Tuesday 10 June 2014

Viongozi wa kimataifa wakutana kupinga ubakaji Vitani

Angelina Jolie ni mmoja wa wanaharakati maarufu wanaopinga dhuluma za kingono ikiwemo ubakaji
Viongozi wa kimataifa wanakutana jijini London kwa wiki nzima, kwa kongamano la kumaliza dhuluma za kimapenzi katika mataifa yanayokabiliwa na mizozo.
Mkutano huo, wa siku nne umeandaliwa na Waziri wa masuala ya nchi za kigeni wa Uingereza, William Hague na muigizaji maarufu na mjumbe maalum wa Umoja wa mataifa, Angelina Jolie.
Kongamano hilo linajiri huku mataifa kadhaa barani Afrika yakikabiliwa na changamoto ya kumaliza ubakaji unaotumiwa kama silaha ya kivita.
Ni mwanzo wa kuidhinishwa kampeni ya miaka miwili kutoa uhamasisho kuhusu kutumiwa kwa ubakaji na unyanyasaji wa kimapenzi kama silaha wakati wa vita.
Waandalizi wa kongamano hilo wanasema wanataka huu uwe wakati ambapo ulimwengu utazinduka na kutangaza kwamba unyanyasaji wa kimapenzi sio jambo lisiloweza kuepukika wakati wa vita.
'Uwajibikaji wa kimataifa'
Ujumbe ni ubakaji sio jambo lisiloweza kuepukika wakati wa vita.

Tangu William Hague na Angelina Jolie wazinduwe kampeni hiyo, mataifa mia moja na arobaini na nane yameidhinisha azimio la uwajibikaji wa kumaliza unyanyasaji huo wa kimapenzi katika mizozo.
Lakini lengo sasa ni kuchukua hatua madhubuti, kuendeleza uchunguzi na kuripotiwa kwa visa hivyo vya unyanyasaji wa kimapenzi.

Pia katika kutoa usaidizi zaidi kwa waathiriwa na kuhakikisha kuwa usawa wa kijinsia unahimizwa katika operesheni za siku zijazo za kulinda amani.
Kiwango cha jukumu hilo ni kikubwa: katika miaka ya tisaini, vita vya Bosnia vilisababisha kuwepo takriban waathiriwa elfu hamsini wa unyanyasaji wa kimapenzi.
Takriban miongo miwili tangu vita hivyo vimalizike, ni wahalifu wapatao 60 pekee walioshtakiwa.

No comments: