Saturday 7 June 2014

Hamisi Tambwe aipa masharti simba

Hamis Tambwe
STRAIKA namba moja wa Simba, Amissi Tambwe, yupo mapumzikoni kwao Burundi, lakini amesisitiza kwamba hatarudi Msimbazi mpaka uongozi mpya utakapomhakikishia anachotaka.
Tambwe ameliambia Maandishi wa habari kwa njia ya simu kutoka Bujumbura  kwamba jambo la kwanza atakalomweleza rais mpya wa Simba baada ya kumpongeza kwa ushindi ni kutaka alipwe fedha zake za usajili zilizobaki.
Lakini hataishia hapo atataka kujua kuwa mshahara wake wa Dola 800(Sh1.3milioni) utaongezwa kwa asilimia ngapi.
Mchezaji huyo aliyeifungia Simba mabao 19 katika msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara na kutwaa tuzo ya Mfungaji Bora, aliongeza kwamba atauambia uongozi huo ubadilishe baadhi ya vipengele na kuboresha mkataba wake vinginevyo hatakuja Dar es Salaam.
Alisema mgombea yeyote atakayeshinda nafasi ya urais kati ya wawili waliobaki awe Evans Aveva au Andrew Tupa waliopitishwa kuwania nafasi hiyo, atapaswa kuweka mambo sawa kwa vile ana ofa kadhaa alizopata DR Congo lakini anaisikiliza Simba kwanza.
“Simba wananijua mimi siyo msumbufu, lakini natambua kuwa sasa wapo katika uchaguzi, kwa nafasi yangu ya mchezaji hainihusu sana, ninachotaka kwa yeyote atakayeshinda katika urais anihakikishie mambo yangu kwanza,” alisema Tambwe ambaye habari za ndani zinadai kwamba ulipomalizika msimu uliopita alianza kushinikiza aongezewe mshahara baada ya kujigundua amezidiwa na wachezaji wengine wa kigeni.
“Sitaki maneno Simba wajue kwamba, nataka kuboreshewa mshahara wangu kwa maana nguvu na mchango wangu kwa timu wameviona. Jingine ni kupatiwa nusu yangu ya fedha za usajili kwa wakati pia hata mshahara uwe unakuja kwa wakati, hayo nitazungumza na huyo rais mpya atakayeshinda vinginevyo sitakuja kirahisi,”aliongeza mchezaji huyo.
Utafiti wa Mwanaspoti katika klabu zote 14 zinazoshiriki Ligi Kuu Bara umeonyesha kuwa klabu tatu; Azam, Yanga na Simba ndizo zinazolipa wachezaji wake mishahara mikubwa zaidi nchini.

No comments: