi hiyo ambapo siku yoyote kuanzia leo wanawashusha nchini wachezaji hao ambao wanaweza kucheza kama mido na straika.
Mmoja ni Joseph Mpande anayeichezea Vipers SC ya Uganda ambayo zamani ilikuwa ikijulikana kwa jina la Bunamwaya iliyopo katika nafasi ya nne katika ligi kuu ya nchi hiyo. Mchezaji huyo  alijumuishwa katika kikosi cha Uganda ‘The Cranes’ kilichoshiriki michuano ya wachezaji wa ndani ya Afrika CHAN iliyofanyika Afrika Kusini.
Mbali na Mpande aliyezaliwa miaka 21 iliyopita ambaye aliwahi kukunjana uwanjani na Haruna Niyonzima wakati wakitumikia mataifa yao, pia katika mchakato huo Simba imemnasa kiungo mchezeshaji Allan Kyambade kutoka klabu ya Express ya Kampala, Uganda.
“Nimeongea na mmoja wao kwa kuwa ni rafiki yangu, yeye amenithibitishia kuwa wanakuja Tanzania kumalizia mazungumzo yao. Kama unakumbuka huyo mshambuliaji aliwahi kutaka kupigana na Niyonzima wakati fulani akiichezea Cranes,” alisema mmoja wa nyota aliyepo katika kikosi cha Cranes.  Hans Poppe hakupatikana kwa  kuwa yuko safarini nchini Malaysia.
 Dili hiyo ikikamilika Simba itaachana na Wakenya wa Gor Mahia Rama Salim na Jerim Onyango waliozungumza na Kocha Logarusic.

No comments: